Mtambo wa kuzalisha hewa ya oksijeni wenye thamani zaidi ya shilingi milioni 500 wazinduliwa Hospitali ya JKCI Dar Group
Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Mbunge wa Jimbo la Ilala Mhe. Mussa Azzan Zungu akikagua eneo lililowekwa
mtambo wa kuzalisha hewa ya oksijeni wakati akizundua mtambo huo leo katika
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group. Mtambo huo hadi
kusimikwa umegharimu shilingi milioni 526,604,116
Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na
Mbunge wa Jimbo la Ilala Mhe. Mussa Azzan Zungu akizungumza na wafanyakazi wa
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) baada ya kuzundua mtambo wa kuzalisha hewa
ya oksijeni leo katika Hospitali ya JKCI Dar Group iliyopo jijini Dar es
Salaam. Mtambo huo hadi kusimikwa umegharimu shilingi milioni 526,604,116
Picha na: Hamis Mussa
*********************************************************************************************************************
Mtambo wa kuzalisha hewa ya oksijeni uliogharimu milioni
526,604,116 umezinduliwa leo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Hospitali ya Dar Group.
Mtambo huo uliozinduliwa na Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri
ya Muungano wa Tanzania na Mbunge wa Jimbo la Ilala Mhe. Mussa Azzan Zungu
umenunuliwa nchini Uturiki kwa shilingi milioni 320 na kugharimu milioni 70
kwaajilii ya kasha lakuhifadhia mtambo huo na usafirishaji, na milioni
136,604,116 zilitumika kwaajili ya kusimika mtambo huo tayari kwa kusambaza
hewa ya oksijeni katika wodi za JKCI Dar Group na sehemu zingine.
Akizungumza na waandishi wa habari wakati akizindua mtambo
huo Mhe. Zungu alisema mtambo huo umefadhiliwa na Umoja wa Mabenki Tanzania
(TBA) ikiwa ni sehemu ya kurejesha baadhi ya mapato yao kwa wananchi wenye
uhitaji wa oksijeni.
Mhe. Zungu alisema kutokana na mtambo huo kuwa sehemu ya TBA
kurudisha katika jamii, hivyo hivo JKCI iwe sehemu ya kutumia mtambo huo na
kuwawezesha wananchi kupata huduma nafuu, safi, salama na kupunguza makali ya
gharama za huduma za matibabu.
“Nawaomba Taasisi ya Moyo baada ya kuanza kutumia oksijeni
mtakayozalisha katika mtambo huu gharama ziwe nafuu ili kuwawezesha wagonjwa
wanaohitaji oksijeni kuipata kirahisi”, alisema Mhe. Zungu
Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mtendani wa Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Delilah Kimambo alisema mtambo huo unatumia umeme wa
KVA 60 na kuzalisha hewa ya oksijeni yenye ujazo wa milimita skweya 21 kwa saa
yenye kasi ya mita skweya 5 kwa saa wakati wakujaza kwenye mitungi.
“Mtambo huu una vifaa vingi ikiwemo kifaa cha kupima ubora wa oksijeni inayozalishwa, kifaa cha kusafirisha oksijeni, kifaa cha kujaza hewa, kifaa cha kukausha hewa hadi kufikia skweya mita 312 kwa saa”, alisema Dkt. Delilah
Dkt. Delilah alisema mtambo huo una tanki la kupokea hewa
lenye ujazo wa lita 1000 na tanki la kupokea hewa ya oksijeni wakati wa kutoa
lenye ujazo wa lita 1000 hivyo ni jukumu la wafanyakazi wa JKCI kuulinda ili
uweze kutoa huduma stahiki kwa wagonjwa wanaohitaji huduma za oksijeni.
Dkt. Delilah alisema mtambo huo utapunguza gharama za
uendeshaji kwa asilimia zaidi ya 3.7 kwa mwaka hivyo kuleta urahisi wa utoaji
wa huduma ya haraka kwa wagonjwa na uzalishaji utakavyoongezeka huduma ya
kusambaza oksijeni itatolewa katika hospitali zinazowazunguka.
“Kutokana na umuhimu
wa hewa ya oksijeni katika hospitali na vituo vya afya kwa wagonjwa wanaohitaji
kuongezewa hewa ya oksijeni JKCI Dar Group ilikuwa ikinunua oksijeni kwa kujaza
mitungi kutoka kwa watoa huduma mbalimbali kwa gharama kubwa”, alisema Dkt.
Delilah
Naye Mwenyekiti wa Umoja wa Mabenki Tanzania (TBA) Herman
Kasekende aliipongeza Serikali ya Tanzania kwa jitihada inayofanya kuboresha
huduma za afya nchini.
Herman alisema kila mwananchi anatamani kuwa na afya bora, umoja
wa mabenki Tanzania unaendelea kuwezesha katika jitihada na mipango inayofanywa
na Serikali pamoja na wadau wengine kuhakikisha wanajenga Tanzania yenye afya
bora.
“TBA tumeweza kusimika mtambo wa kuzalisha oksijeni katika
Taasisi hii ikiwa ni sehemu ya umoja wa mabenki Tanzania kuirudishia jamii kile
tunachopata ili jamii nayo iweze kufaidia kupitia umoja huu”, alisema Herman
Herman alisema watu wanaweza wasione umuhimu wa kuwekeza
mtambo huo kwasababu hawana uhitaji wa oksijeni kwa sasa lakini siku wakiwa na
uhitaji ndio wataelewa thamani ya uwekezaji uliofanywa na umoja wa mabenki
Tanzania.
Comments
Post a Comment