JKCI – Hospitali ya Dar Group yaboresha huduma za matibabu ya moyo


Mtechnolojia Mionzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Hamisi Athuman akiwaonesha waandishi wa habari  moja kati ya mashine mbili za kisasa za kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiogram – ECHO) zilizofungwa katika Hospitali hiyo. Serikali kupitia JKCI imenunua mashine tatu za kisasa za kupima moyo zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni mia sita ambazo mbili zimefungwa Hospitali ya JKCI Dar Group na moja itatumika katika huduma za tiba mkoba zinazojulikana kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services.

Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Dkt.Tulizo Shemu akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa mashine mbili za kisasa za kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiogram – ECHO) zilizofungwa katika Hospitali hiyo. 


Moja kati ya mashine mbili za kisasa za kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiogram – ECHO) zilizofungwa katika Hospitali ya JKCI- Dar Group. 

**********************************************************************************************************************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group imefunga mashine mbili za kisasa za kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiogram – ECHO) kwaajili ya kuboresha huduma za matibabu ya moyo kwa wagonjwa wanaotibiwa katika Hospitali hiyo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group  Dkt.Tulizo Shemu alisema mashine hizo za kisasa zinauwezo wa kubaini matatizo ya moyo ya  ndani ambayo mtu anayo tofauti na ilivyo kwa mashine zingine.

Dkt. Shemu ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo alisema kuwepo kwa mashine hizo katika Hospitali ya JKCI Dar Group kutasaidia  watu wengi wa wilaya ya Temeke na maeneo ya jirani  kupata huduma ya matibabu ya moyo kwa wingi  pasipo kutumia muda mrefu.

“Serikali kupitia Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ilinunua mashine tatu za kisasa za kupima moyo zenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni mia sita ambazo mbili zimefungwa hapa Hospitali ya JKCI Dar Group na moja itatumika katika huduma za tiba mkoba zinazojulikana kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services ambapo wataalamu wa moyo wanawafuata wananchi mahali walipo na kufanya  matibabu”, alisema Dkt. Shemu.

Dkt. Shemu alisema tangu Novemba 14 mwaka jana Serikali ilipokabidhi hospitali ya Dar Group kwa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) idadi ya wagonjwa wanaotibiwa magonjwa ya moyo imekuwa ikiongezeka, kwasasa wanaona wagonjwa 30 hadi 40 kwa siku, pia kliniki za moyo ziko kila siku na huduma inatolewa saa 24 ukilinganisha na hapo nyuma ambapo kliniki za moyo zilikuwa zinatolewa   mara mbili  kwa wiki siku za Jumanne na Alhamisi.

Alisema katika Hospitali hiyo pia wanatoa huduma za matibabu kwa magonjwa mengine tofauti na moyo ambapo huduma zimezidi kuimarika kwa kuongeza idadi ya madaktari bingwa, kununua vifaa vya kisasa, kuimarisha huduma ya dharura, kutoa mafunzo ya mara kwa mara kwa wataalamu wa afya na kuhakikisha dawa zote muhimu zinapatikana.

Kwa upande wake Mtechnolojia mionzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Hamisi Athuman alisema mashine hizo zinauwezo wa kuwapima watoto na watu wazima kwa wakati mmoja,  zinauwezo wa kubaini mtoto aliyepo tumboni kwa mama yake kama ana matatizo ya moyo au la.

“Mashine hizi zinauwezo mkubwa wa kufanya kazi zinaweza kupima watu hamsini hadi sitini kwa siku na mbali na kupima moyo zinapima mishipa ya damu kuona kama inapitisha damu vizuri au la,  zinapima mfumo wa tumbo, mkojo na uzazi”, alisema Hamisi.

Kwa upande wake Nassoro Tangulu ambaye ni mgonjwa anayetibiwa katika Hospitali ya JKCI–Dar Group alishukuru uwepo wa hospitali hiyo ambayo imewasaidia kupata huduma mbalimbali za matibabu yakiwemo ya moyo.

“Mimi na familia yangu tunatibiwa katika Hospitali hii nilikuwa nakuja hapa kwaajili ya matibabu ya shingo na mgongo lakini sasa hivi ninatibiwa moyo, ninaamini uwepo wa mashine hizi utasaidia wananchi wenye matatizo ya moyo na mengine  kupata huduma nzuri na kwa wakati bila kutumia  muda mrefu”.

“Nimeanza kutibiwa katika hospitali hii sasa ni miezi sita hali yangu haikuwa nzuri kwani sikuweza kwenda kazini kwa muda wa miezi mitatu lakini kwa sasa afya yangu imeimarika na ninakwenda kazini”, alisema Tangulu.

Tangulu alitoa wito kwa wananchi wenye magonjwa mbalimbali kwenda kutibiwa katika Hospitali hiyo kwani kuna wataalamu wa kutosha pia huduma zinazotolewa ni nzuri na  zinapatikana kwa urahisi.


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)