Maafisa Utawala na Rasirimali Watu 316 nchini wapimwa moyo
Afisa Muuguzi wa
Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) ambayo inasimamiwa na
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Nadia Zuberi akimpima shinikizo la damu
(BP) Afisa Rasirimali Watu aliyefika katika kliniki ya JKCI wakati wa Mkutano Mkuu
wa pili Jumuishi wa Jumuiya za Wataalamu wa Utawala na Usimamizi wa Rasirimali
Watu katika Utumishi wa Umma Tanzania uliomalizika jana katika Kituo cha
Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC). Jumla ya maafisa Utawala na Rasirimali
Watu 316 wamepima moyo.
Daktari wa Hospitali ya
Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) ambayo inasimamiwa na Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) Adda Justine akimpa ushauri Afisa Rasirimali Watu aliyefika
katika kliniki ya JKCI wakati wa Mkutano Mkuu wa pili Jumuishi wa Jumuiya za
Wataalamu wa Utawala na Usimamizi wa Rasirimali Watu katika Utumishi wa Umma
Tanzania uliomalizika jana katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha
(AICC). Jumla ya maafisa Utawala na Rasirimali Watu 316 wamepima moyo.
Uchunguzi huo
umefanyika kwa siku tatu wakati wa Mkutano Mkuu wa pili Jumuishi wa Jumuiya za
Wataalamu wa Utawala na Usimamizi wa Rasilimali Watu katika Utumishi wa Umma
Tanzania uliomalizika jana katika Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha
(AICC) jijini Arusha.
Akielezea kuhusu
mwitikio wa maafisa hao kufanya uchunguzi wa afya Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi
Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) inayosimamiwa na Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Salehe Mwinchete alisema mwitikio umekuwa
mkubwa na wenye tija kwa maafisa Utawala na Rasirimali Watu nchini.
“Baada ya kuwafanyia
uchunguzi wa afya baadhi ya maafisa Utawala na Rasirimali Watu tumewapa rufaa kufika
katika Hospitali zetu kwaajili ya uchunguzi zaidi kutokana na kuona viashiria
ambavyo vinahitaji uchunguzi zaidi”, alisema Dkt. Salehe
Dkt. Salehe alisema
inapotokea fursa kama hiyo ya kupima afya eneo la kazi ni vizuri watumishi
wakaitumia vizuri kwani wanapokuwa katika maeneo yao ya kazi wanakosa muda wa
kufika hospitali kwaajili ya kufanya uchunguzi wa afya.
“JKCI tumekuwa mstari
wa mbele kuwafikishia watumishi wa umma na sekta binafsi huduma za uchunguzi wa
afya wakati wa mikutano mbalimbali lakini pia hata kuwafuata katika maeneo yao ya
kazi, jitihada zote hizi tunazofanya tunataka kuhakikisha kuwa tunailinda jamii
na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo ya moyo”, alisema Dkt. Salehe
Nao maafisa Utawala na
Rasirimali Watu walioshiriki katika mkutano huo wameiomba JKCI kuendela kutoa
elimu ya magonjwa ya moyo ili kuliokoa taifa la Tanzania na changamoto ya
magonjwa hayo.
Maafisa hao walisema
Serikali ya Tanzania ina mchango mkubwa katika kuhakikisha watu wake wanakuwa
salama ndio maana imefanya uwekezaji mkubwa katika sekta ya afya na kuhakikisha
elimu kuhusu kinga dhidi ya magonjwa mbalimbali inawafikia wananchi.
Comments
Post a Comment