Watu 689 wapimwa moyo Geita

Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Salehe Mwinchete akimpima jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiograph – ECHO) mwananchi wa Geita aliyefika katika banda la JKCI wakati wa maonyesho ya sita ya kitaifa ya teknolojia ya madini yaliyomalizika leo Mkoani Geita. Jumla ya watu 689 wamepatiwa huduma katika banda hilo.

Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) anayetoa huduma katika kliniki maalumu Grace Mbanga akimpima shinikizo la damu mwananchi wa Geita aliyetembelea banda la JKCI wakati wa maonyesho ya sita ya kitaifa ya teknolojia ya madini yaliyomalizika leo Mkoani Geita. Jumla ya watu 689 wamepatiwa huduma katika banda hilo.

Afisa kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Elimiliki Kileo akimpima urefu, uzito na uwiano wa urefu na uzito mkazi wa Geita aliyetembelea banda la JKCI wakati wa maonyesho ya sita ya kitaifa ya teknolojia ya madini yaliyomalizika leo Mkoani Geita. Jumla ya watu 689 wamepatiwa huduma katika banda hilo.

Wananchi wa Mkoa wa Geita wakiwa katika foleni ya kupata huduma katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa maonyesho ya sita ya kitaifa ya teknolojia ya madini yaliyomalizika leo mkoani Geita. Jumla ya watu 689 wamepatiwa huduma katika banda hilo.

Na JKCI

*****************************************************************************************************************

Watu 689 wamepata huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo wakati wa maonyesho ya sita ya kitaifa ya Teknolojia ya madini yaliyokuwa yakifanyika katika viwanja vya EPZA Bombambili mkoani Geita na kumalizika leo.

Maonyesho hayo yalianza Septemba 20 hadi septemba 30, 2023 na kutoa fursa kwa wananchi wa Geita na mikoa ya jirani kupima magonjwa ya moyo, shinikizo la damu na sukari kwenye damu katika kliniki maalum iliyokuwa ikifanywa na wataalamu wa afya kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Akizungumza na waaandishi wa habari leo wakati wa kuhitimisha maonyesho hayo Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Salehe Mwinchete alisema katika maonyesho hayo watu 548 wamefanyiwa kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiograph – ECHO).

“Kati ya watu 689 waliopatiwa huduma katika banda la JKCI watu wazima walikuwa 669 wanaume wakiwa 200 na wanawake 469 huku watoto wakiwa 20”, alisema Dkt. Salehe.

Dkt. Salehe alisema wananchi 213 wamekutwa na magonjwa mbalimbali ya moyo ukiongoza ugonjwa wa shinikizo la juu la damu, sukari kwenye damu, moyo kutanuka, mishipa ya damu kuziba, magonjwa ya valvu (RHD) na magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo kwa watoto ambayo ni matundu na mishipa ya damu kutokuwa sawa.

“Tumetoa rufaa kwa watu 28 watoto wakiwa watano na watu wazima 23 kufika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa ajili ya kupatiwa matibabu zaidi huku wengine wakitakiwa kufanyiwa upasuaji wa moyo kutokana na matatizo waliyonayo”, alisema Dkt. Salehe

Dkt. Salehe alisema kuwa kati ya watu 173 waliokutwa na tatizo la shinikizo la juu la damu zaidi ya nusu walikuwa na tatizo hilo bila ya wao kujijua hivyo kuanzishiwa kliniki ya kufuatilia tatizo hilo kupunguza athari ambazo wanaweza kuzipata kama hawatatibu tatizo la shinikizo la juu la damu.

Aidha Dkt. Salehe amewahasa wananchi kufanya uchunguzi wa afya zao mara kwa mara, kufanya mazoezi, kula matunda na mboga za majani kwa wingi, pamoja na kupata usingizi wa kutosha ili kuweza kuwa na afya bora.

Kwa upande wake mwananchi aliyepatiwa matibabu katika kliniki hiyo maalumu ya uchunguzi wa magonjwa ya moyo Ester John aliushukuru uongozi wa JKCI kwa kuwezesha huduma za matibabu ya moyo kwa wananchi wa Geita kwani wengi wao wasingeweza kupata huduma hiyo.

“Nawashukuru sana kwa huduma yenu nzuri mnayoitoa katika banda hili, ninawaomba muendelee kuwa na moyo huu wa kujitoa kwetu sisi wana Geita na hasa sisi walemavu, leo nimekutwa na shinikizo la juu la damu na daktari kanipa ushauri mzuri naahidi kuufanyia kazi”, alisema Ester

Ester ameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwekeza katika sekta ya afya na kuwapa fursa wananchi kuchunguza afya zao bila gharama kama ambavyo ilikuwa katika banda la JKCI.

“Nilikuwa natamani sana kupima moyo wangu, nilikuwa naisikia tu Taasisi hii ya Moyo Jakaya Kikwete leo nimefika na kujionea mimi mwenyewe wataalamu wa afya wanatoa huduma nzuri”, alisema Ester

Naye mwenyeji wa Kagera Hendry Bamgaya alisema ametembelea maonyesho hayo akiwa na lengo la kufuata huduma za matibabu ya moyo zilizokuwa zikitolewa kwenye banda la JKCI baada ya kusikia uwepo wa wataalamu wa afya kutoka JKCI kwenye maonyesho hayo.

“Nimepokelewa vizuri katika banda la JKCI, nimepimwa moyo wangu na kukutwa na tatizo la moyo kutanuka. Nashukuru daktari kaniandikia dawa za kutumia na kunipa ushauri wa nini cha kufanya”, alisema Hendry

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari