Shiriki CRDB Bank Marathon kwa ajili ya kuchangisha fedha za matibabu ya moyo kwa watoto wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akizungumza kuhusu asilimia kubwa ya watoto wanaotibiwa katika Taasisi hiyo kusumbuliwa na  magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo wakati wa mkutano wa waandishi wa habari  uliofanyika leo jijini Dar es Salaam uliohusu mbio za CRDB Bank Marathon.

Viongozi wa Taasisi mbalimbali ambazo zitashiriki katika mbio za CRDB Bank Marathon wakimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB   Abdulmajid  Nsekela mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa waandishi wa habari uliohusu mbio hizo ambazo lengo lake ni  kuchangisha fedha za matibabu ya moyo kwa watoto wanaotoka katika familia zisizo na uwezo wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Viongozi wa Taasisi mbalimbali ambazo zitashiriki katika mbio za CRDB Bank Marathon wakiwa katika picha ya pamoja  mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa waandishi wa habari uliohusu mbio hizo ambazo lengo lake ni  kuchangisha fedha za matibabu ya moyo kwa watoto wanaotoka katika familia zisizo na uwezo wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB   Abdulmajid  Nsekela akizungumza na waandishi wa habari kuhusu mbio za CRDB Bank Marathon ambazo lengo lake ni  kuchangisha fedha za matibabu ya moyo kwa watoto wanaotoka katika familia zisizo na uwezo wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).



Benki ya CRDB imeandaa mbio za CRDB Bank Marathon kwa ajili ya kuchangisha fedha za matibabu ya moyo kwa watoto wanaotoka katika familia zisizo na uwezo wa kuchangia gharama za matibabu  wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mama Samia  Hassan  Suluhu anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika mbio hizo zitakazofanyika tarehe 16/08/2020 kuanzia saa 12 asubuhi jijini Dar es Salaam.

Akizungumza katika mkutano wa waandishi wa Habari uliofanyika leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Mtendaji wa Benki ya CRDB, Abdulmajid Nsekela alisema lengo la kuandaa mbio hizo ni kuleta tabasamu kwa watoto wenye matatizo ya moyo pamoja na familia zao.

Nsekela alisema licha ya kuandaa mbio hizo Benki ya CRDB imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha watoto wenye matatizo ya moyo ambao wanatoka katika familia zisizokuwa na uwezo wa kuchangia gharama za matibabu wanapata matibabu kama watoto wengine.

“Hadi sasa Benki yetu imechangia   kiasi cha shilingi milioni 100 fedha ambazo zilitumika kulipa gharama za upasuaji wa moyo kwa watoto 50”.

“Kiasi cha fedha kitakachopatikana katika mbio hizi kitaenda kulipia gharama za upasuaji wa moyo  kwa watoto wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete”, alisema Nsekela.

Mkurugenzi huyo  Mtendaji alisema kila mshiriki wa mbio hizo ambazo zitafanyika Tanzania nzima mahali ambako benki hiyo ipo (Virtual Marathon)  atachangia kiasi cha shilingi 30,000/= na kutakuwa na mbio za kilomita 5, 10 na 21 pamoja na mbio za baiskeli.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi aliipongeza Benki ya CRDB kwa kutambua haki ya mtoto ya kupata matibabu na kuamua kuwasaidia watoto wanaosumbuliwa na magonjwa ya moyo wanaotibiwa JKCI.

Prof. Janabi alisema asilimia kubwa ya watoto wanaotibiwa katika Taasisi hiyo wanasumbuliwa na magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo ambayo ni matundu na mishipa ya damu ya moyo kutokuwa katika mfumo  wa kawaida.

Naye Meneja wa kanda ya Mashariki wa mpango wa Taifa wa damu salama Dkt. Kokuhabwa Mkurasi aliwaomba wananchi wenye afya njema kujitokeza kwa wingi kuchangia damu siku hiyo ya CRDB Bank Marathon.

Dkt. Kokuhabwa alisema wataalamu kutoka katika ofisi yake watakuwepo kuanzia asubuhi hadi mwisho wa mbio hizo ili wananchi waweze kuchangia damu kwani wanahitaji damu za kutosha.

Sambamba na mbio hizo ambazo zitafanyika katika uwanja wa Farasi  Oster bay  jijini Dar es  Salaam kutakuwepo na huduma za ushauri na upimaji wa magonjwa ya moyo, homa ya ini pamoja na uchangiaji wa damu.

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari