JKCI wamlilia Prof. Mahalu
Waziri wa Afya Mhe.Ummy Mwalimu akimkabidhi begi lenye vitendea kazi aliyekuwa Mwenyekiti wa bodi ya wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. William Mahalu mara baada ya kuizindua bodi hiyo Agosti mwaka jana jijini Dar es Salaam.
*********************************************************************************************************************************************
Wafanyakazi
wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wamepokea kwa masikitiko makubwa
taarifa ya kifo cha Prof. William Mahalu aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini
ya Taasisi hiyo na mmoja wa madaktari bingwa wa moyo wa kwanza hapa nchini.
Akizungumza na mwandishi wa habari hizi kwa njia ya simu akiwa
jijini Arusha Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Dkt. Peter Kisenge alisema Prof.
Mahalu alikuwa amelazwa JKCI kwaajili ya matibabu na alifariki usiku wa tarehe 20/08/2023.
Dkt. Kisenge alisema Prof. Mahalu ni miongoni mwa madaktari
bingwa wa kwanza watatu wa moyo nchini ambao jitihada zao ziliwezesha kuanzishwa
kwa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na kupatikana kwa matibabu ya
kibingwa ya moyo nchini Tanzania.
“Kifo cha Prof.Mahalu
ni pigo kubwa kwa Taasisi yetu licha ya kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya
JKCI pia alikuwa daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu na
mshauri mzuri katika kutekeleza majukumu yetu hii ni kutokana na uzoefu wake wa
muda mrefu aliokuwa nao,”.
“Tumempoteza mwasisi wa upasuaji wa moyo hapa nchini, ni pigo
kubwa kwetu sisi wataalamu wa magonjwa ya moyo kwani kupitia Prof. Mahalu
wataalamu wengi wa afya walivutiwa kujiendeleza na kuwa madaktari bingwa wa
upasuaji wa moyo hapa nchini”, alisema Dkt. Kisenge.
Kwa upande wake daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa
ya damu wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Evarist Nyawawa alisema alimfahamu Prof.William
Mahalu kuwa ni mmoja wa madaktari wa kwanza kabisa katika kusomea fani ya upasuaji
wa moyo hapa nchini ambaye ni mzalendo kwani
alipohitimu mafunzo yake ya upasuaji nchini Uingereza alirudi Tanzania na
kutaka kuanzisha upasuaji wa moyo lakini kulingana na vipaumbele vya serikali kwa
kipindi hicho hakuweza kufanya upasuaji huo na kwenda nchini Zimbabwe.
Dkt. Nyawawa alisema mara baada ya serikali kutia mkazo wa kutaka
kuanzisha upasuaji wa moyo ikawachagua wataalamu 26 na kuwapeleka nchini India kujifunza
upasuaji wa moyo wa fani mbalimbali na mara baada ya kurudi Prof. Mahalu kwa
uzalendo wake alirejea nchini ili kujumuika nao na kuanza kufanya upasuaji wa moyo katika
chumba cha upasuaji cha Taasisi ya Tiba ya Mifupa Muhimbili (MOI).
“Prof. Mhalu ndiye aliyetuwezesha sisi kuanza upasuaji wa
moyo hapa nchini kwasababu ukitoka kwenye mafunzo mara nyingi unahitaji mtu
ambaye atakusimamia ili uweze kufanya
upasuaji wa moyo,” alisema Dkt. Nyawawa.
“Baada ya kurudi hapa nchini Prof. Mahalu alikwenda Hospitali ya
Rufaa Bugando na akiwa kule sehemu kubwa ya muda wake aliutumia kuja kujumuika
na sisi kufanya upasuaji wa moyo, mbali
na hapo alitufundisha na kutafuta wataalmu wengi ambao mpaka leo wapo hapa kwenye Taasisi
ya Moyo wakihudumia wananchi,” alisema Dkt. Nyawawa.
“Prof. Mahalu alikuwa ni mzalendo,mshauri na mwenye maono
makubwa na ndio maana Mheshimiwa Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan alimchagua kuwa
mwenyekiti wa Bodi tangu Taasisi inaanzishwa, kutokana na maono yake katika
fani hii ya upasuaji wa moyo kwa sasa Taifa linajivunia kuwa na Taasisi ya Moyo
na kwa kiwango kikubwa karibu aina zote za upasuaji zinafanyika hapa nchini”
alisema Dkt. Nyawawa.
Licha ya kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mahalu pia alikuwa Mkuu wa Idara ya upasuaji
wa moyo na mishipa ya damu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Afya na Sayansi
Shirikishi Bugando (CUHAS).
Comments
Post a Comment