JKCI yapata tuzo katika kongamano la kisayansi nchini Kenya
Tafiti mbili kati ya tano za magonjwa ya moyo kutoka Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) zimechaguliwa kuwa tafiti bora na kupewa tuzo katika
kongamano la kisayansi la 41 la mabingwa wa moyo nchini Kenya.
Tafiti hizo mbili zilizopewa tuzo zilihusiana na utafiti wa
ugonjwa wa moyo kutanuka kutokana na uzazi (Peripartum Cardiomyopathy) utafiti
ambao umechukua miaka nane kufuatilia tatizo hilo.
Akizungumza na mwandishi wa habari hii Daktari wa Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Pedro Pallangyo alisema aliwasilisha tafiti hizo
katika kongamano la kisayansi la 41 lililoandaliwa na chama cha madaktari
bingwa wa moyo wa Kenya (Kenya Cardiac Society) na kufanyika mwishoni mwa wiki
iliyopita.
“Tafiti mbili kutoka JKCI zilichaguliwa kuingia kwenye
ushindani wa tafiti bora na kupewa tuzo, tafiti hizi zilihusiana na utafiti wa
ugonjwa wa moyo kutanuka kutokana na uzazi (Peripartum Cardiomyopathy)”, alisema
Dkt. Pedro
Dkt. Pedro ambaye pia ni Mkuu wa Kitengo cha Utafiti na
Mafunzo alisema Kongamano hilo lilikuwa na jumla ya tafiti 40 zilizowasilishwa
ambapo tafiti 8 zilichaguliwa kuwa tafiti bora na kustahili kupewa tuzo.
“Mbali na tafiti mbili za JKCI kupewa tuzo mimi kama
mwandishi wa tafiti hizo nimekaribishwa
katika mkutano kama huu wa mwakani na gharama zote zitalipiwa na waandaaji wa
mkutano huo”, alisema Dkt. Pedro.
Comments
Post a Comment