Shinikizo la Damu laua kimyakimya, JKCI yatoa wito wa hatua za haraka
.jpeg)
Afisa Muuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Kliniki ya Oysterbay Noel Mushi akimpima shinikizo la damu mwandishi wa Azam TV Esterbella Malisa wakati wa zoezi la upimaji afya ikiwa ni kuelekea katika Maadhimisho ya Siku ya Shinikizo la Juu la Damu Duniani yanayofanyika kila mwaka tarehe 17 Mei.
***************************************************************************************************************************************************************************************************
Mtindo usiofaa wa maisha umetajwa kuwa miongoni mwa sababu kuu zinazochangia kuongezeka kwa tatizo la shinikizo la juu la damu ugonjwa unaoendelea kuwa tishio kubwa la afya duniani na kusababisha vifo vya watu zaidi ya milioni 10 kila mwaka.
Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Afya Duniani (WHO) za mwaka 2023
takribani watu bilioni 1.28 duniani
wenye umri wa miaka 30 hadi 79 wanaishi na ugonjwa wa shinikizo la juu
la damu huku karibu theluthi mbili ya wagonjwa hao wakiishi
katika nchi zenye kipato cha chini na cha kati ikiwemo nchi nyingi za Afrika.
Kauli hiyo imetolewa leo na Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati
akizungumza na waandishi wa habari katika Kliniki ya Oysterbay jijini Dar es
Salaam kuelekea maadhimisho ya Siku ya Shinikizo la Juu la Damu Duniani yanayoadhimishwa
kila mwaka Mei 17.
Dkt. Kisenge ambaye pia ni Daktari Bingwa wa
Magonjwa ya Moyo alisema jamii inapaswa kuchukua hatua za mapema kujikinga
dhidi ya ugonjwa huo huku akieleza kuwa
shinikizo la juu la damu lisipodhibitiwa linaweza kusababisha madhara makubwa
ikiwemo vifo na kupunguza nguvu kazi ya taifa.
"Wananchi
wanapaswa kujua namba zao za shinikizo la damu kwani hatua hiyo rahisi inaweza
kusaidia kugundua ugonjwa mapema, kuanza matibabu kwa wakati na kuepuka madhara
makubwa yanayoweza kujitokeza”. alisema Dkt. Kisenge.
Alisisitiza umuhimu wa kuzingatia mtindo bora
wa maisha kwa kufanya mazoezi mara kwa mara, kula lishe bora yenye matunda na
mboga za majani, kupunguza matumizi ya chumvi, pamoja na kuacha matumizi ya
sigara na unywaji wa pombe kupita kiasi ili kujikinga dhidi ya magonjwa
yasiyoambukiza.
Dkt. Kisenge alieleza kuwa shinikizo la juu la
damu ni miongoni mwa magonjwa yasiyoambukiza yanayoweza kusababisha madhara
makubwa ikiwemo kiharusi, matatizo ya moyo na figo kushindwa kufanya kazi
vizuri hali inayochangia pia kudorora kwa uzalishaji na maendeleo ya taifa.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Magonjwa ya Moyo
wa JKCI, Dkt. Tatizo Waane alisema ugonjwa wa shinikizo la juu la damu
umeendelea kuwa "muuaji wa kimyakimya" kutokana na wananchi wengi
kutokuwa na uelewa wa kutosha kuhusu dalili na madhara yake.
"Licha ya
ugonjwa huu kuua kimyakimya unaweza
kudhibitiwa ikiwa wananchi watachukua tahadhari kwa kupima afya zao mapema,
kutumia dawa kwa usahihi na kutositisha matumizi ya dawa bila ushauri wa
daktari", alisema Dkt.
Waane.
Aliongeza kuwa katika mkutano huo JKCI pia
ilitoa huduma ya uchunguzi wa afya pamoja na elimu kupitia kampeni ya “Jua
Namba Zako”, inayolenga kuhamasisha wananchi kufahamu viwango vya afya zao
ikiwemo shinikizo la damu, kiwango cha sukari kwenye damu, uwiano wa uzito na
urefu pamoja na kiwango cha mafuta mwilini.
Akisisitiza umuhimu wa kauli mbiu ya mwaka huu
isemayo: "Kudhibiti shinikizo la damu kwa pamoja: Pima shinikizo lako
la damu mara kwa mara ushinde ugonjwa huu unaoua kimyakimya", Dkt.
Waane alisema jamii na sekta ya afya zinapaswa kushirikiana katika kukabiliana
na tatizo hilo.
Katika mkutano huo waandishi wa habari
walipata fursa ya kupima afya zao bila malipo ambapo baadhi yao walieleza
kufurahishwa na huduma hiyo kwa kuwa imewasaidia kutambua hali zao za afya na
kuchukua hatua za kuimarisha mtindo bora wa maisha.
"Huduma hii imekuwa msaada mkubwa kwetu kwani kutokana na majukumu ya kazi mara nyingi tunakosa nafasi ya kufika vituo vya afya na kujua hali zetu kiafya. Nashauri huduma hizi ziendelee kutolewa hata kwenye maeneo yetu ya kazi ili watu wengi zaidi wajue namba zao", alisema Esterbella Malisa wa Azam TV.
.jpeg)
Comments
Post a Comment