Wataalamu wa upasuaji wa moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) na mwenzao kutoka Chuo Kikuu cha Jagiellonian cha nchini Poland
Prof. Tomasz Mroczek
wakifanya upasuaji wa kurekebisha mishipa ya damu ya moyo ambayo haijakaa
katika mpangilio wake wakati wa kambi maalumu ya siku tano ya matibabu ya
magonjwa ya moyo kwa watoto iliyofanyika JKCI. Prof. Mroczek ni mmoja wa
madaktari bingwa wachache duniani wanaofanya upasuaji mgumu wa moyo kwa watoto
alifika JKCI ili kuona namna ambavyo madaktari wa taasisi hiyo wanavyofanya
upasuaji na kuangalia jinsi watakavyoweza kushirikiana katika kufanya upasuaji
mgumu zaidi.
***********************************************************************************************************************************************************************************************************
Mmoja wa madaktari
bingwa wachache duniani wanaofanya upasuaji mgumu
wa moyo kwa watoto Prof. Tomasz Mroczek kutoka Chuo Kikuu cha Jagiellonian cha nchini Poland ameipongeza
Serikali kwa kusomesha wataalamu wa moyo na kununua vifaa tiba vinavyotumia
teknolojia ya kisasa.
Prof. Mroczek alizitoa pongezi hizo hivi karibuni wakati
akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya kumalizika kwa kambi maalumu ya siku tano ya matibabu ya
magonjwa ya moyo kwa watoto waliyoifanya katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI).
Prof. Mroczek alisema hii ni mara yake ya kwanza kufika hapa nchini na walikuja kuona namna ambavyo madaktari wa JKCI
wanavyofanya upasuaji wa moyo na kuangalia jinsi watakavyoweza kushirikiana
katika kufanya upasuaji mgumu zaidi.
“Kitu nilichokitegemea kukikuta siyo nilichokikuta hapa, nimekuta
madaktari wanafanya upasuaji mgumu wa kurekebisha mishipa ya damu ya moyo
ambayo haijakaa katika mpangilio wake kwa kutumia muda mfupi tofauti na nchi zingine
nilizokwenda pia kuna wataalamu wazuri na vifaa tiba viko vya kutosha na vya
kisasa vinavyoenda na teknolojia ya matibabu ya moyo inayotumika katika nchi
zilizoendelea”,.
“Nimekutana na watalamu wazuri ambao tumefanya nao upasuaji wa
moyo kwa watoto wenye matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo ninaamini ushirikiano huu
utakuwa endelevu ili sote kwa pamoja tuweze kuwahudumia watanzania wenye
matatizo ya moyo”, alisema Prof. Mroczek.
Kwa upande wake Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge
aliwashukuru wataalamu hao kutoka nchini Poland ambao walifanya upasuaji mkubwa
kwa watoto na mdogo kwa watu wazima na kusema kuwa ujio wao unaenda kufungua milango ya mafunzo kwa
madaktari hapa nchi.
Dkt. Kisenge ambaye pia ni daktari
bingwa wa moyo alisema kwa muda wa siku
tano ambao madaktari hao walikuwepo katika Taasisi hiyo wameweza kufanya
upasuaji mgumu wa moyo na kutoa mafunzo na ujuzi kwa wataalamu wa JKCI.
“Tulisaini makubaliano na
wenzetu wa Chuo Kikuu cha Jagiellonian cha
nchini Poland ya
kushirikiana katika mafunzo, tafiti na kufanya matibabu. Ushirikiano huu
umeanza kufanya kazi na utakwenda kufungua milango ya kufanya tafiti mbalimbali
zitakazoleta manufaa kwa nchi ikiwepo uingizaji wa fedha za kigeni”, alisema
Dkt. Kisenge.
"Walipofika wametuonyesha
vitu ambavyo kwetu sisi ilikuwa ni vigunu kufanya kwani wamekuja kutuonyesha
namna ya kutumia mitambo iliyopo ikiwepo kurekebisha mishipa ya damu kwenye
moyo”, alisema Dkt. Kisenge.
Prof. Bartconie Guzlk kutoka Chuo Kikuu cha Jagiellonian cha nchini Poland ambaye kwa kushirikiana
na wataalamu wa kuzibua mishipa ya damu wa JKCI walifanya upasuaji mgumu (Complex Percutaneous
Coronary Intervention – PCI) wa kuzibua mshipa wa moyo iliyokuwa imeziba kwa
asilimia 99 na hivyo kushindwa kupitisha damu vizuri kwa wagonjwa 14 alisema madaktari wa Tanzania
wapo tayari kujifunza kwaajili ya kusaidia watu wenye matatizo ya moyo kwani wanafanya kazi kwa bidii na umakini mkubwa.
"Tutaendelea kushirikiana na
JKCI katika kufanyakazi ya kuwatibu watu wenye matatizo ya moyo na kufanya
tafiti zitakazosaidia katika matibabu, hii ni mara yangu ya kwanza kuja Tanzania
nimefurahi na nimeipenda hii nchi ninaahidi tutaendelea kushirikiana zaidi”, alisema
Prof. Guzlk.
Uzibuaji
wa mishipa hiyo ulifanyika kwa njia ya upasuaji wa moyo kwa kutumia tundu dogo
(Minimum Invasive Surgery) bila kufungua kifua kwa kutoboa mshipa kwenye paja
(Percutaneous Coronary Angioplasty) kwa kutumia mtambo wa Cathlab (Catheterization
Laboratory) ambayo ni maabara inayotumia mionzi maalum kwa ajili ya uchunguzi
na tiba za magonjwa ya moyo.
Awali Mkurugenzi wa Upasuaji wa
JKCI Dkt. Angela Muhozya amesema uwepo wa madaktari hao ambao ni Daktari
bingwa wa moyo na Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto umetoa fursa
kwa wao kujifunza mambo makubwa zaidi katika upasuaji wa moyo.
"Tangu tumeingia nao
mkataba ni mwaka sasa na tulipopata nafasi ya kuwatembelea wenzetu katika chuo
chao tuliona ni namna gani wanafanya upsauaji wa mishipa ya damu pamoja
na moyo tukatumia fursa hiyo kuomba waje nchini ili na sisi tuweze
kufaidika,"alisema Dkt. Angela.
Naye daktari bingwa wa upasuaji moyo kwa watoto wa
JKCI Godwin Sharau alisema uwepo wa madaktari bingwa kutoka Poland umesaidia
kwa wao kujifunza zaidi kwani madaktari hao ndani ya siku tatu wamefanikiwa
kuwafanyia upasuaji mkubwa watoto watano ambao ulikuwa mgumu kwa wao kufanya.
"Tumekutana na madaktari
ambao tunaamini tunaweza kufika kwenye viwango vya juu kutokana na utendaji
wetu na pia kwetu ni fursa kwani Prof. Mroczek anatumiwa na watu wengi
duniani katika kusaidia watoto”, alisema Dkt. Sharau.
Comments
Post a Comment