Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto
wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Naizihijwa Majani akimpima mwananchi alietembelea banda la JKCI
lililopo ukumbi wa Karume shinikizo la damu (BP) pamoja na kutoa ushauri wa
magonjwa ya moyo wakati wa Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es
Salaam.
Wagonjwa saba waliowahi kwenda kufanyiwa
upasuaji wa moyo nje ya nchi ambao hawajaweza kurudi huko kuhudhuria kliniki
zao, ‘wamekimbilia’ katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI),
lililopo kwenye maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa -SABASABA.
Katika banda la JKCI wameweza kuonwa na
wataalamu wabobezi wa magonjwa ya moyo na kisha kupatiwa utaratibu wa namna
watakavyoweza kuanza kuhudhuria kliniki katika taasisi hiyo iliyopo Upanga,
Jijini Dar es Salaam.
Sambamba na hilo, wananchi waliotembelea
banda la JKCI lililopo katika ukumbi wa Karume wameweza kufanyiwa uchunguzi wa
magonjwa ya moyo kwa kufanyiwa vipimo vya kisasa vya Electoral Cardiograph (ECG)
na Echo Cardiograph (ECHO).
Kwa upande wake Fundi Sanifu wa Moyo
(Cardiovasicular technologist), Abubakar Dalidali alisema mwitiko wa wananchi
umekuwa mkubwa hivyo kuonesha kuwa wananchi wengi wanauhitaji wa kuchunguza
afya zao mara kwa mara.
“Wananchi saba waliowahi kufanyiwa upasuaji
nje ya nchi, hawajaweza kurudi walikofanyiwa upasuaji kuhudhuria kliniki, hivyo
kufika katika banda la JKCI na kuchunguzwa tena mioyo yao inavyoendelea na kuweza
kujua namna gani wataweza kuanza kuhudhuria kliniki kwenye taasisi yetu,
tumewaelekeza,” alisema Dalidali.
Dalidali aliongeza kuwa kwenye banda la JKCI
kuna vipimo mbalimbali vya uchunguzi wa afya ya moyo, kikiwemo kipimo cha Electoral
Cardiograph (ECG) kinachochunguza mpitisho wa umeme unaopita kwenye moyo pamoja
na kipimo cha Echo Cardiograph kinachochunguza utendaji mzima wa moyo.
“Kutegemeana
na utaratibu wake ulivyopangwa mapigo ya moyo huwa kati ya wastani wa mapigo 60
hadi 100 kwa mtu mzima, hivyo ECG ni kipimo cha kwanza ambacho kinaweza
kuonesha kama mapigo ya moyo yamezidi zaidi ya 100 na kuonesha kuwa kuna tatizo
ama yamepungua chini ya 60 na kuwa tatizo pia,” alisema.
“Tuliowafanyia uchunguzi wamegawanyika katika
makundi mawili, wapo ambao majibu yao yameonekana hawana shida na wapo ambao yameonesha
wanahitaji taratibu zaidi za kimatibabu, tumewapa rufaa kufika JKCI kwa ajili
ya matibabu zaidi,” alisema Dalidali.
Mkazi wa Mbagala Jijini Dar es Salaam Fatuma
Ally amesema kuwa katika maisha yake hakuwahi kuwaza kuwa ipo siku atachunguza
moyo wake kama uko salama lakini baada ya kusikia kuwa wataalamu wa afya kutoka
JKCI wapo katika maonesho ya Sabasaba akatumia fursa hiyo kutembelea banda hilo
na kufanya vipimo vya kuchunguza moyo wake.
“Nimefurahi
kupata majibu kutokana na vipimo nilivyofanya vya ECG na ECHO kuwa moyo wangu
uko samala, umeme wangu wa moyo unafanya kazi vizuri na mapigo yangu ya moyo
yapo sawa, sasa naenda kubadilisha mfumo wangu wa maisha kama wataalam wa lishe
walivyonishauri ili moyo wangu uendelee kuwa salama” alisema Fatuma
|
Comments
Post a Comment