WATAALAM WABOBEZI WA MOYO WAPANDIKIZA KIFAA CHA KUUSAIDIA MOYO KUFANYA KAZI VIZURI BILA KUTUMIA MTAMBO WA CATHLAB
Kwa mara ya
kwanza wataalamu wabobezi wa moyo na wazibuaji wa mishipa ya damu ya moyo
wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wamepandikiza kifaa cha kuusaidia moyo
kufanya kazi vizuri (Pacemaker) nje ya Taasisi hiyo bila ya kutumia mtambo wa
Cathlab.
Mgonjwa aliyewekewa
pacemaker alipata ajali iliyosababisha uti wa mgongo kupata
shida na kusababisha baadhi ya viungo vya mwili kupoteza uwezo wa
kufanya kazi ikiwemo mishipa ya damu inayoratibu uwezo wa moyo
kutengeneza mapigo yake (Sympathetic Waves System).
Akizungumza na waandishi wa
habari leo jijini Dar es Salaama daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete Yona Gandye alisema kutoka na tatizo alilolipata mgonjwa
mara baada ya kupata ajali mapigo ya moyo yalishuka hadi kufikia 30
kwa dakika na mgonjwa kuonesha dalili za ukosefu wa mahitaji
muhimu ya mwili yanayosambazwa na mapigo ya moyo
ambayo ni oxygen , virutubisho, madini na chakula.
“Mgonjwa huyo alikuwa
amelazwa katika Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI) na alihitaji huduma ya haraka
ya kuwekewa kifaa kisaidizi ambacho kinausaidia moyo kufanya kazi vizuri
(Pacemaker) ili mapigo yafikie 60 hadi 100 ambayo ni mapigo ya
kawaida ya moyo”.
“Kutokana na mazingira ya
mgonjwa kutoweza kuhamishika kutoka MOI na kuletwa JKCI ilibidi tumfuate
kumwekea Pacemaker. Tulitumia vyumba vya upasuaji vya kawaida kutumia mashine
tofauti na yetu ambayo yao inajulikana kwa jina la C-ARM”, alisema Dkt. Gandye.
Dkt. Gandye alisema huduma
hiyo wameitoa kwa mara ya kwanza nje ya Taasisi hiyo na kuifanya bila ya
kutumia mtambo wa Cathlab (Catheterization Laboratory) ambao ni maabara ya
uchunguzi wa mishipa ya damu ya moyo na tiba
Alimalizia kwa kusema
ushirikiano wa JKCI na MOI na utayari wa JKCI kuhudumia wagonjwa nje ya Taasisi
hiyo ulisaidia kufanyika kwa huduma hiyo kwa haraka. Aliziomba Hospitali
kuwasiliana na JKCI kama watapata mgonjwa mwenye matatizo ya moyo
ambaye hawezi kuhamishika ili waone namna ambavyo wataweza kumsaidia
mgonjwa huyo kwa kumfuata mahali alipo.
Comments
Post a Comment