Kateni bima za afya kumudu gharama za matibabu – Prof.Janabi

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akimpima shinikizo la damu (BP) mwananchi aliyetembelea banda la Taasisi hiyo kwa ajili ya kufanya vipimo vya magonjwa ya moyo na kisukari wakati wa maonesho ya 46 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa.

Mkurugenzi wa Fedha na Mipango wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Agnes Kuhenga akisaini kitabu cha wageni alipotembelea banda la Taasisi hiyo lililopo katika Maonesho ya 46 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayoendelea kwenye viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa.

Mteknolojia wa maabara wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Jordan Megabe akimchukuwa kipimo cha damu mwananchi aliyetembelea banda la Taasisi hiyo kwa ajili ya kumfanyia vipimo vya kuchunguza figo, ini na kiwango cha mafuta mwilini wakati wa Maonesho ya 46 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayoendelea katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa.

Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mzuma Mzuma akitoa ushauri wa matumizi sahihi ya dawa za moyo kwa mwananchi aliyefika katika banda la Taasisi hiyo kwa ajili ya kupata huduma ya vipimo vya magonjwa ya moyo wakati wa maonesho ya 46 ya Biashara ya  Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) yanayofanyika katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa.

Baadhi ya wananchi waliotembelea  banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakipatiwa  huduma za vipimo na ushauri wa jinsi ya kuepukana na magonjwa ya moyo wakati wa maonesho ya 46 ya Biashara ya  Kimataifa ya Dar es Salaam  (SABASABA) yanayofanyika katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa.


 Baadhi ya Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wanaotoa huduma za ushauri na matibabu ya magonjwa ya moyo kwa wananchi wanaotembelea banda la Taasisi hiyo lililopo katika maonesho ya 46 ya Biashara ya Kimataifa ya Dar es Salaam (SABASABA) wakiwa katika picha ya pamoja.

Picha na: Khamis Mussa

****************************************************************************

Wananchi wahimizwa kukata bima za afya kumudu huduma za matibabu kwani magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo hutumia gharama kubwa kuyatibu na mara nyingi hutibiwa kwa kipindi chote cha maisha pale mtu anapogundulika kuwa na magonjwa hayo.

Rai hiyo imetolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi wakati wa maonesho ya 46 ya Kimataifa ya Biashara (SABASABA) yanayoendelea katika Viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa.

“Ni muhimu kila mtanzania akakata bima ya afya kwani matibabu ya moyo ni gharama, mtu mwenye magonjwa haya hutibiwa maisha yake yote, na dawa zinazotumika pia gharama hivyo huwezi kuwa unatoa hela kila siku kwa ajili ya matibabu  kwani hata uchumi wako unaweza kuyumba kwa ajili ya matibabu” alisema Prof. Janabi.

Aidha Prof. Janabi aliwahimiza wananchi kutembelea katika banda la Taasisi hiyo kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo na kisukari ili kujenga tabia ya kuchunguza afya zao mara kwa mara

“Uchunguzi huu wa magonjwa ya moyo kwa wananchi usiishie hapa Sabasaba, tuwe na tabia ya kuchunguza afya zetu mara kwa mara katika vituo vya afya vilivyo karibu nasi ili pale tutakapogundulika kuwa na matatizo na kuhitaji huduma za kibingwa zaidi tuweze kupata rufaa mapema kufika katika hospitali yetu kwa ajili ya matibabu zaidi”, alisema Prof. Janabi

Prof. Janabi alisema kuwa watu wanaowafanyia vipimo katika banda la JKCI lililopo Sabasaba na kugundulika kuwa wanahitaji huduma za kibingwa zaidi hupatiwa fursa ya moja kwa moja kwenda kwenye Taasisi hiyo kwa ajili ya matibabu zaidi.

“Niko hapa katika banda letu kwa ajili ya kutoa huduma za upimaji wa magonjwa ya moyo, shinikizo la damu na sukari mwilini. Mwananchi niliyetoka kumhudumia sasa hivi nimekuta anatembea na presha ya 195 kwa 117 ambapo kidaktari ni hatari kwa sababu ni mtu ambaye akianguka hapo huwezi kushangaa kutokana na shinikizo lake la damu kuwa juu”,

“Tumemuanzishai dawa za Shinikizo la juu la damu kwa ajili ya kuweka presha yake sawa, lakini tumemshauri kufuatilia mwenendo wa presha yake mara kwa mara na pale atakapoona anahitaji huduma zaidi afike katika Taasisi yetu”, alisema Prof. Janabi.

Kwa upande wake mwananchi aliyepatiwa huduma katika banda la JKCI Rehema Daniel aliwapongeza wataalam wa afya wa Taasisi hiyo kwa kutoa elimu ya magonjwa ya moyo kabla ya kufanyiwa vipimo kwani kwa kufanya hivyo kumemuwezesha kufahamu sababu, viashiria na namna ya kuepukana na magonjwa ya moyo.

“Sikuwa na uelewa wa kina kuhusu magonjwa haya ya moyo, lakini elimu niliyoipata hapa leo inaniwezesha kwenda kuwa mwalimu katika familia yangu kuhusu magonjwa haya kwa kuhakikisha kuwa familia yangu inaepukana na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo”,

“Naelewa umuhimu wa kuwa na bima ya afya ndio maana hata mimi ninayo, rai yangu kwa wananchi wenzangu ni kuwa na kadi hizi za bima ya afya kwasababu maradhi hutufika wakati wowote bila kuangalia kama wakati huo tuko vizuri ama vibaya kiuchumi”, alisisitiza Rehema.

Naye Mteknolojia wa Maabara wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Jordan Megabe alisema kuwa mwitikio wa wananchi kufika katika banda la JKCI kuchunguza magonjwa ya moyo na vipimo vya damu vinavyofanywa maabara ni mkubwa kutokana na hamasa zinazotolewa katika banda hilo.

“Tupo hapa Sabasaba kwa ajili ya kuwahudumia wananchi kutoka pande zote za Tanzania wasisite kufika katika banda letu, tumejipanga kutoa huduma bora kwa kila mwananchi anayehitaji kufanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo”, alisema Jordan.

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Wafanyakazi waliohama JKCI waagwa