Rushwa na Ukiukwaji wa maadili vyapigwa vita JKCI
Afisa Maadili Mwandamizi kutoka Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Grace Matunda akitoa elimu ya maadili kwa viongozi na wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) hii leo katika ukumbi wa mikutano wa JKCI jijini Dar es Salaam. Elimu hiyo imelenga kuwajenga viongozi na wafanyakazi wa taasisi hiyo kuendelea kuwa na maadili mazuri katika maeneo yao ya kazi.
Afisa Maadili Mwandamizi kutoka Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum ya Dar es Salaam Hamadi Bakari akitoa elimu ya maadili ya Utumishi wa Umma kwa viongozi na wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa mafunzo hayo yaliyofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.

.jpeg)
Baadhi ya Viongozi na Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakifuatilia mafunzo ya maadili kwa viongozi wa utumishi wa yaliyokuwa yanatolewa na Afisa Maadili Mwandamizi kutoka Ofisi ya Rais, Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma Kanda Maalum ya Dar es Salaam Hamadi Bakari leo katika ukumbi wa mikutano wa taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
************************************************************************************************************************************************************************************************************************
Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kuzingatia maadili ya kazi kwa kufuata kanuni, taratibu na miongozo ya utumishi wa umma, ikiwemo matumizi ya lugha yenye staha, kuepuka rushwa na unyanyasaji pamoja na kuvaa mavazi yanayozingatia mwongozo wa kiutumishi.
Wito huo umetolewa leo jijini
Dar es Salaam na Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Naizihijwa Majani wakati wa mafunzo
ya siku moja ya uadilifu kwa viongozi wa umma yaliyoandaliwa na Ofisi ya Rais Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa
Umma.
Dkt. Naizihijwa ambaye pia
ni daktarin bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto alisema lengo la mafunzo hayo
ni kuwakumbusha watumishi umuhimu wa kuzingatia maadili mema ya kazi, kuwa
mfano wa kuigwa na kutoa huduma kwa weledi bila upendeleo.
Alieleza
kuwa mafunzo hayo yamewajengea uwezo wafanyakazi wa ngazi mbalimbali wa kusimama
imara katika nafasi zao kwa kufuata miiko ya kiutumishi na kuwa na mwenendo
mwema wa utumishi wa umma.
“Ninaamini mafunzo haya
yataleta mabadiliko chanya katika utendaji wetu wa kazi za kila siku, kwani
yameimarisha uelewa wa watumishi kuhusu wajibu wao na namna bora ya kuwahudumia
wananchi wakiwemo wagonjwa”, alisema Dkt. Naizihijwa.
Kwa
upande wake Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa JKCI, Ghati Chacha alisema
ni takwa la Serikali kwa watumishi wote kuzingatia maadili ya kiutumishi ili
kuhakikisha huduma zinazotolewa zinakuwa bora na zenye kuzingatia maslahi ya
wananchi.
Alisisitiza kuwa viongozi wanapaswa kuwa mfano wa
kuigwa kwa kuzingatia misingi ya utu, haki, uwajibikaji na uadilifu katika
utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku kwani maadili hayo ndiyo msingi wa
kujenga taasisi imara na yenye kuheshimika mbele ya jamii.
“Katika mafunzo haya tumekumbushwa kuwa
viongozi tunatakiwa kuzingatia utu na haki, uadilifu na wawajibikaji ili
kuendelea kutoa huduma bora kwa wateja wa ndani na nje” alisema Ghati.
Naye
Afisa Maadili Mwandamizi kutoka Sekretarieti ya Maadili ya Viongozi wa Umma,
Hamadi Bakari alisema mafunzo hayo yatawasaidia wafanyakazi kufanya kazi kwa
kuzingatia sheria, kanuni na taratibu na hivyo kuepuka ukiukwaji wa maadili
unaoweza kuathili utendaji kazi wa taasisi na serikali kwa ujumla.
Aidha, alibainisha umuhimu
wa matumizi sahihi ya vifaa vya TEHAMA kama vile kompyuta na vifaa vya
kuhifadhia taarifa (flash) ili kulinda nyaraka za serikali na kuepusha madhara
yanayoweza kusababisha matatizo ya kimaadili au kinidhamu.
“Wafanyakazi
wakifuata taratibu za kazi na kanuni za utumishi wa umma wana uwezo mkubwa wa
kutojiingiza kwenye matatizo ya ukiukwaji wa maadili katika taasisi kwa maslahi
mapana ya serikali”, alisema Bakari.
Mmoja
wa washiriki wa mafunzo hayo Afisa Muuguzi wa JKCI, Jilala John alisema mafunzo
hayo yatamsaidia kuimarisha utoaji wa huduma bora kwa wagonjwa kwa kuzingatia
maadili, kuepuka vitendo vya rushwa na kutumia lugha ya faraja pamoja na
kutunza siri za wagonjwa.
“Tunaishukuru
serikali kupitia JKCI kwa kutupatia mafunzo haya ambayo ni muhimu kwetu katika
kutoa huduma kwa wagonjwa, kwani tumesisitizwa kutumia lugha za faraja na
kutunza siri za wagonjwa wetu”, alisema Jilala.
Mafunzo hayo ni sehemu ya juhudi za Serikali za kuimarisha misingi ya uadilifu, uwajibikaji na utawala bora katika taasisi za umma kwa lengo la kuongeza imani ya wananchi kwa watumishi wao.



Comments
Post a Comment