Idadi ya wagonjwa wa moyo na shinikizo la damu yaongezeka nchini

 


Waziri wa Afya Mhe.Ummy Mwalimu akizungumza na wananchi waliohudhuria maadhimisho ya siku ya moyo duniani yaliyofanyika leo katika viwanja vya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group iliyopo Temeke jijini Dar es Salaam.


Waziri wa Afya Mhe.Ummy Mwalimu akisaini kitabu cha wageni mara baada ya kufika katika  viwanja vya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group iliyopo Temeke jijini Dar es Salaam kwaajili ya kushiriki maadhimisho ya siku ya moyo duniani.

Waziri wa Afya Mhe.Ummy Mwalimu akikagua maeneo mbalimbali ya  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group alipofika katika Hospitali hiyo leo  kwaajili ya maadhimisho ya siku ya moyp duniani. 

 

Baadhi ya wananchi waliofika  katika viwanja vya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group iliyopo Temeke jijini Dar es Salaam wakipata huduma za upimaji na matibabu ya magonjwa ya moyo wakati wa maadhimisho ya siku ya moyo duniani.


Baadhi  ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wananchi wakimsikiliza Waziri wa Afya Mhe.Ummy Mwalimu wakati akizungumza nao katika  maadhimisho ya siku ya moyo duniani yaliyofanyika leo katika viwanja vya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group iliyopo Temeke jijini Dar es Salaam.


Baadhi  ya  wananchi wakisoma vipeperushi vya shinikizo la juu la damu wakati wa  maadhimisho ya siku ya moyo duniani yaliyofanyika leo katika viwanja vya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group iliyopo Temeke jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Afya Mhe.Ummy Mwalimu akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), wanachama wa Chama cha Madaktari Bingwa wa Moyo Nchini (TCS) na wawakilishi wa makampuni ya uingizaji na usambazaji wa dawa za binadamu wakati wa maadhimisho ya siku ya moyo duniani yaliyofanyika leo JKCI Dar Group Hospitali.

**************************************************************************************************************************************************************************************

Takwimu za wizara ya Afya kupitia MTUHA (DHIS -2) zinaonesha kumekuwa na ongezeko la asilimia 9.4 kwa magonjwa ya moyo na shinikizo la damu pekee kutoka wagonjwa milioni 2.5 mwaka 2017 hadi wagonjwa 3.4 mwaka 2022.

Hayo yamesemwa leo na Waziri wa Afya Mhe.Ummy Mwalimu wakati akizungumza  na wananchi waliohudhuria maadhimisho ya siku ya moyo duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group iliyopo Temeke jijini Dar es Salaam.

Mhe. Waziri Ummy alisema taarifa za ufuatiliaji wa magonjwa yasiyoambukiza kutoka mwaka 1980 hadi mwaka 2020 inaonesha ongezeko la magonjwa ya shinikizo la juu la damu na kisukari katika jamii kutoka asilimia 1 hadi 9 kwa wagonjwa wa kisukari na kutoka asilimia 5 hadi 26 kwa wagonjwa wa shinikizo la juu la damu.

“Magonjwa haya mawili ndiyo chanzo kikuu cha magonjwa ya moyo, figo pamoja na ugonjwa wa kiharusi hivyo ongezeko hili ni tishio kwa ustawi wa afya ya jamii yetu na ndiyo sababu inatuweka hapa leo kujadili mikakati ya kukabiliana nayo”,.

“Matatizo haya ya moyo na ugonjwa wa kiharusi yanaweza kuzuilika kwa mtu mmoja mmoja na jamii yetu kuweza kuchukuwa hatua. Kwa mujibu wa maelezo ya wataalam sababu zinazopelekea kuongezeka kwa magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo magonjwa ya kiharusi ni pamoja na kutozingatia ulaji unaofaa ambapo kwa nchi yetu inaonesha asilimia 3 tu ya watu wazima wanatumia kiasi cha wastani wa kutosha cha matunda na mbogamboga”, alisema Mhe. Ummy Mwalimu.

Akizungumzia kuhusu suala la kufanya mazoezi waziri Ummy alisema idadi ya watu wazima wanaofanya mazoezi ni kubwa ukilinganisha na watoto na vijjana ambapo takwimu zinaonesha kwa takribani asilimia 20 ya vijana wote wenye umri wa chini ya miaka 17 wanaendekeza tabiabwete na kutoshughulisha miili yao ipasavyo.

