Dkt. Kisenge: Tumuenzi Prof. William Mahalu kwa kutoa huduma bora kwa wagonjwa

Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba akitoa neno la shukrani kwa wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa huduma nzuri walizompatia aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo marehemu Prof. William Mahalu wakati wa uhai wake leo wakati familia ya Prof. Mahalu ilivyofika JKCI kwaajili ya kushukuru. 

Mdogo wa aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Costa Mahalu akiwashukuru wafanyakazi wa Taasisi hiyo kwa kumhudumia aliyekuwa kaka yake marehemu Prof. William Mahalu wakati familia ya Prof. Mahalu ilipofika JKCI leo kwaajili ya kushukuru.

Prof. Costa Mahalu akimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge zawadi ya kuthamini mchango uliotolewa na Taasisi hiyo wakati wa kumuuguza hadi kumpumzisha aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo marehemu Prof. William Mahalu leo wakati familia hiyo ilivyofika JKCI kwaajili ya kushukuru.


Baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakisikiliza wakati famila ya aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo marehemu Prof. William Mahalu ilivyofika JKCI leo kwaajili ya kushukuru.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiwa katika picha ya pamoja na wanafamilia ya Mahalu leo baada ya familia hiyo kufika JKCI kwaajili ya kutoa neno la shukrani kwa huduma alizopatiwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi hiyo marehemu Prof. William Mahalu wakati wa uhai wake.

Na: JKCI
******************************************************************************************************

Madaktari wa moyo wametakiwa kumuenzi aliyekuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) marehemu Prof. William Mahalu kwa kutoa huduma bora kwa wagonjwa wenye matatizo ya moyo.

Rai hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati wa hafla fupi iliyofanywa na familia ya marehemu Mahalu kutoa neno la shukrani kwa wafanyakazi wa Taasisi hiyo kwa kumuuguza hadi kumpumzisha Marehemu Prof. William Mahalu.

“Marehemu Prof. Mahalu ni mlezi wetu, asilimia kubwa ya wataalamu wa magonjwa ya moyo hapa wamefundishwa naye, Tunamshukuru Mungu kwa mambo makubwa ambayo ameyafanya katika sekta hii ya afya hasa upande wa upasuaji wa moyo, tunaahidi kuyaenzi yote ili tusije tukapoteza jina lake”, alisema Dkt. Kisenge.

Dkt. Kisenge alisema kabla ya kuanza safari yake ya matibabu nchini India marehemu Prof. William Mahalu alikaa naye na kumuomba kuziendeleza huduma za matibabu ya moyo kwa kuwafikia wananchi mahali walipo.

“Sasa hivi JKCI tumekuwa tukifanya huduma ya tiba mkoba kwa kuwafuata wananchi mahali walipo na kuwapa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo hii yote ni jitihada za marehemu Prof. Mahalu kutusihi tuwafikishie wananchi huduma karibu”, alisema Dkt. Kisenge

Dkt. Kisenge alisema ukiizungumzia historia ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete uwezi kuacha kumzungumzia Prof. Mahalu kwani yeye ni miongoni mwa waanzilishi wa upasuaji wa moyo hapa nchini.

Kwa upande wake Waziri Mkuu Mstaafu Mhe. Jaji Joseph Sinde Warioba aliwashukuru wataalamu wa afya wa JKCI kwa kumhudumia kwa kiwango cha juu marehemu Prof. William Mahalu na kuhakikisha kuwa afya yake inaimarika.

“Huduma mlizompa hapa zilikuwa za hali ya juu, wakati wote wahudumu walikuwa naye karibu, mlijitahidi sana kuokoa maisha yake lakini Mungu akampenda zaidi”, alisema Mhe. Jaji Warioba.

Jaji Warioba alisema marehemu Prof. William Mahalu kimwili hayupo lakini kiroho babo yupo kwani ameweza kuifanya kazi yake kwa kutoa mchango mkubwa hapa nchini hivyo kuacha msingi katika huduma za kibingwa za upasuaji wa moyo.

Naye mdogo wa marehemu Prof. Costa Mahalu aliwataka wafanyakazi wa JKCI na wataalamu wa afya wengine wanaomfahamu marehemu Prof. William Mahalu kuyasherehekea maisha yake kwa kuvienzi na kuviendeleza vile alivyokuwa akivifanya wakati wa uhai wake.

Prof. Costa alisema wafanyakazi wa JKCI wamekuwa sehemu ya familia ya Prof. Mahalu kwa upendo, ushirikiano na umoja waliokuwa nao tangu kuumwa hadi kumpumzisha marehemu Prof. William Mahalu.

“Tunamshukuru Mungu mapenzi yake ameyatimizwa, marehemu Prof. William Mahalu ametuachia upendo na familia ya JKCI tunamshukuru Mungu kwa hilo”, alisema Prof. Costa

 

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari