Wataalam wa maabara kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) wakipima vipimo vya damu kwa ajili ya kuangalia magonjwa ya moyo
kwa wananchi waliofika katika banda hilo kwa ajili ya kupima afya zao wakati wa
Maonesho ya 44 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam
Wananchi waliotembelea banda la Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) katika Maonesho ya Sabasaba wamevutiwa na uwepo wa
chumba cha mfano cha kuhudumia wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum (ICU)
pamoja na mashine maalum ya kupumulia ‘ventilator’.
Mashine hiyo ndiyo ambayo hutumika kusaidia
mgonjwa mwenye shida ya upumuaji kuweza kupumua vema baada ya kufanyiwa
upasuaji mkubwa ikiwemo upasuaji wa moyo.
Mkazi wa Buguruni, Said Abdallah alisema
amefurahi kuona mashine hiyo kwa macho yake, kwani hapo kabla alisikia kwenye
vyombo vya habari ikielezwa kwamba ni msaada mkubwa kwa watu wenye shida ya
upumuaji.
“Katika kipindi hiki cha Corona, nilisikia
wakisema mashine ya ‘ventilator’ inasaidia kuokoa maisha, sasa sikuwa nimewahi
kuiona mashine hiyo, ndiyo maana leo unaona nina furaha kubwa, nimeiona hapa
kwenye banda la JKCI, SABASABA,” alisema
Abdallah.
Kwa upande wake Afisa Uuguzi kutoka JKCI,
Mary Haule akizungumza na waandishi wa habari alisema wananchi wengi wamevutiwa
na mashine ya ventilator na kuuliza maswali mengi hasa namna gani mashine hiyo
inaweza kusaidia kuokoa maisha.
“Sabasaba ya mwaka huu imekuwa ya tofauti
katika banda letu tumeweka mfano wa chumba cha ICU, tuna mfano wa binadamu
(mdoli) na tumekuja na mashine hii ya ‘ventilator’ tunawaonesha wananchi jinsi
tunavyomsaidia mgonjwa aliyetoka katika chumba cha upasuaji na kuwekewa mashine
hii kumsaidia kupumua,” alisema Haule.
Aliongeza “Mgonjwa tunayemuhudumia hapa
anakuwa bado hajaamka kutoka kwenye dawa ya usingizi, tunamsaidia mpaka hali
yake itakapoimarika na kutoka usingizini.
“Hivyo, tunatoa ufahamu kwa wananchi waweze
kuelewa kwamba katika Taasisi yetu tuna kitengo cha kusaidia wagonjwa mahututi
waliofanyiwa upasuaji na hapa tumekuja tu na baadhi ya mashine kwa ajili ya
maonesho, Lakini pale JKCI tunazo zaidi ya mashine 20 za Ventilator, wananchi
wamefurahi kuona mfano wa chumba hiki,” alisema Haule.
Wakati huo huo Mariam Kaisa ambaye ni Mkazi
wa Kiwalani alisema amepata elimu ya kutosha katika banda la JKCI kuhusu lishe
na umuhimu wa kufanya mazoezi ili kujikinga dhidi ya magonjwa ya moyo.
“Nimepima afya yangu, nimeambiwa moyo wangu
upo vizuri, nimeshauriwa kuzingatia kanuni za afya hasa ulaji unaofaa na mtindo
bora wa maisha ili nizidi kulinda afya ya moyo wangu,” alisema Mariam.
|
Comments
Post a Comment