Bilionea
Saniniu Laizer namna ambavyo wananchi wamekua na mwitikio mkubwa wa kufanya
uchunguzi wa afya ya moyo katika banda la JKCI alipotembelea banda hilo kuona
huduma zinazotolewa wakati wa Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa leo
Jijini Dar es Salaam.
Bilionea
Saniniu Laizer aipongeza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa huduma za
ushauri na upimaji wa magonjwa ya moyo wanazozitoa kwa wananchi wanaotembelea banda
la Taasisi hiyo wakati wa Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Sabasaba
yanayoendelea Jijini Dar es Salaam.
Pongezi
hizo amezitoa leo alipotembelea banda la JKCI kwa ajili ya kuona huduma
wanazozitoa pamoja na kupata elimu ya lishe na magonjwa ya moyo.
Lazier
alisema huduma zinazotolewa ni nzuri kwani zinaokoa maisha ya watu wenye
matatizo ya moyo ambao baada ya afya zao kuimarika watakua sehemu ya kukuza
uchumi wa nchi yetu.
Kwa
upande wake Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Pedro Pallangyo alimshukuru
bilionea Laizer kwa kutembelea katika banda lao na kujionea huduma mbalimbali
za upimaji na ushauri wa magonjwa ya moyo zinazotolewa.
Dkt. Pedro
ambaye pia ni mtafiti wa magonjwa ya moyo alisema ugeni wa Bilionea Laizer
katika banda la hilo utawavutia wananchi wengi kufanya vipimo vinavyotolewa na
Taasisi hiyo.
Dkt.
Pedro alisema mwitikio wa wananchi katika banda la JKCI kwa ajili ya kufanya
uchunguzi umekua ukiongezeka mwaka hadi mwaka kwa miaka minne ambayo taasisi
hiyo imeshiriki maonyesho Sabasaba.
Mbali na
huduma za upimaji wa afya ya moyo na magonjwa mengine sugu, Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete pia imejikita kuhakikisha inatoa elimu ya kutosha kwa jamii ili
iweze kufahamu sababu hatarishi za magonjwa ya moyo na magonjwa mengine sugu.
“Tulichojifunza
katika ushiriki wetu kwenye maonyesho haya ni kuwa wananchi wengi wana shauku
ya kujua afya zao ila wengi hawajui ni wapi na kwa namna gani wataweza kufika
sehemu stahiki kufanya uchunguzi.
“Uzito
mkubwa na shinikizo la damu yameonekana kuwa ni matatizo mawili makubwa ambayo
yanakuwa kwa kasi mwaka hadi mwaka katika jamii ya kitanzania.
Ni rai
yetu kwa taifa zima kuwa kinga ni bora kuliko tiba hivyo jamii nzima ivalie
njuga sababu hatarishi za magonjwa sugu ikihusisha uzito sahihi, ulaji unaofaa,
mazoezi ya mara kwa mara, kunywa pombe kwa kiasi au kuacha kabisa, na kutovuta
sigara,”. alisema Dkt. Pedro.
Hadi sasa
jumla ya watu 1940 wamefanyiwa vipimo katika banda hilo ambapo vipimo vya
viashiria vya magonjwa ya moyo ambavyo ni uzito, urefu, sukari mwilini na shinikizo
la damu (BP) vimefanyika bila malipo na vipimo vya damu, ECG na ECHO wananchi
wanachangia kiasi kidogo cha fedha.
Comments
Post a Comment