Watu 587 wapimwa moyo Arusha

Watu 587 wamepimwa moyo wakati wa kambi maalumu ya siku sita iliyofanywa na wataalamu wa afya wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) mkoani Arusha.

Kambi hiyo maalumu iliyomalizika hivi karibuni imefanyika katika viwanja vya Kituo cha Mikutano cha Kimataifa Arusha (AICC) kuanzia tarehe 19 Februari ambapo wananchi wa Arusha na mikoa ya jirani walipata fursa ya kupima magonjwa ya moyo.

Akizungumzia kambi hiyo Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Samweli Rweyemamu alisema jumla ya wanawake 364 sawa na asilimia 60 na wanaume 223 sawa na asilimia 40 walipatiwa huduma za vipimo na matibabu ya magonjwa ya moyo.

Dkt. Rweyemamu alisema baada ya watu hao kufanyiwa vipimo na matibabu, watu 58 sawa na asilimia 10 walipewa rufaa kufika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwaajili ya matibabu zaidi na wengine kwaajili ya kufanyiwa upasuaji wa moyo.

“Asilimia 90 ya watu wote waliopatiwa matibabu katika kambi hii tumewakuta na matatizo ya shinikizo la juu la damu ambapo baadhi yao tayari wapo katika matibabu na wengine tumewagundua kwa mara ya kwanza”, alisema Dkt. Rweyemamu

Akizungumza mara baada ya kupatiwa huduma katika kambi hiyo mkazi wa Arusha Furaha Saitori aliwashukuru wataalamu wa afya kutoka JKCI kwa kuweka kambi hiyo kuwasaidia wananchi wa Arusha ambao bila kambi hiyo wasingepata nafasi ya kupima afya zao.

Furaha aliziomba hospitali za kibingwa nchini kuwapeleka wataalamu wake maeneo mbalimbali nchini kutoa huduma kwa wananchi kwani wapo wananchi wengi wana matatizo ya kiafya lakini hawawezi kuzifikia hospitali hizo.

“Kwakweli wananchi wa Arusha tumefurahi sana kupitia kambi hii tumepima moyo na kujijua, tunaomba na wataalamu wa magonjwa mengine watufikia ili tuweze kupima afya zetu kwani wapo watu wanapoteza maisha kwa kutogundua ugonjwa mapema”, alisema Furaha


 

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)