Waishukuru JKCI kwa kuwasogezea huduma za matibabu ya moyo
Mtafiti wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Loveness
Mfanga akimsikiliza mwananchi wa mkoa wa Kilimanjaro akijibu maswali ya ufahamu
kuhusu magonjwa yasiyoambukiza wakati wa kambi maalum ya siku tano ya upimaji
na matibabu ya moyo inayofanywa na wataalamu wa afya wa JKCI na wenzao wa
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mawenzi (MRRH)
Na: JKCI
**************************************************************************************************************
Wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro na mikoa ya jirani
wameishukuru Serikali kupitia Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa
kufikisha huduma za kibingwa za matibabu ya moyo mkoani Kilimanjaro.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti wakati wa kambi maalum ya
siku tano ya upimaji na matibabu ya moyo inayoendelea katika Hospitali ya Rufaa
ya Mkoa Mawenzi (MRRH) wananchi hao wamesema uhitaji wa matibabu ya kibingwa ya
magonjwa ya moyo mkoani humo ni mkubwa.
Elishadai Kimaro mkazi wa Kilimanjaro alisema kutokana na
wingi wa watu kutoka mkoa wa Kilimanjaro na mikoa ya jirani idadi ya watu
wanaohitaji matibabu ya moyo toka kambi hiyo kuanza imekuwa kubwa hivyo watu
kurudishwa nyumbani na kurejea tena siku inayofuata.
“Ninaiomba Serikali huduma za matibabu ya moyo hapa mkoani
kwetu zifanyike mara kwa mara au ikiwezekana tuwe na hospitali yetu inayotoa
huduma hizi za matibabu ya moyo, kambi maalum ya siku tano na baadaye wataalamu
kuondoka haitoshelezi kufikia mahitaji ya wanakilimanjaro”, alisema Kimaro.
Kimaro alisema kupitia kambi hiyo amepata nafasi ya kuchunguza
afya ya moyo wake kwani alikuwa na hofu ya kuwa na matatizo ya moyo lakini
hakujua ni nini afanye hadi hapo aliposikia ujio wa madaktari bingwa wa moyo
kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete hivyo naye kutumia fursa hiyo kupima.
Twaha Masawe mkazi wa Kilimanjaro alisema huduma za matibabu
ya moyo zinazotolewa na wataalamu wa afya kutoka JKCI amezipenda kutokana na
watoa huduma wanavyozungumza vizuri na wagonjwa na kuwapa elimu ya namna ya
kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza.
Masawe alisema kupitia kambi hiyo ameelimishwa kutokuacha
kutumia dawa za shinikizo la damu na kama ataacha anaweza kupata madhara katika
moyo wake ama kupata kiharusi.
“Namshukuru Mungu toka nilipogundulika kuwa na shinikizo la
damu nimekuwa nikitumia dawa, kupitia elimu niliyoipata hapa nitaendelea
kutumia dawa kama inavyotakiwa sitapenda kuona napata madhara mengine ya kiafya
yanayoletwa na tatizo la shinikizo la damu”, alisema Masawe
Naye Isha Rashidi Mkazi wa Kilimanjaro alisema ujio wa
madaktari bingwa wa moyo Mkoani Kilimanjaro umekuwa fursa kwake kupima moyo
wake kutokana na kupenda kwake kuchunguza afya yake lakini pia kuna hali
anazozipata mara kwa mara angependa kujua tatizo lake.
Isha alisema baada ya vipimo vya moyo kufanyika yupo tayari
kupokea majibu yake na kama atakuwa na shida ya moyo atafuata mtindo bora wa
maisha ili kuweza kuepukana na magonjwa ya moyo.
“Kuna wakati napata maumivu kwenye moyo na kusikia mapigo
yangu ya moyo kupiga kwa kasi japo sio mara kwa mara inaweza pita hata miezi
miwili ndio nikasikia tena hali hii, nipo tayari kujua shida niliyonayo na
kufuata ushauri wa madaktari”, alisema Isha
Comments
Post a Comment