Huduma za kibingwa za matibabu ya moyo zafika Namtumbo


Mbunge wa Jimbo la Namtumbo mkoani Ruvuma Mhe. Vitta Rashid Kawawa akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam kuhusu kambi maalumu ya siku sita ya uchunguzi na matibabu ya moyo ijulikanayo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba itakayofanyika katika Wilaya ya Namtumbo kuanzia tarehe 8 hadi 13 mwezi Julai mwaka huu.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akielezea namna huduma ya tiba mkoba ijulikanayo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan itakavyofanyika katika Wilaya ya Namtumbo kuanzia tarehe 8 hadi 13 mwezi Julai mwaka huu wakati wa mkutano na waandishi wa habari uliofanyika leo jijini Dar es Salaam.

Mganga Mkuu wa Wilaya ya Namtumbo na Mkuu wa Divisheni ya Afya, ustawi wa jamii na huduma za lishe Dkt. Aaron Hyera akielezea hali ya afya ilivyo kwa wananchi wa Namtumbo wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu kambi maalumu ya siku sita ya uchuguzi na matibabu ya moyo ijulikanayo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba itakayofanyika katika Wilaya hiyo kuanzia tarehe 8 hadi 13 mwezi Julai mwaka huu.

Baadhi ya wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakisikiliza wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu kambi maalumu ya siku sita ya uchuguzi na matibabu ya moyo ijulikanayo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba itakayofanyika katika Wilaya ya Namtumbo mkoani Ruvuma kuanzia tarehe 8 hadi 13 mwezi Julai mwaka huu.

Na: JKCI

*************************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na ofisi ya Mbunge wa jimbo la Namtumbo Mhe. Vitta Rashidi Kawawa kufanya kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya moyo ijulikanayo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba.

Kambi hiyo maalumu ya siku sita itakayoanza tarehe 8 hadi 13 Julai mwaka huu inatarajiwa kufanyika kwa siku mbili katika Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya, siku mbili katika Kituo cha afya cha Lusewa na siku mbili katika Kituo cha afya cha Mputa.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Mbunge wa Jimbo la Namtumbo Mhe. Vitta Rashidi Kawawa alisema ofisi yake imeamua kuwafikishia wananchi huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya moyo pamoja na elimu ya lishe bora ili waweze kuepukana na magonjwa hayo ambayo yamekuwa tishio katika jamii.

“Tunamshukuru sana Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuanzisha program ya tiba mkoba inayotolewa na wataalamu wa JKCI kuwafikia wananchi wasioweza kufuata huduma hizi mahali zilipo na kuweza kuwapa ujuzi wataalamu waliopo katika Hospitali za Wilaya na Mikoa”, alisema Mhe. Vitta.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema Mbunge wa jimbo la Namtumbo anafunga wigo wa kuanza kuwafuata wananchi waliopo katika wilaya mbalimbali hapa nchini.

“Mbunge huyu anawajali wananchi wake ndio maana ameweza kuandaa kambi hii maalumu kuwafikisha wananchi huduma za kibingwa za matibabu ya magonjwa ya moyo katika kata za Wilaya ya Namtumbo”, alisema Dkt. Kisenge

Dkt. Kisenge alisema katika kambi hiyo wataangalia magonjwa ya moyo ya watoto, magonjwa ya shinikizo la damu, magonjwa ya valvu za moyo, matatizo ya mishipa ya damu na magonjwa mengine ya moyo.

“Tunawaomba wananchi wa Wilaya ya Namtumbo kujitokeza kwa wingi kupima afya zenu hata kama hamna dalili ni vizuri mkatumia fursa hii kupima na kupata ushauri kutoka kwa wataalamu wetu”, alisema Dkt. Kisenge

Dkt. Kisenge alisema Magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo ndio yanayochangia vifo vingi duniani hivyo kama wananchi wataweza kufuata mfumo bora wa maisha wataweza kuepukana na magonjwa hayo kwani kinga ni bora zaidi ya tiba.

“Kupitia kambi hii ya matibabu bila gharama kwa wananchi wa Namtumbo JKCI itaendelea kuwapa ujuzi wataalamu wa Namtumbo na hapo baadaye tutatengeneza kituo endelevu cha matibabu ya moyo katika Wilaya ya Namtumbo”, alisema Dkt. Kisenge

Naye Mnganga mkuu wa Wilaya ya Namtumbo Dkt. Aaron Hyera alisema huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya moyo zitakazofanyika kwa wananchi wa Wilaya ya Namtumbo zimegharamiwa na Mbunge wa jimbo la Namtumbo.

“Ama hakika Mhe. Vitta Kawawa anawajali watu wake hasa katika eneo la afya kwasababu bila afya hakuna maendeleo ukizingatia wananchi wa Namtumbo wanafanya shughuli za kuzalisha mazao ya kilimo hivyo inahitaji nguvu na afya njema kwa mafanikio ya Wilaya”, alisema Dkt. Aaron

Dkt. Aaron ambaye pia ni Mkuu wa Divisheni ya Afya, ustawi wa jamii na huduma za lishe alisema kupitia kambi hiyo wataalamu wa Namtumbo wanaenda kupata nafasi ya kujifunza ili hapo baadaye waweze kuendelea kuwatibu wale watakahitaji huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo.

“Huduma hizi zinaenda kuwapunguzia wananchi wa Namtumbo gharama, adha na usumbufu ambao wangeweza kuupata kusafiri kutoka Namtumbo hadi Dar es Saalam kwaajili ya kupata huduma za kibingwa za matibabu ya moyo”, alisema Dkt. Aaron

Dkt. Aaron aliwashukuru Mbunge wa jimbo la Namtumbo Mhe. Vitta Kawawa na Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI kwa ushirikiano walioufanya kusogeza huduma za kibingwa kwa wananchi wa Namtumbo kwani watu wengi wenye magonjwa ya moyo katika Wilaya hiyo ni kuanzia umri wa miaka 40 na kuendelea ambao wengi wao wangeshindwa kusafiri umbali mrefu kufuata huduma mahali zilipo.

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari