JKCI yapongezwa kwa kusogeza huduma za matibabu ya kibingwa kwa wananchi

 

Mkuu wa Kitengo cha Mafunzo na Utafiti wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Pedro Pallangyo akimsikiliza mtoto anayetaka kuwa daktari bingwa wa moyo wakati wa kambi maalum ya matibabu ya siku tano inayofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Abdulla Mzee iliyopo wilaya ya Mkoani kisiwani Pemba.

Mtaalamu wa vipimo vya moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Jasmin Keria akimpima mtoto kipimo cha kuangalia jinsi umeme wa moyo unavyofanya kazi (Electrocardiography – ECG ) wakati wa kambi maalum ya matibabu ya moyo ya siku tano inayofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Abdulla Mzee iliyopo wilaya ya Mkoani kisiwani Pemba.


Mkuu wa Kitengo cha Mafunzo na Utafiti wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Pedro Pallangyo akizungumza na mkazi wa Chakechake  Kisiwani Pemba kuhusu madhara ya magonjwa ya moyo wakati wa kambi maalum ya matibabu ya moyo inayofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Abdulla Mzee iliyopo wilaya ya Mkoani kisiwani humo.

******************************************************************************************************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imepongezwa kwa kusogeza huduma za kibingwa za matibabu ya moyo kwa wananchi kwa kuwafuata mahali walipo jambo ambalo limesababisha wagonjwa wa moyo kupata matibabu kwa wakati.

Pongezi hizo zimetolewa leo na Mkuu wa Idara ya Tiba Pemba Massoud Suleiman Abdulla wakati alipotembelea kambi kambi maalum ya siku tano ya upimaji na matibabu ya moyo inayofanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Abdulla Mzee iliyopo wilaya ya Mkoani kisiwani Pemba.

Massoud alisema kambi hiyo imesaidia kwa kiasi kikubwa wananchi kufanyiwa vipimo na kupata ushauri na wale wanaokutwa na shida wanatibiwa na wenye shida kubwa zaidi wanapata rufaa ya kwenda kutibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete iliyopo Dar es Salaam.

“Changamoto kubwa tuliyonayo ni rufaa za JKCI kutoka hapa Hospitali ya Rufaa ya Abdulla Mzee ni lazima zipitie Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja iliyopo Unguja lakini uongozi unafanya jitihada ya kuwaombea wagonjwa waliokutwa na matatizo ya moyo kwenda moja kwa moja kutibiwa JKCI kwa kufanya hivi kutapunguza mzunguko mrefu wa kupata huduma”, alisema Massoud.

Massoud alisema kuna baadhi ya kambi zilizofanyika changamoto iliyotokea ni kwa wagonjwa kuchelewa kupata matibabu ya kibingwa lakini anaamini wagonjwa waliokutwa na matatizo ya moyo watapata matibabu kwawakati jambo la muhimu ni kwa viongozi kuhakikisha wagonjwa wote waliopewa rufaa wanakwenda JKCI kutibiwa.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tulizo Shemu ambaye pia ni daktari bingwa mbobezi wa magonjwa ya moyo alisema Taasisi hiyo imejipanga kuwafikia wagonjwa wengi wa moyo kwa kuwafuata mahali walipo ili wapate matibabu kwa wakati.

“Tumekuwa tukikutana na  changamoto ya wagonjwa wetu tunaowatibu kufika JKCI wakiwa wamechelewa hivyo basi kupitia huduma ya tiba mkoba ijulikanayo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services tunawafuata wananchi mahali walipo na kutoa huduma za matibabu na vipimo vya moyo”.

“Tunafanya upimaji kwa kushirikiana na wataalmu wenzetu wa Hospitali za Rufaa, Kanda na mikoa wakati wa upimaji tunawajengea uwezo wataalamu wa afya ili waweze kuwatambua wagonjwa wa moyo mapema pamoja na kufanya vipimo vya moyo kwa kufanya hivyo kumesaidia kwa kiasi kikubwa wagonjwa kupata matibabu kwa wakati”, alisema Dkt. Shemu.

Dkt. Shemu alisema upimaji huo unaenda sambamba na utoaji wa elimu kwa wananchi ili waweze kuepukana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo kwa kufuata mtindo bora wa maisha wa kufanya mazoezi, kula chakula bora, kutokutumia bidhaa aina ya tumbaku, kuepuka uzito uliopitiliza na kunywa pombe kwa kiasi.


 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)