Serikali yamuokoa Mama wa Kivule kwa matibabu ya moyo ya shilingi milioni 29 JKCI

Afisa Muuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Zaina Mlingo akimpima shinikizo la damu Mama Anna Mwansasu mkazi wa Kisamvule jijini Dar es Salaam ambaye amefanyiwa upasuaji mdogo wa kupandikiziwa  kifaa cha CRT (Cardiac Resynchronization Therapy) ambacho kinausaidia moyo kupiga mapigo yake kwa mpangilio sahihi. Gharama ya matibabu hayo ni zaidi ya shilingi  milioni 29 ambapo serikali ya awamu ya sita ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan imelipia.

*****************************************************************************************************************************************************************************************************

Mkazi wa Kivule jijini Dar es Salaam Mama Anna Mwansasu, ameishukuru Serikali ya awamu ya Sita chini ya uongozi wa Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kumsaidia kugharamia matibabu ya kubadilishiwa kifaa cha CRT (Cardiac Resynchronization Therapy) ambacho kinausaidia moyo kupiga mapigo yake kwa mpangilio sahihi.

Mama Anna alifanyiwa upasuaji mdogo wa moyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na kupandikizwa kifaa hicho ambapo gharama ya matibabu ni zaidi ya shilingi milioni 29 na kwa sasa anaendelea vizuri kiafya baada ya kupata matibabu hayo.

Akizungumza na waandishi wa habari jana akiwa wodini, Mama Anna alisema hali yake inaendelea kuimarika baada ya kufanyiwa upasuaji wa kubadilishiwa kifaa hicho muhimu.

“Naishukuru sana JKCI kwa huduma nzuri niliyoipata. Baada ya kufanyiwa upasuaji sina tatizo lolote na nasubiri kumaliza dawa nilizoandikiwa ili niruhusiwe kurudi nyumbani”, alisema Mama Anna.

Alieleza kuwa alifika hospitalini hapo tarehe 6 Machi, akalazwa tarehe 7 na kufanyiwa upasuaji tarehe 8. Awali madaktari walitarajia kubadilisha CRT peke yake lakini baada ya uchunguzi wa kina ilibainika kuwa ilibidi kubadilisha CRT pamoja na vifaa vyake vyote.

Mama Anna aliongeza kuwa hakuwa na uwezo wa kugharamia matibabu hayo ya gharama kubwa lakini baada ya taarifa yake kurushwa kupitia Azam Media, Serikali iliamua kugharamia matibabu yote.

“Nilikuwa sina uwezo wa kupata fedha za kubadilishiwa kifaa hiki lakini baada ya taarifa kusikika kwenye vyombo vya habari, Serikali ya Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ilinisaidia kugharamia matibabu yote”,  alisema Mama Anna.

Aidha Mama Anna alimshukuru Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Dkt. Peter Kisenge pamoja na timu nzima ya wataalamu wa taasisi hiyo kwa huduma bora aliyopata.

“Kifaa hiki kimenisaidia sana. Ninaamini nitaweza kufanya shughuli ndogo ndogo za maisha yangu. Kwa kweli JKCI imenipa maisha mapya”, aliongeza.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema walimpokea mgonjwa huyo baada ya kujitokeza kuomba msaada wa matibabu kutokana na tatizo la moyo kushindwa kufanya kazi vizuri ambapo awali alishafanyiwa upasuaji wa kuwekewa kifaa hicho miaka iliyopita.

Dkt. Kisenge alifafanua kuwa matatizo ya umeme wa moyo na moyo kushindwa kufanya kazi vizuri husababishwa na umri mkubwa, presha ya juu, kisukari, kuziba ghafla kwa mishipa ya damu, pamoja na baadhi ya watu kuzaliwa na tatizo hilo.

Aliwashauri wananchi kuchukua hatua za kujikinga na magonjwa ya moyo kwa kufanya mazoezi angalau mara mbili hadi tatu kwa wiki, kuepuka uvutaji wa sigara na matumizi ya pombe kupita kiasi pamoja na kuzingatia ulaji wa lishe bora.

Dkt. Kisenge pia aliwahimiza wagonjwa wote waliofanyiwa matibabu ya kuwekewa vifaa vya kuusaidia moyo kufanya kazi vizuri (CRT, Pacemaker) kufika hospitalini hapo mara kwa mara kwa ajili ya  uchunguzi ili kufuatilia maendeleo ya vifaa hivyo.

“Tunawashauri wagonjwa hawa wafike hospitalini kwa uchunguzi angalau kila baada ya miezi sita ili kufuatilia maendeleo ya kifaa na kuhakikisha kinafanya kazi vizuri”, alisema Dkt. Kisenge.

Aidha Dkt. Kisenge aliishukuru Serikali kwa kuanzisha mpango wa Bima ya Afya kwa Wote huku akisema utasaidia wananchi wengi hasa wenye kipato cha chini kupata matibabu ya magonjwa mbalimbali ikiwemo ya moyo ambayo mara nyingi huwa na gharama kubwa.

Naye Daktari bingwa wa Moyo na mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba wa JKCI, Yona Gandye aliyemuhudumia mgonjwa huyo alisema Mama Anna aligundulika kuwa na tatizo la moyo kushindwa kufanya kazi vizuri (heart failure) takribani miaka saba iliyopita.

Alisema tatizo hilo lilitokana na moyo kutanuka, hali iliyosababisha dalili za uchovu wa mara kwa mara, kupumua kwa shida pamoja na kikohozi.

Baada ya kufanyiwa uchunguzi zaidi, ilibainika kuwa kifaa cha awali cha CRT (Cardiac Resynchronization Therapy) alichokuwa amewekewa kilikuwa kimepoteza nguvu hivyo kulihitajika kubadilishwa ili kuepusha kurejea kwa tatizo hilo.

Dkt. Gandye alisema kwa sasa mgonjwa huyo anaendelea vizuri baada ya kufanyiwa upasuaji wa kubadilishiwa kifaa kipya cha CRT na anaendelea kupata uangalizi wa madaktari wa JKCI hadi hali yake itakapotengamaa na kuruhusiwa kurejea nyumbani.

Kifaa hiki cha CRT (Cardiac Resynchronization Therapy) kinatumia pacemaker maalum yenye nyaya nyingi (leads) zinazowekwa kwenye sehemu tofauti za moyo ili kurekebisha rhythm yake, kufanya moyo usukume damu vizuri, kupunguza dalili za uchovu, kizunguzungu na kupumua kwa shida na kumwezesha mgonjwa kufanya shughuli za kila siku kwa urahisi na kupata maisha bora zaidi.

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na Burkina Faso zasaini makubaliano ya ushirikiano katika kutoa tiba ya magonjwa ya moyo

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi