ASILIMIA 68 WAKUTWA NA UZITO ULIOPITILIZA

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimpima mwananchi alietembelea banda la JKCI lililopo ukumbi wa Karume shinikizo la damu (BP) pamoja na kutoa ushauri wa magonjwa ya moyo wakati wa Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam.

Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) George Msabila akielezea vifaa mbalimbali vinavyotumika katika chumba cha upasuaji mdogo wa moyo kwa wananchi waliotembelea banda la JKCI katika Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam

Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mary Haule akimpima kiwango cha sukari mwilini  mwananchi aliyetembelea banda la JKCI lililopo ukumbi wa Karume wakati wa  maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam.

Maafisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakiwapima wananchi waliotembelea banda la JKCI lililopo ukumbi wa Karume shinikizo la damu (BP) pamoja na kutoa ushauri wa magonjwa ya moyo wakati wa Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam.

ASILIMIA 68 ya waanchi kati ya 1500 waliojitokeza kujiandikisha ili kuonwa na madaktari kwenye banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), katika maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (sabasaba), wamekutwa na uzito uliopitiliza (obesity).

Uzito uliopitiliza ni kiashiria cha hatari kwani wananchi hao wapo kwenye uwezekano mkubwa wa kupata magonjwa mbalimbali yasiyo ya kuambukiza (NCD’s), ikiwamo magonjwa ya moyo.

Akizungumza na waandishi wa habari jana katika banda la JKCI, lililopo ndani ya jengo la Karume, Daktari kutoka JKCI Winnie Masakuya, alisema asilimia 58 kati ya watu waliotembelea banda la JKCI ni wanawake huku wanaume wakiwa asilimia 42.

“Tangu Julai mosi, mwaka huu hadi kufikia leo (Julai 8, 2020) tumeona watu wapatao 1,500, kati ya hao asilimia 68 tumewakuta na uzito uliopitiliza huku asilimia 40 tumewakuta na tatizo la shinikizo la juu la damu (high blood pressure).

“Asilimia saba tumewakuta na kisukari bila ya wao kujijua hali zao kabla ya kufika kwenye banda letu, na asilimia 18 tuliwakuta wana kiwango kikubwa cha mafuta kwenye damu (cholesterol’)” alibainisha.

Dk. Masakuya alisema watu 500 kati ya hao 1,500 walioonwa, wamefanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo kwa kutumia kipimo cha ECG na ECO ambavyo wanavyo ndani ya banda JKCI.

“Maonesho haya ni fursa kwa wananchi, kwa sababu kwa kuja kwao hapa kwenye banda letu, wameonwa na madaktari bingwa na waliogundulika kuwa na matatizo tumewapa rufaa kwenda kwenye taasisi yetu kwa matibabu zaidi.

“Aidha, wananchi waliofika kwenye banda letu wamepata fursa ya kupata elimu ya lishe kutoka kwa wataalamu wetu wa lishe, namna gani wanaweza kulinda afya zao kwa kuzingatia mfumo bora wa maisha, ulaji unaofaa na hivyo kuepuka magonjwa mbalimbali yasiyo ambukiza hususan magonjwa ya moyo,” alisema.

Aliongeza “Nawasihi Watanzania waendelee kuja kwenye banda letu hapa sabasaba hadi tarehe 13 Julai mwaka huu, hii ni fursa nzuri ya kuweza kujifunza mtindo wa maisha ulio mzuri ili waweze kutunza afya za mioyo yao, isichoke mapema.

Naye mwananchi aliyetembelea banda la JKCI katika Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam Zainab Hassan ameshukuru kwa kupatiwa huduma nzuri na ya wakati katika banda la JKCI na kuomba fursa za upimaji wa magonjwa ya moyo kwa wananchi kama zinazofywa katika banda la Sabasaba ziweze kuongezwa ili wananchi wengi waweze kufahamu afya zao hasa afya ya moyo.

“Nimefurahi sana kufanyiwa uchunguzi wa afya ya moyo wangu na kukutwa salama, sikutarajia kama siku moja nitapima afya ya moyo wangu, hii ni fursa kubwa sana kwetu wananchi kujitokeza na kuchunguza afya zetu”. 


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari