Watoto 24 wafanyiwa upasuaji wa moyo katika kambi ya matibabu inayoendelea JKCI
Madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo na
mishipa ya damu kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
wakishirikiana na mwenzao kutoka Kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya
Kibinadamu kilichopo nchini Saudi Arabia Mohammed Shihata kumfanyia upasuaji wa
kurekebisha mishipa ya damu mtoto ambaye mishipa yake ya damu haipo katika
mpangilio wake wakati wa kambi maalum ya siku tano ya matibabu ya magonjwa ya
moyo kwa watoto inayoendelea JKCI.
Mtaalamu wa kuendesha mashine ya kuusaidia moyo na mapafu kufanya kazi (Heart Lung Machine) wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Robert Luchemba na mwenzake kutoka Kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya Kibinadamu kilichopo nchini Saudi Arabia wakiendesha mashine hiyo wakati wa kambi maalum ya siku tano ya matibabu ya moyo kwa watoto inayofanyika JKCI.
Daktari bingwa wa usingizi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Steven Nandi akiweka sawa mashine ya kuangalia mapigo ya moyo ya mgonjwa (monitor) wakati wa kambi maalum ya upasuaji wa moyo kwa watoto inayofanywa na madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao kutoka Kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya Kibinadamu kilichopo nchini Saudi Arabia.
******************************************************************************************************************************************************************************
Watoto 24 wenye matatizo ya moyo ya
kuzaliwa nayo wamefanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo katika kambi maalumu ya
matibabu ya moyo inayoendelea katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
Akizungumza kuhusu kambi hiyo Mkuu wa
kitengo cha upasuaji wa moyo kwa watoto wa JKCI Dkt. Godwin Sharau alisema licha
ya kufanya kambi hiyo ya matibabu wamepata pia
fursa ya kujifunza mbinu mpya za kitabibu na kuongeza ufanisi wa namna
ya kufanya kazi kwa haraka katika muda mfupi hivyo kuweza kuwahudumia wagonjwa
wengi zaidi.
“Leo ni siku ya nne tangu kambi hii kuanza,
tumefanikiwa kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto 24 na tunategemea mpaka mwisho
siku ya Alhamisi ambayo ni siku ya mwisho tutakuwa tumefanya upasuaji kwa watoto zaidi ya 30”, alisema
Dkt. Sharau.
Dkt. Sharau ambaye pia ni daktari
bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto alisema baadhi ya watoto ambao wamefanyiwa
upasuaji ni wale waliozaliwa na matundu katika moyo, watoto ambao valvu zao hazijajitengeneza
vizuri na wengine ambao mishipa yao ya damu haijakaa katika mpangilio wake.
“Baada ya kuwafanyia upasuaji huu watoto
wengi wataweza kupona kabisa na kuendelea na maisha kama watoto wengine lakini
kuna wachache ambao upasuaji huu ni hatua katika hatua kadhaa za upasuaji ambazo
zinahitajika ili waweze kupona”, alisema Dkt. Sharau.
Akizungumza kuhusu vifaa hivyo Dkt. Sharau
alishukuru kwa msaada huo na kusema kwamba vimesaidia watoto wengi kufanyiwa
upasuaji kwani vifaa vipo vya kutosha.
“Wenzetu hawa kutoka Kituo cha Mfalme
Salman cha Misaada ya Kibinadamu cha nchini Saudi Arabia wamekuwa wakija hapa
nchini mara kwa mara na kutoa huduma ya matibabu ya moyo kwa watoto na kusaidia vifaa
vya matibabu hayo”, alisema Dkt. Sharau.
Kwa upande wake daktari bingwa wa moyo
na mishipa ya damu kutoka Kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya Kibinadamu Abdulrahman
Redhyan alisema kambi hiyo imekuwa ikidhaminiwa na Mfalme Salman wa nchini Saudi
Arabia kuwawezesha watoto kupata matibabu na kubadilishana uzoefu na wataalamu wa
afya wa JKCI.
Dkt. Abdulrahman alisema jumla ya timu
ya watu 26 kutoka nchini Saud Arabia ambao ni wataalamu wa usingizi, waendesha
mashine za moyo, wauguzi na madaktari wameshiriki katika kambi hii ili kuhakikisha
watoto wengi wanafanyiwa upasuaji wa moyo kwa kipindi cha muda mfupi.
“Tunaamini yakuwa kuna watoto wengi
wenye uhitaji wa huduma hizi za upasuaji wa moyo ndio maana tumekuwa tukija kwa
wingi ili kwapamoja tuweze kuwasaidia watoto wetu kupata matibabu kwa haraka na
kuwapunguzia maumivu ya ugonjwa”, alisema Dkt Abdulrahman.
Naye mzazi ambaye mtoto wake
amefanyiwa upasuaji katika kambi hiyo Mwamini Sabimana Rebeka kutoka nchini
Kongo alisema mtoto wake amekuwa akisumbuliwa na magonjwa ya moyo tangu
alipomzaa na kumpeleka katika Hospitali mbalimbali bila ya mafanikio.
“Sikugundua mapema kama mtoto wangu
alikuwa na shida ya moyo, hadi mwaka huu akiwa na miaka nane ndio nligundulika
kuwa na tatizo la moyo la kuzaliwa nalo”, alisema Mwamini.
Mwamini alisema mtoto wake alikuwa na
dalili mbalimbali ikiwemo kushindwa kupumua vizuri, kupata homa za mara kwa
mara, kuwa mdhoofu, kuvimba mwili lakini
dalili zote hizo hospitali nilizokwenda zilishindwa kutambua tatizo alilokuwa
nalo.
“Baada ya kukosa matibabu nchini Kongo
alikwenda nchinii Rwanda na baadaye kupata taarifa kuhusu Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) hivyo kufika hapa na kupatiwa matibabu kwa wakati”,.
“Namshukuru Mungu mara baada ya mtoto
wangu kupatiwa matibabu anaendelea vizuri sio kama mwanzo, nawashukuru wataalamu
wa afya wa JKCI kwa huduma zao nzuri sana, wananchi wenzangu kutoka Kongo
nawashauri mtakapopata matatizo ya moyo mfike hapa JKCI kwani huduma za
matibabu zipo na nzuri”, alisema Mwamini.
Comments
Post a Comment