JKCI kushirikiana na Zanzibar kutibu wagonjwa wa moyo
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.
Dkt. Hessein Ali Mwinyi akizungumza na washiriki wa mkutano wa kimataifa wa
magonjwa ya moyo kutoka nchi 30 wakati wa kufunga mkutano wa kimataifa wa
magonjwa ya moyo uliofanyika kwa siku mbili katika Hotel ya Golden Tulip
iliyopo mjini Zanzibar
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dkt. Hessein Ali Mwinyi akimkabidhi ngao mwakilishi kutoka kampuni ya kusambaza dawa za binadamu ya Anudha wakati wa kufunga mkutano wa kimataifa wa magonjwa ya moyo leo katika Hoteli ya Golden Tulip iliyopo mjini Zanzibar
Daktari wa wagonjwa wa dharura na wanaohitaji uangalizi maalumu anayetoka Hospitali ya Taifa Muhimbili Said Kilindimo akiwaonyesha wataalamu wa afya namna ya kumhudumia mgonjwa wa dharura wakati wa mkutano wa kimataifa wa magonjwa ya moyo uliomalizika leo katika Hoteli ya Golden Tulipo iliyopo mjini Zanzibar
Na: JKCI
***************************************************************************************************************
Wizara ya afya Zanzibar imelekezwa kushirikiana na Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kuhakikisha huduma za upasuaji wa moyo zinaanza kutolewa
kwa kipindi cha muda mfupi Zanzibar.
Ushirikiano huo na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete umelenga
kupunguza athari na matatizo yanayoweza kuhusishwa na kuchelewa kwa matibabu
hivyo kuokoa maisha ya wananchi na wageni wanaotembelea Zanzibar wanapokutwa na
maradhi ya moyo.
Akizungumza wakati wa kufunga mkutano wa kimataifa wa
magonjwa ya moyo leo Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.
Dkt. Hussein Ali Mwinyi alisema Serikali ya Zanzibar iko tayari kukuza ushirikiano
na kutenga rasilimali zitakazohusika katika utafiti, kinga na matibabu ya
magonjwa ya moyo na mishipa ya damu kuboresha huduma za afya Zanzibar.
“Serikali ya Zanzibar iko tayari kuwekeza rasilimali za
kutosha na vifaa vinavyohitajika kushirikiana na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) na Taasisi nyingine zinazotoa huduma za matibabu ya moyo duniani kuifanya
Hospitali ya Lumumba kuwa na kitengo cha kuhudumia wagonjwa wa moyo ”,
“Ushirikiano huu utasaidia kujenga uwezo wa ndani na kuhakikisha
kuwa wagonjwa wa moyo waliopo Zanzibar wanapata huduma na matibabu ya dharura
kwa wakati ili kupambana na vifo vinavyoweza kuepukika”, alisema Mhe. Dkt. Mwinyi
Mhe. Dkt. Mwinyi alisema ili kuhakikisha wananchi wengi zaidi
wenye magonjwa ya moyo wanapata faraja, Serikali inatengeneza mkakati wa taifa
wa kupunguza matumizi ya vyakula vinavyohusishwa na magonjwa ya moyo ili
kutunza afya za wananchi.
“Nchi yetu ina dhamira ya kukuza utalii ikiwemo utalii wa
matibabu hivyo Zanzibar ina fursa ya kipekee kwani ikiwekeza miundombinu
mizuri, kuwa na vifaa vya kisasa wageni wataweza kuchanganya mapumziko yao na
kuwa na uhakika wa kupata huduma za afya zenye viwango wanapokuwa nchini”,
alisema Mhe. Dkt, Mwinyi
Akizungumza kuhusu mkutano huo Mhe. Dkt. Mwinyi alisema ni
matumaini yake kuwa mafunzo yaliyopatikana na ushirikiano ulioundwa katika
mkutano huu utachangia kwa kiasi kikubwa kuboresha huduma za afya na kuimarika
kwa afya za watu walioathirika na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya
moyo.
“Kwa hakika kufanyika kwa mkutano huu hapa Zanzibar ni
ushahidi kuwa juhudi na ushirikiano uliopo kwa wizara zetu mbili za afya katika
kuboresha huduma za afya kwa wananchi kupitia mbinu ya kubadilishana maarifa na
kukuza ufumbuzi katika tafiti mbalimbali”,
Mhe. Dkt. Mwinyi alisema uwepo wa wataalamu kutoka ndani na nje
ya nchi unaonyesha nia ya kitaifa na kimataifa ya kujitolea katika kuendeleza
huduma ya kudhibiti magonjwa ya moyo na kutoa matibabu ya magonjwa hayo hapa
nchini.
Kwa upande wake kaimu Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete Asha Izina alisema kupitia mkutano huo wataalamu wa afya
wameweza kubadilishana uzoefu utakaowasaidia kutoa huduma bora zaidi.
Asha alisema huduma za matibabu ya moyo umekuwa ukihimarishwa
kupitia programu mbalimbali kwa wataalamu wa afya lengo likiwa kuzifanya huduma
hizo kuwa na adhi sawa duniani.
“Tunaamini wataalamu wa afya walioshiriki katika mkutano wetu
walivyokuja na wanavyoondoka wako tofauti kwani wameweza kupata kitu kipya
katika fani zao za kutoa huduma kwa wagonjwa wa moyo”, alisema Asha
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema washiriki 100 kutoka Serikali ya mapinduzi ya
Zanzibar wameweza kushiriki mkutano huo uliowawezesha kupata mwanga wa namna ya
kutoa huduma kwa wagonjwa wa moyo.
Dkt. Kisenge alisema kupitia mkutano huo wataalamu wa afya
wameweza kujadili maendeleo ya magonjwa ya moyo barani Afrika na kuweka
mikakati itakayosaidia wagonjwa hao.
Jumla ya washiriki 500 kutoka ndani na nje ya nchi
wameshiriki mkutano wa pili wa kimataifa wa magonjwa ya moyo ulioandaliwa na
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) uliokuwa na kauli mbiu “Maendeleo katika
utoaji wa huduma za matibabu ya moyo Afrika”.
Comments
Post a Comment