Watu 335 wapimwa moyo Dar
Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Husna Faraji akitoa elimu ya jinsi ya kuepukana na magonjwa yasiyo ya kuambukiza yakiwemo ya moyo kwa kufuata mtindo bora wa maisha kwa wananchi waliofika katika kambi maalumu ya siku mbili ya matibabu ya moyo iliyomalizika jana JKCI Hospitali ya Dar Group.
Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Dkt. Tulizo Shemu akizungumza na Nadim Durrani kutoka kampuni ya uuzaji na usambazaji wa dawa za binadamu ya MORAF wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya moyo liliyomalizika jana katika Hospitali hiyo. Katika upimaji huo kampuni hiyo ilishirikiana na JKCI kwa kutoa dawa za mifupa kwa wananchi waliokutwa na shida.
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Ibrahim Amir akimpima uzito na urefu mwananchi aliyefika katika Hospitali hiyo kwaajili ya kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kambi maalumu ya matibabu iliyomalizika jana jijini Dar es Salaam.
Watafiti wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) makao makuu na Hospitali ya Dar Group wakichukuwa taarifa za wananchi waliofika katika Hospitali ya Dar Group kwaajili ya kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kambi maalumu ya matibabu iliyomalizika jana.
Mtaalamu wa Maabara wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Jane Mathew akimpima kiwango cha sukari kwenye damu mtoto aliyefika katika Hospitali hiyo kwaajili ya kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kambi maalumu ya matibabu iliyomalizika jana jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Flaviana Masegesa na Afisa Masoko wa Hospitali hiyo Ireen Mbonde wakichukuwa taarifa mbalimbali wakati wa zoezi la uchunguzi na matibabu ya moyo lililomalizika jana katika Hospitali hiyo.
Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Janeth Mmari na Husna Faraji wakitoa ushauri wa jinsi ya kuepukana na magonjwa ya moyo, matumizi sahihi ya dawa za moyo na lishe bora kwa wananchi waliofika JKCI Hospitali ya Dar Group kwaajili ya kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kambi maalumu ya matibabu iliyomalizika jana jijini Dar es Salaam.
Watu 335 wamepata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo kwenye kambi maalumu ya matibabu ya siku mbili iliyomalizika jana katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group.
Kaimu Mkurugenzi wa hospitali hiyo Dkt.Tulizo Shemu alisema matibabu
hayo ya tiba mkoba yajulikanayo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan
Outreach Services yalifanyika maalumu kwaajili ya kusogeza huduma za kibingwa za
matibabu ya moyo kwa wananchi wa mkoa wa Dar es Salaam na mikoa ya jirani.
Dkt. Shemu ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo alisema
katika kambi hiyo watu waliowaona walitoka ndani na nje ya mkoa wa Dar es
Salaam na wengi wao walikuwa na tatizo la shinikizo la juu la damu pamoja na
matatizo mengine ya moyo.
“Nusu ya watu tuliowaona walikuwa na tatizo la shinikizo la
juu la damu na wengine walikuwa na matatizo ya kutanuka kwa moyo, mishipa ya
damu ya moyo kuziba, mafuta mengi kwenye mishipa ya damu, maumivu ya kifua, shida
za valvu, shida ya mfumo wa umeme wa moyo pia tumewaona watoto waliokuwa na
matatizo ya matundu kwenye moyo na mishipa ya damu ya moyo kutokukaa kwenye
mpangilio wake”,.
“Tuliowakuta na shida za moyo na wengine waliokuwa na shida
mbalimbali za mwili kama vile masikio, mifupa, ngozi, macho tumewapeleka katika
kliniki zetu kwaajili ya matibabu kwani katika hospitali hii licha ya kutibu
moyo tunatibu pia magonjwa mengine pia wengine tumewapa rufaa ya kwenda
kutibiwa katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH)”, alisema Dkt. Shemu.
Dkt. Shemu alisema kambi za aina hiyo zitakuwa zinafanyika
mara kwa mara katika Hospitali hiyo kwani kwa kufanya hivyo wananchi wengi wa
mkoa wa Dar es Salaam na mikoa jirani watafikiwa na huduma za kibingwa za matibabu
ya moyo.
Kwa upande wao wananchi waliopata matibabu katika kambi hiyo
waliishukuru Serikali kwa huduma waliyoipata na kuomba iwe endelevu ili watu
wengi zaidi waweze kufikiwa na huduma za kibingwa za matibabu ya moyo.
Tatu Hassan mkazi wa Shinganya alisema aliona katika TV tangazo
la kufanyika kwa matibabu hayo na kuchukuwa hatua ya kwenda kufanyiwa uchunguzi
na matibabu ya moyo.
“Ninaishukuru Serikali kwa kutuangalia wananchi wanyonge wenye
kipato cha chini na kutufikishia huduma hii ya matibabu ya kibingwa. Nimefika
hapa nimefanyiwa vipimo, nimepewa ushauri na dawa za kwenda kutumia mwezi mmoja
kwani mimi ninatatizo la shinikizo la juu la damu ambalo limepelekea moyo wangu
kutanuka”, alisema Tatu.
“Ninatoa wito kwa wananchi wenzangu wanapoona matangazo ya
upimaji wa magonjwa mbalimbali wasipuuze wawahi hospitali mapema kwa ajili ya kufanyiwa
uchunguzi na kupata matibabu mapema kuliko kusubiri hadi waumwe ndipo waende
kutibiwa”, alisema Richard John mkazi wa Tegeta.
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imekuwa ikitoa huduma ya tiba mkoba ya kuwafuata wananchi mahali walipo kwa kufanya uchunguzi na matibabu ya moyo katika maeneo mbalimbali hapa nchini. Hadi sasa wameshatoa huduma hiyo katika mikoa 12 na kuona watu 7196 ambapo 847 walikutwa na matatizo ya moyo yaliyohitaji matibabu ya kibingwa na kupewa rufaa ya kwenda kutibiwa katika Taasisi hiyo.
Comments
Post a Comment