Maafisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) wakiwapima wananchi waliotembelea banda la JKCI lililopo ukumbi wa
Karume shinikizo la damu (BP) pamoja na kutoa ushauri wa magonjwa ya moyo
wakati wa Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam.
ASILIMIA 68 ya waanchi kati ya 1500
waliojitokeza kujiandikisha ili kuonwa na madaktari kwenye banda la Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), katika maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya
Dar es Salaam (sabasaba), wamekutwa na uzito uliopitiliza (obesity).
Uzito uliopitiliza ni kiashiria cha hatari
kwani wananchi hao wapo kwenye uwezekano mkubwa wa kupata magonjwa mbalimbali
yasiyo ya kuambukiza (NCD’s), ikiwamo magonjwa ya moyo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana
katika banda la JKCI, lililopo ndani ya jengo la Karume, Daktari kutoka JKCI Winnie
Masakuya, alisema asilimia 58 kati ya watu waliotembelea banda la JKCI ni
wanawake huku wanaume wakiwa asilimia 42.
“Tangu Julai mosi, mwaka huu hadi kufikia leo
(Julai 8, 2020) tumeona watu wapatao 1,500, kati ya hao asilimia 68 tumewakuta
na uzito uliopitiliza huku asilimia 40 tumewakuta na tatizo la shinikizo la juu
la damu (high blood pressure).
“Asilimia saba tumewakuta na kisukari bila ya
wao kujijua hali zao kabla ya kufika kwenye banda letu, na asilimia 18
tuliwakuta wana kiwango kikubwa cha mafuta kwenye damu (cholesterol’)”
alibainisha.
Dk. Masakuya alisema watu 500 kati ya hao
1,500 walioonwa, wamefanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo kwa kutumia kipimo
cha ECG na ECO ambavyo wanavyo ndani ya banda JKCI.
“Maonesho
haya ni fursa kwa wananchi, kwa sababu kwa kuja kwao hapa kwenye banda letu,
wameonwa na madaktari bingwa na waliogundulika kuwa na matatizo tumewapa rufaa
kwenda kwenye taasisi yetu kwa matibabu zaidi.
“Aidha, wananchi waliofika kwenye banda letu
wamepata fursa ya kupata elimu ya lishe kutoka kwa wataalamu wetu wa lishe,
namna gani wanaweza kulinda afya zao kwa kuzingatia mfumo bora wa maisha, ulaji
unaofaa na hivyo kuepuka magonjwa mbalimbali yasiyo ambukiza hususan magonjwa
ya moyo,” alisema.
Aliongeza “Nawasihi Watanzania waendelee kuja
kwenye banda letu hapa sabasaba hadi tarehe 13 Julai mwaka huu, hii ni fursa
nzuri ya kuweza kujifunza mtindo wa maisha ulio mzuri ili waweze kutunza afya
za mioyo yao, isichoke mapema.
Naye mwananchi aliyetembelea banda la JKCI
katika Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam Zainab Hassan
ameshukuru kwa kupatiwa huduma nzuri na ya wakati katika banda la JKCI na
kuomba fursa za upimaji wa magonjwa ya moyo kwa wananchi kama zinazofywa katika
banda la Sabasaba ziweze kuongezwa ili wananchi wengi waweze kufahamu afya zao
hasa afya ya moyo.
“Nimefurahi sana kufanyiwa uchunguzi wa afya
ya moyo wangu na kukutwa salama, sikutarajia kama siku moja nitapima afya ya
moyo wangu, hii ni fursa kubwa sana kwetu wananchi kujitokeza na kuchunguza
afya zetu”.
Comments
Post a Comment