“Ninawasihi ndugu zangu mtenge muda wa kufanya mazoezi japo dakika 150 kwa wiki na mazoezi haya siyo lazima yawe ya kukimbia yanaweza kuwa hata ya kutembea, kupima afya japo mara moja kwa mwaka, kupunguza vilevi na kuacha kabisa matumizi ya tumbaku , kupunguza matumizi yaliyokithiri ya chumvi, sukari na mafuta ya  kupikia yenye lehemu na kuzingatia ushauri wa muhimu unaotolewa na madaktari  kwa kufanya hivi tutaweza kukabiliana  na ongezeko la magonjwa haya yasiyoambukiza ikiwemo tatizo la moyo pamoja na ugonjwa wa kiharusi”, alisema Mhe. Ummy.

Aidha Mhe. Waziri Ummy aliitaka Taasisis ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) pamoja na Hospitali za Kanda Maalum kufanya ulezi wa kuwajengea uwezo hospitali zilizo chini ya ngazi zao kwenye mikoa na kanda walizopo kwa kushuka chini na kufanya kambi za matibabu za pamoja, huduma mkoba na kuwaalika wataalam kutoka hospitali hizo kuja kujishikiza kwao na kujifunza stadi mbalimbali kutoka kwa muda mfupimfupi.

Akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mkuu wa wilaya ya Temeke Mhe. Mobhare Matinyi aliishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kufanya maadhimisho ya siku ya moyo duniani katika wilaya yake na kuwaomba wananchi wajitokeze kwa wingi katika zoezi la upimaji na matibabu ya moyo.

“Ninawapongeza wananchi mliojitokeza siku ya leo kwaajili ya kupima afya zenu, ninawaomba wananchi wengi zaidi mjitokeze siku ya kesho ambapo zoezi la upimaji litakuwa linaendelea pia tutakuwa na matembezi ya kupambana na magonjwa yasiyoambuikiza yatakayoanzia uwanja wa Taifa na kuishia hapa JKCI Hospitali ya Dar Group”, alisema Mhe.Matinyi .

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya alimshukuru waziri wa Afya kwa kukubali kuwa mgeni rasmi katika maadhimisho hayo na kusema kuwa wataalamu wamejipanga kufanya upimaji wa magonjwa ya moyo kwa wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam na mikoa ya jirani.

Dkt. Angela alisema katika kupambana na magonjwa yasiyoambukiza Taasisi hiyo imekuwa ikitoa elimu kwa wananchi ya jinsi ya kuepukana na magonjwa ya moyo hii ikiwa ni pamoja na kutoa huduma ya tiba mkoba ijulikanayo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan outreach Services kwa kuwafuata wananchi mahali walipo na kufanya upimaji pamoja na kutoa ushauri.

“Tunakwenda katika mikoa mbalimbali hapa nchini kutoa huduma za upimaji na matibabu ya magonjwa ya moyo kwa wananchi,  katika maeneo hayo kumekuwa na uitikio mkubwa na wengi wa watu tunaowapima tunawakuta na tatizo la shinikizo la juu la damu, kutanuka kwa misuli ya moyo, umeme wa moyo, kuziba kwa mishipa ya damu ya moyo  na kwa watoto tunawakuta na matundu pamoja na mishipa yao ya damu kutokukaa katika mpangilio wake”, alisema Dkt. Angela.

Naye Rais wa Chama cha Madaktari Bingwa wa Moyo Nchini (TCS) Robert Mvungi alisema historia ya maadhimisho ya siku ya moyo duniani ilianza kuadhimishwa mwaka 2000 na Shirikisho la Moyo Duniani kwakuona kuna umuhimu wa kuwa na siku hyo hii ni  kutokana na matatizo ya moyo kuzidi kuongezeka.

“Duniani kote siku hii inaadhimishwa kwa kutoa uelewa kwa wananchi kuhusu magonjwa ya moyo ili wajue jinsi ya kujikinga nayo pia tunafanya upimaji wa magonjwa haya kwa wananchi na upimaji huu unafanyika bila malipo yoyote yale ili kila mwananchi aweze kufikiwa na huduma hii”, alisema Dkt. Mvungi.

Katika maadhimisho hayo ya siku ya moyo duniani Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na Chama cha Madaktari Bingwa wa Moyo Nchini (TCS) na makampuni mbalimbali ya uingizaji na usambazaji wa dawa za binadamu wanatoa huduma za upimaji na matibabu ya moyo pamoja na kutoa dawa kwa wananchi wanaokutwa na  matatizo. Huduma hii ya siku mbili inatolewa bila malipo yoyote yale JKCI Dar Group Hospitali.


 

 

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari