Dkt. Kisenge: Dar jitokezeni kupima moyo
Mwakilishi wa kampuni ya dawa za binadamu ya Micro Labs Limited – Laborex Tanzania Zawadi Mbasha akizunguma na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge kuhusu dawa za magonjwa ya moyo na kisukari wanazozitoa kwa wananchi waliofika katika kambi maalumu ya siku mbili ya upimaji na matibabu ya moyo inayofanyika JKCI Hospitali ya Dar Group kwaajili ya kupata huduma za matibabu ya moyo.
Picha na JKCI
Rai hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati akizungumza
na wananchi waliofika katika zoezi la upimaji na matibabu ya moyo linalofanyika
katika kambi maalumu ya siku mbili
inayofanyika JKCI Hospitali ya Dar Group.
Dkt. Kisenge alisema wananchi wakipata mapema huduma za
uchunguzi na matibabu ya moyo wataisaidia Serikali kupunguza gharama za kulipia
matibabu hayo kwani matibabu ya kibingwa ikiwemo upasuaji wa moyo gharama zake
ni kubwa.
“Hadi sasa watu 84 wameshapata huduma za uchunguzi na
matibabu ya moyo na wengi tuliowaona
wanamatatizo ya shinikizo la juu la damu, huu ni ugonjwa ambao tumekuwa tukiwakuta nao
wananchi wengi tunaowaona katika maeneo mbalimbali hapa nchini”, alisema Dkt.
Kisenge.
Dkt. Kisenge alisema magonjwa ya moyo yamekuwa yakiongoza kwa
kuua watu wengi hapa Duniani ambapo kwa takwimu za Shirika la Afya Dunia (WHO) watu
milioni 17 wanapoteza maisha kila mwaka kutokana na magonjwa hayo.
“Taasisi yetu imeamua
kusogeza upatikanaji wa huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya moyo kwa
kuwafuata wananchi mahali walipo, tunahitaji wananchi wenye matatizo ya moyo wapate
huduma za matibabu mapema”,.
“Huduma hii inajulikana kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu
Hassan Outreach Services tunawafuata wananchi mahalli walipo na kutoa huduma za
uchunguzi na upimaji wa magonjwa yasiyo
ya kuambukiza yakiwemo ya moyo na kisukari
pia tunatoa ushauri wa jinsi ya kuepukana na magonjwa haya pamoja na elimu ya
lishe bora”, alisema Dkt. Kisenge.
Kwa upande wao wananchi waliopata huduma za uchunguzi na
matibabu ya moyo waliishukuru Serikali kwa huduma waliyoipata na kuomba Taasisi
hiyo kutoa huduma hiyo mara kwa mara kwani wengi wao inawawia vigumu kwenda
moja kwa moja JKCI kupata matibabu hii ni kutokana na utaratibu uliopo wa kupata
rufaa.
“Taratibu za kwenda kutibiwa JKCI kama hauna bima ya afya ni
lazima uwe na rufaa na kupata rufaa mlolongo wake ni mrefu, baada ya kuona
tangazo hili niliona ni vyema nami nije kufanya uchunguzi wa afya yangu
nimepima nakupewa dawa za moyo. Nawaomba wananchi wenzangu tutumie nafasi hii
kuja kupima magonjwa ya moyo”, alisema Selemani Athumani mkazi wa Mbagala.
“Niliona tangazo la upimaji huu katika mitandao ya kijamii
nikaona nije kupima na kujua kama nina matatizo ya moyo au la hii ni kutokana
na maisha ninayoishi sifanyi mazoezi na hata ulaji wangu wa chakula siyo mzuri
kwani sili vyakula bora”, alisema Birgitha Boaz mkazi wa River Side.
Naye Festus Asenga mwakilishi wa kampuni ya dawa za binadamu
ya Micro Labs Limited – Laborex Tanzania ambao wako katika kambi hiyo kwaajili
ya kutoa huduma ya dawa kwa watu wanaokutwa na matatizo ya moyo na kisukari
alisema kampuni hiyo iliona waungane na JKCI kwa kutoa dawa bure kwa wananchi watakaokutwa na
matatizo.
“Tunatoa dawa za siku 30 bure kwa watu wanaokutwa na matatizo
kwani wananchi wengi hawana uwezo wa kununua dawa kwa kufanya hivi tunawasaidia
kuanza matibabu mapema”, alisema Asenga.
Katika kambi hiyo ya uchunguzi na matibabu ya moyo ya siku mbili huduma zinazotolewa ni upimaji wa sukari mwilini, urefu, uzito, uwiano baina ya urefu na uzito, shinikizo la damu, elimu ya lishe bora na matumizi sahihi ya dawa, vipimo vya kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi pamoja na umeme wa moyo na dawa za moyo na kisukari.
Comments
Post a Comment