JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari


Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Asha Izina akikata utepe wakati wa kuzindua magari mawili yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwaajili ya kutoa huduma kwa wagonjwa wanaotibiwa JKCI. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge.


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiwa ndani ya gari la kuhudumia wagonjwa lililotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na kuzinduliwa leo na Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo Asha Izina.

Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Asha Izina akizungumza na waandishi wa Habari mara baada ya uzinduzi wa magari mawili yaliyotolewa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwaajili ya kutoa huduma kwa wagonjwa wanaotibiwa katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.

*********************************************************************************************************************************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuipatia magari mawili ambayo yatatumika kutoa huduma za afya kwa wagonjwa wanaotibiwa katika Taasisi hiyo.

Shukurani hizo zimetolewa leo jijini Dar es Salaam na Kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo Asha Izina wakati akizundua magari hayo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Asha ambaye pia ni mratibu wa huduma za afya ya uzazi na mtoto mkoa wa Rukwa alisema magari hayo yametolewa ili kusaidia katika huduma za afya ambapo katika Taasisi hiyo yatasaidia kutoa huduma kwa wagonjwa wa moyo watakaohitaji huduma ya gari la wagonjwa.

Kaimu Mwenyekiti wa Bodi hiyo ya Wadhamini alisema  Mhe. Dkt. Samia ametoa magari zaidi ya 700 katika Hospitali zote nchini kwaajili ya kutoa huduma katika hospitali ambapo JKCI imepokea magari mawili.

“JKCI tumepata magari mawili, moja likiwa gari la kuhudumia wagonjwa (Ambulance) na lingine kwaajili ya kusimamia usimamizi shirikishi unaofanywa na wataalamu wabobezi wa magonjwa ya moyo waliopo JKCI”, alisema Asha.

Asha alisema gari la kuhudumia wagonjwa litasaidia katika kazi za kuchukua wagonjwa kutoka maeneo mbalimbali ya ndani na nje ya Dar es Salaam pale litakapohitajika.

“Lengo kubwa la kupewa gari la kuhudumia wagonjwa ni kuhakikisha wagonjwa wanapata huduma kwa wakati kwani mara nyingi kumekuwa na tatizo la baadhi ya wagonjwa kuchelewa kufika hospitali kwaajili ya kupata huduma pale wanapokuwa na dharura”, alisema Asha.

Aidha Asha ametoa maelekezo ya kuitaka JKCI kuwa na namba ya dharura ambayo itawaruhusu wananchi kupiga simu wakati wowote wanapohitaji msaada wa gari linalohudumia wagonjwa.

“Sasa hivi Taasisi yetu inahudumia wagonjwa wengi waliopo ndani ya nchi na wengine kutoka nchi za jirani, hivyo kupitia gari hili tunaenda kurahisisha huduma za kupokea wagonjwa wanapofika katika uwanja wetu wa ndege wanapokelewa na kufikishwa JKCI kwa haraka”, alisema Asha.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imekuwa ikiwajali wananchi wake ndio maana ikaona umuhimu wa kutoa magari hayo ili kurahishisha huduma zinazotolewa na JKCI.

Dkt. Kisenge alisema JKCI imefarijika kupokea magari hayo kwani sasa hivi imekuwa ikipokea idadi kubwa ya wagonjwa kutoka mikoa mbalimbali na nje ya nchi wengi wao wakiwa na hali isiyoridhishwa hivyo kwa kutumia magari hayo wagonjwa watapokelewa kirahisi.

“JKCI inapokea wagonjwa kutoka nchi zaidi ya 20 wengi wao wanapofika katika uwanja wetu wa ndege wanahitaji gari la kuhudumia wagonjwa kuwapokea na kuwafikisha hapa kwetu; ndani ya miezi mitatu tumeweza kupokea wagonjwa takribani 100 kutoka nje ya nchi”, alisema Dkt. Kisenge.

 

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma