Fanyeni kazi kwa uweledi na ufanisi katika kutekeleza majukumu yenu ya kazi

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane akimkabidhi cheti cha pongezi mstaafu ambaye alikuwa Afisa Uuguzi wa JKCI Marcelina Granima wakati wa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu iliyofanyika katika ukumbi wa Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam.

Na: JKCI

Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kufanya kazi kwa uweledi, ufanisi na kuepuka vitendo vyote vinavyoweza kuwasababishia kushindwa kufikia hatua ya kustaafu katika utumishi wa umma.

Rai hiyo imetolewa na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane wakati wa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu wawili waliofikia ukomo wa utumishi wa umma hivi karibuni na kuagwa leo katika ukumbi wa Taasisi hiyo Jijini Dar es Salaam.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo Dkt. Waane amesema kuwa wapo watu wengi ambao wanaanza utumishi wa umma katika ngazi mbalimbali lakini hawafikii ukomo wa utumishi wao kutokana na sababu mbalimbali, hivyo ni vyema kwa wastaafu hao kumshukuru Mungu kwa kuwafikisha salama siku ya leo.

“Mnastahili pongezi kwa utumishi uliotukuka, Tunafahamu ni kwa namna gani ambavyo mmekuwa mkifanya kazi, mmekuwa mkitoa huduma bora kwa wagonjwa wetu, kila mstaafu amekuwa na namna yake ya kufanya kazi, mmetumia utashi mwingi na kujitoa kwa ajili ya wagonjwa, hongereni sana” alisema Dkt. Waane.

Aidha Dkt. Waane amewataka wastaafu hao kutokusita kuendelea kutoa maoni yao yatakayoiboresha JKCI ili kuendelea kuboresha huduma za matibabu ya moyo nchini pamoja na kujenga undungu ambao umejengwa baina yao.

Kwa upande wake mstaafu ambaye alikuwa Afisa Uuguzi Marcelina Granima ameushukuru uongozi wa JKCI kwa kuwa Taasisi ya umma ya kipekee kabisa katika kutoa huduma bora za afya lakini pia kuwawekea mazingira salama na wezeshi watumishi wake.

Granima amesema kuwa safari ya utumishi wake wa umma haikuwa raisi, ilikua ni safari ndefu yenye mafanikio na matope mengi lakini kwasababu kazi ya uuguzi na udaktari ni kazi ambayo inahitaji wito hivyo kumfanya kuendelea kujitoa kwa ajili ya wagonjwa.

“Nawasihi watumishi wenzangu mnaoendelea na utumishi wa Umma, ni vyema mkawa na hekima katika kazi, mjue yakuwa hamkuja kazini kutembea, bali angalieni hekima ambayo Mungu amewapa katika kutekeleza majikumu yenu” alisema Granima

“JKCI mtaani inapeperuka kama bendera, naenda kuwa mwakilishi wenu mzuri, hili jina tulilolijenga liendelee kukua na kuheshimika Tanzania na duniani kote” alisema Granima

Naye mstaafu aliyekuwa Mhudumu wa Afya Sofi Josiah amewataka wafanyakazi wa JKCI kuendelea kuwa na ushirikiano unaojenga na kuifanya JKCI kuwa Taasisi bora zaidi.

“Kustaafu ni matakwa ya kisheria, kikubwa zaidi ni kustaafu na kuacha kumbukumbu katika nafasi uliyokuwa ukiitumikia, niwaombe wote tufanye kazi kwa ushirikiano na tukistaafu tukumbukwe kwa uweledi wetu kazini” alisema Sofi

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane akimkabidhi mfano wa hundi mstaafu ambaye alikuwa Mhudumu wa afya wa JKCI Sofi Josiah wakati wa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu iliyofanyika katika ukumbi wa Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam.

Wastaafu Marcelina Granima na Sofi Josiah wakikata keki wakati wa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu hao iliyofanyika katika ukumbi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) leo Jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane akimlisha keki mstaafu ambaye alikuwa Mhudumu wa afya wa JKCI Sofi Josiah wakati wa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu iliyofanyika katika ukumbi wa Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Kurugenzi ya huduma ya Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Robert Mallya akimlisha keki      mstaafu ambaye alikuwa Afisa Uuguzi wa JKCI Marcelina Granima wakati wa hafla fupi ya kuwaaga wastaafu iliyofanyika katika ukumbi wa Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Kurugenzi ya huduma ya Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Robert Mallya katika picha ya pamoja na wastaafu Afisa Uuguzi wa JKCI Marcelina Granima (wapili kushoto) na Sofi Josiah (wapili kulia mstari wa chini) pamoja na baadhi ya wafanyakazi baada ya hafla fupi ya kuwaaga wastaafu hao iliyofanyika katika ukumbi wa Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam.


 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari