Wagonjwa 15 kuzibuliwa mishipa ya damu ya moyo iliyoziba kwa asilimia 99

Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao wa Shirika la Madaktari Afrika la nchini Marekani wakimfanyia mgonjwa upasuaji mgumu wa kuzibua mishipa ya damu iliyokuwa imeziba kwa asilimia 99 na kushindwa kupitisha damu vizuri kwa kutumia tundu dogo wakati wa kambi maalumu ya siku saba inayofanywa na wataalamu hao katika taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.


 Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao wa Shirika la Madaktari Afrika la nchini Marekani wakimfanyia upasuaji wa kuzibua valvu ya moyo iliyofunga mgonjwa mwenye matatizo ya moyo wakati wa kambi maalumu ya siku saba inayofanywa na wataalamu hao katika taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.

Na: JKCI

**************************************************************************************************************

Wagonjwa 15 ambao mishipa yao ya damu ya moyo ilikuwa imeziba kwa asilimia 99 na kushindwa kupitisha damu vizuri kufanyiwa upasuaj wa moyo kupitia tundu dogo kwa kutumia mtambo wa Cathlab.

Aidha wagonjwa wengine 10 ambao valvu zao za moyo zilikuwa zimeziba nao watafanyiwa upasuaji wa kufungua valvu hizo kupitia tundu dogo lililopo kwenye paja.

Upasuaji hizo zinafanyika katika kambi maalumu ya siku saba inayofanywa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao kutoka Shirika la Madaktari Afrika lililopo nchini Marekani.

Akizungumza na mwandishi wa habari hii daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Kawajika Mwinyipembe alisema wapo baadhi ya wagonjwa wanaofanyiwa upasuaji katika kambi hiyo matibabu yao hayakufanyika hapo awali kutokana na ukosefu wa baadhi ya vifaa.

“Kwakushirikiana na wataalamu kutoka Shirika la Madaktari Afrika tumeweza kupata vifaa vya kisasa vya matibabu vinavyotumika kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba kwa asilimia 99 kuwasaidia wagonjwa wetu lakini pia kuweza kubadilishana uzoefu”, alisema Dkt. Mwinyipembe

Dkt. Mwinyipembe alisema wagonjwa ambao valvu zao za moyo zimeziba mara nyingi ufanyiwa upasuaji wa kufungua kifua lakini kutokana na teknolojia kukua wagonjwa hao siku hizi ufanyiwa upasuaji kupitia tundu dogo.

“Tunatarajia kuzibua vavlu zilizoziba kwa asilimia 99 kwa wagonjwa 10 bila ya kuwafanya upasuaji wa kufunga kifua, matibabu ambayo yatamsaidia mgonjwa kupona kwa haraka na kutumia muda mfupi hospitali tofauti na mgonjwa aliyefanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo”, alisema Dkt. Mwinyipembe

Kwa upande wake Daktari bingwa wa upasuaji mdogo wa moyo kutoka Shirika la Madaktari Afrika Joanna Ghobrial alisema wataalamu kutoka Shirika la Madaktari Afrika wamekuwa wakishirikiana na wataalamu wa JKCI lengo likiwa kubadilishana uzoefu na kuwasaidia wagonjwa wanaohitaji matibabu ya moyo.

Dkt. Joanna alisema wataalamu wa JKCI wameendelea katika kutoa huduma za upasuaji wa moyo wa aina mbalimbali utaalamu ambao huko mbeleni hawatahitaji wataalamu wa mashirika makubwa kuwasimamia katika kutoa huduma za upasuaji wa moyo.

“Madaktari Afrika tumekuwa tukishirikiana na Taasisi hii kwa muda mrefu na matokeo ya ushirikiano wetu tunayaona, hapo baadaye wataalamu wa JKCI hawatatuitaji tena kwani wameshabobea”, alisema Dkt. Joanna.


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari