Watoto 35 kufanyiwa upasuaji wa moyo katika kambi maalum ya Mfalme Salman
*************************************************************************************************************
Watoto 35 wenye magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo yaani
matundu na mishipa ya damu ya moyo kuziba au kukaa vibaya wanatarajiwa
kufanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo katika kambi maalum ya matibabu ya moyo inayofanyika
katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
Kambi hiyo ya siku tano iliyoanza leo Septemba 9, 2023
inafanywa na madaktari bingwa wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
kwa kushirikiana na wenzao kutoka Kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya
Kibinadamu kilichopo nchini Saud Arabia.
Akizungumza leo jijini Dar es Salaam Mkuu wa Idara ya
Magonjwa ya Moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt.
Sulende Kubhoja alisema madaktari hao kutoka Kituo cha Mfalme Salman wamekuwa
na utaratibu wa kila mwaka kufanya kambi ya matibabu ya moyo na Taasisi hiyo
lengo likiwa kubadilishana ujuzi na kuongeza maarifa.
Dkt. Kubhoja alisema katika kambi wanazofanya na madaktari kutoka
Kituo cha Mfalme Salman watoto wengi wamekuwa wakifanyiwa upasuaji kwa kipindi
cha muda mfupi hivyo kupunguza idadi ya watoto wanaosubiri kufanya upasuaji wa
moyo.
“Madaktari wa JKCI tukiwa wenyewe tunaweza kufanya upasuaji
mkubwa wa moyo kwa watoto wawili hadi watatu kwa siku lakini wakija hawa wenzetu
kwasababu wanakuja wengi ushirikiano unakuwa mkubwa na kupelekea kutoa huduma
ya upasuaji wa moyo kwa watoto watano hadi sita kwa siku”, alisema Dkt. Kubhoja
Aidha Dkt. Kubhoja amewaomba wazazi wenye watoto wenye
magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo kujitokeza kwa wingi ili watoto wao waweze
kupatiwa huduma za matibabu kwa wakati.
Kwa upande wake daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto
kutoka Kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya Kibinadamu kilichopo nchini Saud
Arabia Mohammed Shihata alisema ujio wao hapa nchini ni kampeni ya kutoa huduma
za upasuaji wa moyo kwa watoto wenye magonjwa ya moyo.
Dkt. Shihata alisema madaktari kutoka Kituo cha Mfalme Salman
wanapenda kufanya kazi na wataalamu wa afya wa JKCI kwasababu ya ukarimu wa
watu wa Tanzania, uwajibikaji wa wataalamu wa afya wa JKCI na ujuzi ulipo
kwa wataalamu hao.
“Kambi zetu za matibabu ya moyo kwa watoto hapa Tanzania ni
moja ya kambi ambazo zinakuwa zimeratibiwa vizuri hivyo mara nyingi kutupa
nafasi ya kuanza kazi siku ya kwanza tunayofika”, alisema Dkt. Shihata.
Dkt. Shihata alisema ujio wa wataalamu hao umekuja na vifaa
tiba vilivyotolewa na Kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya Kibinadamu
kilichopo nchini Saud Arabia kwa ajili ya kuwafanyia upasuaji watoto 35 wenye
magonjwa ya moyo.
Naye mzazi ambaye mtoto wake anatarajiwa kufanyiwa upasuaji
katika kambi hiyo kutoka Mkoani Kigoma Merry Japhet alisema anamshukuru Mungu
kwa mwanaye kuwekwa kwenye listi ya watoto wakataopatiwa matibabu katika kambi
hiyo kwani ni matamanio yake kuona mtoto wake anapona kabisa tatizo la moyo.
“Mungu akijalia mwanangu atafanyiwa upasuaji wa moyo,
nilimzaa akiwa na tundu kwenye moyo na mishipa yake ya damu ikiwa imesinyaa, akiwa
bado na miezi michache baada ya kuzaliwa alikuwa akiumwa mara kwa mara,
nilimpeleka Hospitali wakaniamba ana tatizo la nimonia na kumchoma sindano za
nimonia lakini hakupona”, alisema Merry.
Merry alisema siku moja akiwa anamuogesha mwanaye aliona
upande wa kushoto wa kifua umevimba hivyo kuamua kumpeleka Hospitali ya Wilaya
na kugundulika kuwa mtoto ana shida ya moyo hivyo kuanza kufuatilia matibabu ya
moyo katika hospitali ya Bugando, Benjamini Mkapa na baadaye kupewa rufaa
kufika JKCI.
“Namshukuru Mungu nilivyofika hapa JKCI nimepokelewa vizuri,
mtoto amepatiwa tiba kwa kipindi cha mwezi mmoja hadi sasa anaendelea vizuri
ndio wakaona ni wakati sasa afanyiwe upasuaji wa moyo kurekebisha changamoto
alizonazo”, alisema Merry.
Comments
Post a Comment