Wafanyakazi JKCI wametakiwa kuwa wabunifu na kutumia utaalamu walionao kuwahudumia wagonjwa

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akikata keki ya kuadhimisha miaka nane tangu kuanzishwa kwa Taasisi hiyo wakati wa mafunzo ya jinsi ya kufanya kazi kimkakati na kufikia malengo waliyojiwekea kwa wafanyakazi wa JKCI yaliyofanyika hivi karibuni katika msitu wa mazingira asilia Pugu Kazimzumbwi uliopo Kisarawe mkoani.

Mkufunzi kutoka Taasisi ya Uongozi Institute Dunstan Mulaku akiwafundisha wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) jinsi ya kufanya kazi kimkakati na kufikia malengo waliyojiwekea wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyika hivi karibuni  katika msitu wa mazingira asilia Pugu Kazimzumbwi uliopo Kisarawe mkoani Pwani.


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimkabidhi zawadi ya mfano wa hundi ya shilingi milioni 11.1 Afisa Uuguzi  Mstaafu Fatihiya Mustafa wakati wa mafunzo kwa wafanyakazi ya jinsi ya kufanya kazi kimkakati na kufikia malengo waliyojiwekea yaliyokwenda sambamba na hafla fupi ya kumuaga mfanyakazi huyo iliyofanyika katika msitu wa mazingira asilia Pugu Kazimzumbwi uliopo Kisarawe mkoani Pwani

Afisa Uuguzi mstaafu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Fatihiya Mustafa akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Dkt. Peter Kisenge zawadi ya picha ya saa ya ukutani kwaajili ya wafanyakazi wanaofanya kazi katika chumba cha kutoa huduma ya vipimo vya moyo vya ECHO na ECG wakati wa hafla fupi ya kumuaga iliyofanyika hivi karibuni katika msitu wa mazingira asilia Pugu Kazimzumbwi uliopo Kisarawe mkoani Pwani

Na: JKCI
*************************************************************************************************************

Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kuwa wabunifu na kutumia utaalamu walionao kwa kuwahudumia wagonjwa kwa kufanya hivyo watakuwa wameisadia Serikali ambayo imetumia fedha nyingi kuwasomesha na kununua vifaa tiba vya kisasa vya kutibu magonjwa ya moyo.

Rai hiyo imetolewa hivi karibuni na Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge wakati akifungua mafunzo ya siku moja kwa wafanyakazi wa Taasisi hiyo ya jinsi ya kufanya kazi kimkakati na kufikia malengo waliyojiwekea yaliyofanyika katika msitu wa mazingira asilia Pugu Kazimzumbwi uliopo  Kisarawe mkoani Pwani.

Dkt. Kisenge alisema ubunifu mahali pa kazi unasaidia kutatua changamoto mbalimbali zinazojitokeza na hivyo kufikia dira ya Taasisi hiyo ya kuwa Taasisi inayotambulika kimataifa katika kutoa huduma, mafunzo na utafiti wa moyo.

“Ninawaomba mfanye kazi kwa bidii huku mkifuata maadili ya kazi yenu ya kuwahudumia wagonjwa kwani kazi hii inahusisha maadili , fanyeni kazi kwa pamoja na kutumia utaalamu mlio nao  kuwasaidia watu wenye matatizo ya moyo”.

“Tumeamua kufanya mafunzo haya katika msitu huu mahali ambapo ni nje kabisa ya eneo la kazi ili wafanyakazi waweze kuelewa kirahisi vitu vinavyofundishwa ambavyo vitawasaidia katika utendaji wao wa kazi za kila siku”, alisema Dkt. Kisenge.

Kwa upande wake mkufunzi wa mafunzo hayo kutoka Taasisi ya Uongozi Dunstan Mulaku alisema  amewafundisha wafanyakazi hao namna ya kufanya kazi kimkakati na kufikia malengo waliyojiwekea kwa kufanya hivyo wataisaidia JKCI kufika mbali zaidi.

Mulaku alisema maadili ya msingi ya Taasisi hiyo ni ushirikiano, uadilifu, weledi na ubunifu kama wafanyakazi hao watayafuata wataweza kufikia malengo ya Taasisi ya kutoa huduma za  moyo zenye uthibitisho, mafunzo na utafiti.

Kwa upande wa wafanyakazi walioshiriki mafunzo hayo walishukuru  kwa nafasi waliyoipata ya kushiriki mafunzo na kusema kuwa imewasidia kujua mbinu za kufanya kazi kimkakati na kufikia malengo waliyojiwekea.

Dkt.Tulizo Shemu ambaye ni Mkurugenzi wa Hospitali ya JKCI Dar Group alisema mafunzo hayo yameenda sambamba na maadhimisho ya miaka nane ya kuanzishwa kwa Taasisi hiyo na wafanyakazi  wamefundishwa jinsi ya kufanya kazi kama timu ili wafikie malengo ya miaka mitano kama yalivyopangwa katika mpango mikakati.

Monica Mwaluka ambaye ni daktari kutoka Hospitali ya JKCI Dar Group alisema amefurahi kuungana na wafanyakazi wa JKCI  makao makuu kwa pamoja wamepata mafunzo na kufanya utalii wa ndani katika msitu huo wa mazingira asilia Pugu Kazimzumbwi kwa kuwa kwao karibu wataweza kufanya kazi kwa ushirikiano mkubwa.

“Ninaushukuru uongozi kwa kuandaa mafunzo haya ambayo yameniwezesha kujua mbinu za kufanya kazi kimkakati huku nikishirikiana na wenzangu  hakika yatanisaidia katika utendaji wangu wa kazi za kila siku”, alisema Dkt. Monica.

“Mafunzo haya yamenifanya niweze kujitambua na kujua jinsi ya kufanya kazi na watu wenye tabia mbalimbali nitayatumia katika kutoa huduma kwa wagonjwa ili wananchi wengi waweze kufaidika na Taasisi yetu iweze kusonga mbele zaidi”, alisema Dominick.

Licha ya kushiriki mafunzo hayo wafanyakazi hao walipata nafasi ya kufanya utalii wa ndani kwa  kutembelea  maeneo mbalimbali  ya msitu huo  ikiwa ni pamoja na bwawa la Minaki lenye kina cha  mita nane na urefu wa kilomita 1.2, mapango ya popo, pango la mzimu wa Mavoga, kupanda mlima wenye urefu wa kilomita 1.5 kwa kutumia kamba pamoja na kuona miti ya asili , ndege, vipepeo na panzi wenye bendera ya taifa .

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari