Zaidi ya wananchi 7000 wafikiwa na huduma ya tiba mkoba
Daktari wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mawenzi (MRRH) Anandumi
Mmari akimpima kipimo cha kuangalia jinsi mfumo wa umeme wa moyo unavyofanya
kazi (Electrocardiography – ECG) mkazi wa Kilimanjaro aliyefika katika
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mawenzi (MRRH) kwaajili ya kupima moyo wakati wa
kambi maalum ya upimaji na matibabu ya moyo inayofanywa na wataalamu wa afya wa
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa MRRH.
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Kilalo
Barati akimpima shinikizo la damu mkazi wa Kilimanjaro aliyefika katika
Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mawenzi (MRRH) kwaajili ya kupima moyo wakati wa
kambi maalum ya upimaji na matibabu ya moyo inayofanywa na wataalamu wa afya wa
JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa MRRH
Na: JKCI
**************************************************************************************************************
Wananchi zaidi ya 7000 wafikiwa na huduma za uchunguzi na
matibabu ya moyo kupitia huduma ya tiba mkoba ijulikanayo kama Mhe. Dkt. Samia
Suluhu Hassan Outreach Services inayofanywa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI).
Hayo yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge leo wakati akifungua kambi maalum ya uchunguzi na matibabu ya moyo
inayoendelea mkoani Kilimanjaro katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mawenzi (MRRH).
Dkt. Kisenge alisema JKCI imekuwa ikifanya huduma ya tiba
mkoba katika mikoa mbalimbali ya Tanzania ambapo hadi sasa mikoa 11 ya Tanzania
bara na Zanzibar imeshafikiwa na wananchi takribani 700 kupewa rufaa kufika
JKCI kwa ajili ya matibabu zaidi.
Dkt. Kisenge ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo
alisema kambi hiyo ya matibabu ya moyo ni muendelezo wa tiba mkoba ijulikanayo
kama Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services yenye nia ya kuwafikishia
wananchi wa mkoa wa Kilimanjaro huduma ya tiba bobezi ya magonjwa ya moyo
mahali walipo.
“Nia ya JKCI kufanya kambi katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa
Mawenzi ni kuhakikisha kuwa tunaendeleza ujuzi kwa wataalamu wa afya wa hapa Mawenzi
pamoja na kuwasaidia wananchi wa Mkoa wa Kilimanjaro ambao wana magonjwa ya
moyo”,
“Mwitikio katika Mkoa huu wa Kilimanjaro umekuwa mkubwa sana ndani ya siku mbili tayari wagonjwa 600 wamefika katika Hospitali hii kwa ajili ya kupatiwa huduma, wagonjwa wengi wanaofika tumewakuta na shinikizo la damu na hii inatokea katika kila mkoa tunaoenda ugonjwa wa shinikizo la juu la damu umekuwa changamoto kwa watu wengi hivyo kupata madhara ya moyo kutanuka”,
Dkt. Kisenge alisema kuwa JKCI Itaendelea kufanya kambi hizo
katika mikoa mingine iliyobaki lengo likiwa kuendeleza dhana ya kufikisha
huduma za kibingwa kwa wananchi pale walipo.
“Katika kambi hii pia tunatoa huduma za uchunguzi na matibabu
ya magonjwa ya moyo kwa watoto ambapo kwa siku hizi mbili watoto waliofanyiwa
uchunguzi wengi wao wamekutwa na matundu kwenye moyo”, alisema Dkt. Kisenge
Kwa upande wake Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa
Mawenzi Dkt. EdnaJoy Munisi aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania chini ya uongozi wa Rais Dkt. Samia kwa kusogeza huduma karibu na
wananchi.
Dkt. EdnaJoy alisema Mwitikio wa kambi maalum ya matibabu ya
moyo umekuwa mkubwa tofauti na ilivyotarajiwa lakini timu ya wataalamu wa afya
wa Mawenzi kwa kushirikiana na wenzao waliotoka JKCI wamejipanga kuhakikisha
kuwa kila mwananchi anayefika katika Hospitali ya Mawenzi anapatiwa huduma kwa
wakati na kwa ufanisi.
“Tunawasihi wananchi wa mkoa wa Kilimanjaro na mikoa ya
jirani kuendelea kufika katika Hospitali ya Mawenza kupata fursa ya kupima moyo
kwani ni fursa ya pekee hasa kwa watu wazima ambao mara nyingi hushindwa
kusafiri kufuata huduma mahali zilipo”, alisema Dkt. EdnaJoy
Naye mwananchi aliyefika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa
Mawenzi kwaajili ya kufanya vipimo vya moyo Helen Kavishe alisema furaha ya
watu wa Kilimanjaro haieleziki kwa kufikishiwa huduma ya kibingwa ya uchunguzi
na matibabu ya moyo ambayo wengi wao hawakutarajia ingekuwa rahisi hivyo kupata
huduma hiyo.
Helen alisema kutokana na wingi wa watu imemchukua siku mbili
kupata huduma lakini kutokana na umuhimu wa matibabu ya moyo haikuwa shida kwa
wananchi wa mkoa wa Kilimanjaro kurejea tena siku ya pili ili kufanikisha
matibabu hayo.
“Tunaomba huduma kama hizi wakati mwingine zipelekwe na
maeneo ya vijijini ili wote kwa pamoja tuweze kufaidika na matibabu haya ya
kibingwa kwani kiuhalisia tunaona hapa uhitaji ni mkubwa na wagonjwa ni wengi”,
alisema Helen
Comments
Post a Comment