JKCI yapongezwa kupambana dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza


Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Edna Kajuna akitoa elimu kuhusu magonjwa ya moyo kwa wanafunzi wa chuo cha KAM College walipotembelea banda la Taasisi hiyo wakati wa maonesho ya Dental Expo 2026 yaliyomalizika leo katika viwanja vya Mlimani City vilivyopo jijini Dar es Salaam.




Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Edna Kajuna akitoa elimu ya namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza kwa wananchi waliotembelea banda la Taasisi hiyo wakati wa maonesho ya Dental Expo 2026 yaliyomalizika leo katika viwanja vya Mlimani City vilivyopo jijini Dar es Salaam.

Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Edna Kajuna akimuonesha jinsi moyo unavyokuwa mwananchi aliyetembelea banda la JKCI wakati wa maonesho ya Dental Expo 2026 yaliyomalizika leo katika viwanja vya Mlimani City vilivyopo jijini Dar es Salaam.

Na JKCI

*********************************************************************************************************

Washiriki wa maonesho ya Dental Expo 2026 wameipongeza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kuendelea kutoa elimu ya namna ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza na kutoa motisha kwa jamii kufuata mtindo bora wa maisha.

Pongezi hizo zimetolewa leo wakati wa kuhitimisha maonesho ya Dental Expo 2026 yaliyokuwa yakifanyika katika viwanja vya Mlimani City vilivyopo jijini Dar es Salaam. 

Washiriki hao walisema elimu waliyoipata kupitia maonesho hayo itawasidia kuzingatia mtindo bora wa maisha na kuisaidia jamii inayowazunguka kutambua magonjwa hayo ili isiwe sehemu ya kupata magonjwa ya moyo.

Shadrack Mgeni mkazi wa Tanga aliiomba JKCI inapopata nafasi ipeleke huduma na elimu kuhusu magonjwa ya moyo mkoani Tanga kuisaidia jamii hiyo ili iweze kufuata mtindo bora wa maisha hasa katika masuala la lishe.

Kwa upande wake Purity Wanjiru kutoka Nairobi nchini Kenya alisema Tanzania imekuwa mfano mzuri katika kutoa elimu dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza na kuitaka Kenya kuongeza nguvu ya kutoa elimu ya magonjwa hayo, na madhari ya vilevi kuokoa vijana ambao ni taifa la kesho.

“Nimefurahi kuifahamu JKCI kabla sijaondoka Tanzania nitafika JKCI katika tawi lake la Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) kwaajili ya kufanya uchunguzi wa afya kwani dalili za magonjwa ya moyo nilizoambiwa hapa moja wapo imekuwa ikinipata lakini sikuchukua hatua”, alisema Purity.

Akielezea muitikio wa wananchi kufika katika banda la Taasisi hiyo kupata elimu Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Edna Kajuna alisema mwitiko wa rika la vijana umekuwa mkubwa ukilinganishwa na watu wazima hivyo kuonesha kuwa vijana wameanza kutambua umuhimu wa kuyajua na kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza.

“Vijana wengi wamevutiwa na kampeni ya “Jua Namba Zako” na kuona umuhimu wa kwenda kubadilisha mfumo wao wa maisha, kama kweli watakuwa mstari wa mbele kubadilika itapunguza idadi ya watu wanaopata magonjwa yasiyoambukiza”, alisema Edna.

Edna alisema kampeni ya “Jua Namba Zako” inalenga kuihamasisha jamii kujua viashiria vitano vinavyoweza kusababisha magonjwa yasiyoambukiza ili iweze kujikinga na magonjwa hayo na kutoathiri nguvu kazi ya taifa.

“Tumeshuhudia matukio ya vifo vya gafla vinavyojitokeza katika jamii ambapo sababu mojawapo ni kutokufanya uchunguzi wa mapema na kufahamu hali zetu kiafya”, alisema Edna.


Comments

Popular posts from this blog

Kutoka miaka 22 hadi kustaafu: Safari ya Lemmah yatoa somo kwa Watumishi wa Umma

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi