JKCI kushirikiana na Misri kuboresha matibabu ya moyo nchini


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na wadau kutoka Kampuni ya STERI CARE iliyopo nchini Misri walipofika JKCI jana kwaajili ya kuangalia maeneo ambayo taasisi hiyo itashirikiana na kampuni hiyo kuboresha upatikanaji wa vifaa tiba na ujuzi katika kutoa huduma za matibabu ya moyo. 
Baadhi ya wawakilishi kutoka Kampuni ya STERI CARE iliyopo nchini Misri wakifuatilia wakati wa kikao na uongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kujadili maeneo yakushirikiana kuboresha upatikanaji wa vifaa tiba na ujuzi katika kutoa huduma za matibabu ya moyo jana jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiwa katika picha ya pamoja na wadau kutoka Kampuni ya STERI CARE iliyopo nchini Misri baada ya kikao cha kuangalia maeneo ya ushirikiano jana katika ukumbi wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.

Na: JKCI
*************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kushirikiana na kampuni ya STERI CARE iliyopo nchini Misri kurahisisha upatikanaji wa vifaa tiba vya matibabu ya magonjwa ya moyo nchini.

Ushirikiano huo utagusa eneo la vifaa tiba vya moyo, mavazi yanayotumiwa na wataalamu wa afya eneo la kazi pamoja na kushirikiana katika kubadilishana ujuzi wa kutoa huduma za matibabu ya moyo.

Akizungumza wakati wa kikao na wadau kutoka kampuni ya STERI CARE Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema JKCI inatamani kuagiza vifaa tiba kutoka nje ya nchi moja kwa moja kupunguza gharama za vifaa hivyo itakayopelekea gharama za matibabu kupungua pia.

“Kama JKCI itapata makampuni makubwa nje ya nchi na kuchukua mahitaji yake huko gharama za vifaa vinavyohitajika kwaajili ya matibabu ya moyo zitapungua lakini pia kupunguza athari za ukosefu wa vifaa hivyo kwa wakati”, alisema Dkt. Kisenge

Dkt. Kisenge alisema Taasisi itafanya utafiti yakinifu na kuainisha viwanda mbalimbali vinavyotengeneza vifaa tiba ili iweze kufanya navyo kazi kwani uhitaji wa vifaa tiba umekuwa mkubwa.

Naye mwakilishi kutoka kampuni ya STERI CARE iliyopo nchini Misri Mohmad Tohan alisema kampuni hiyo ipo tayari kufanya kazi na JKCI kwani huduma nyingi zinazotolewa na kampuni hiyo zipo JKCI.

“Leo tumekuja na mavazi ya wataalamu wa afya tuliyonayo ili muweze kuona kazi zetu lakini pia tunavyo vifaa vinavyotumika katika matibabu ya magonjwa ya moyo ambavyo tunaamini mkichukua kwetu gharama zitapungua”, alisema Mohmad

 

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)