Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete watakiwa kufanya kazi kwa kufuata maadili na kuepuka mazingira ya rushwa
Mkurugenzi wa utawala na Fedha
wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) CPA Agnes Kuhenga akisoma bajeti ya
Taasisi hiyo kwa mwaka wa fedha 2021/22
wakati wa kikao cha Baraza la Wafanyakazi kilichofanyika leo jijini Dar es
Salaam.
Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kutoa huduma kwa wateja wanaowahudumia kwa kufuata maadili ya kazi na kuepuka mazingira ya rushwa kwa kufanya hivyo wananchi wataridhika na huduma wanazozitoa.
Rai hiyo imetolewa leo jijini
Dar es Salaam na Mwenyekiti wa baraza la wafanyakazi wa Taasisi hiyo Prof.
Mohamed Janabi wakati akizungumza na
wajumbe waliohudhuria kikao cha baraza
la wafanyakazi wa Taasisi hiyo.
Prof. Janabi ambaye pia ni
Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI alisema
ushirikiano wa pamoja baina ya wafanyakazi pamoja na uwazi katika utendaji kazi
vinachangia kwa kiasi kikubwa kutoa huduma bora kwa wateja wanaowahudumia
wakiwemo wagonjwa.
"Unapomuhudumia mteja toa
huduma yako kwa moyo na kujituma epuka kuchukuwa hela za mgonjwa
sijasema kama mnafanya hivyo bali natoa onyo kwani yeyote atakayebainika
kufanya hivyo atachukuliwa hatua kali za kinidhamu”,.
“Hakikisheni wateja
mnaowahudumia wanaridhika na huduma mnayoitoa kwani kupata huduma ni haki yao
na wewe unawajibika kutoa huduma hiyo kwani Serikali imekuajiri kwa ajili ya
kuwahudumia wananchi”, alisema Prof. Janabi.
Mwenyekiti huyo wa baraza la
wafanyakazi alisema menejimenti ya Taasisi hiyo itaendelea kusimamia na
kuhakikisha wafanyakazi wanapata masslahi yao kwa wakati na kuhakikisha wanatoa
huduma bora kwa wateja wao wakiwemo wagonjwa.
Akitoa mada kuhusu
majukumu na wajibu wa wajumbe wa baraza la wafanyakazi Afisa Mwandamizi kutoka
Wizara ya Kazi Deus Mshelila alisema ni muhimu kwa wajumbe wa baraza la wafanyakazi
wakafahamu wajibu wao kwa kufanya hivyo kutasaidia baraza hilo kutatua matatizo
mbalimbali yanayowakabili wafanyakazi.
Alisema katika Taasisi yeyote
ile ukitoa kikao cha Bodi kikao kinachofuata ni baraza la wafanyakazi hivyo
basi kikao hicho ni cha muhimu kwani kinajadili na kushauri namna ya
utekelezaji wa masuala ya Kisera na uchumi wa Taasisi.
"Katika kikao cha baraza la
wafanyakazi hakuna kunyoosheana vidole bali ni kutatua changamoto ikiwa ni
pamoja na kushauri, kurekebisha na kukosoa kasoro zilizopo katika utendaji kazi
kwa maslahi ya wafanyakazi na Taasisi husika”,.
“Kisheria vikao vya baraza la
wafanyakazi vinafanyika mara mbili kwa mwaka lakini kama kuna jambo la dharula
vinaweza kufanyika mara tatu kwa mwaka”, alisema Mshelila.
Kwa upande wake katibu wa baraza la kwanza ambaye amemaliza
muda wake Dkt. Samweli Rweyemamu alishukuru kwa nafasi aliyopewa ya
kufanya kazi katika baraza hilo na kuwaomba wajumbe na menejimenti ya Taasisi
hiyo kutoa ushirikiano wa kutosha kwa viongozi wapya waliochaguliwa.
Katika kikao hicho cha baraza la pili la wafanyakazi tangu ianzishe Taasisi hiyo mwaka 2016 ulifanyika uchaguzi wa kuchagua Katibu na Katibu msaidizi ambapo Afisa Tawala Abdulrahman Muya alichaguliwa kuwa Katibu na Afisa Uuguzi Theresia Marombe alichaguliwa kuwa Katibu Msaidizi.
Comments
Post a Comment