Wasemavyo wakazi wa Geita huduma za matibabu ya moyo
Wananchi wa Mkoa wa Geita wameishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) kwa kufikisha huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya
moyo kwa wananchi hao bila gharama.
Shukrani hizo zimetolewa na wananchi mbalimbali waliotembelea
banda la JKCI lililopo katika maonesho ya sita ya kitaifa ya Teknolojia ya
madini yanayoendelea katika viwanja vya EPZA Bombambili mkoani Geita.
Akizungumza na mwandishi wa habari hii Donard Francis alisema
Taasisi ya JKCI imeonyesha kuwajali watanzania ambao hawakuwa na matarajio ya
kuchunguza mioyo yao kutokana na mazingira waliyopo hivyo kuwaomba kuendelea
kushiriki katika matukio mbalimbali yatakayowapa nafasi wananchi kujua afya ya
mioyo yao.
“Leo kwa mara ya kwanza nimepima moyo wangu, nimepima sukari
kwenye damu na shinikizo la damu, kwakweli sikujua kama kuna umuhimu wa
kuchunguza magonjwa haya hapo awali lakini kupitia Taasisi hii nimepata elimu
ambayo nitawaelimisha na wenzangu umuhimu wa kuchunguza afya zao”, alisema
Donard
Kwa upande wake Sada Hassan mkazi wa Geita aliyepatiwa huduma
katika banda la JKCI alisema kuwa yeye ni mjamzito anayetarajia kujifungua
wakati wowote wiki hii lakini tangu alipobeba ujauzito huo hakuwahi kupima
shinikizo la damu hadi wiki hii ya mwisho alipoenda Hospitali ya Rufaa ya Mkoa
wa Geita na kupimwa shinikizo la damu ambapo majibu yake hayakuwa mazuri.
“Nimetoka kijiji cha Nyang’wale ambapo nimekuwa nikienda
kliniki lakini sikuwahi kupimwa shinikizo la damu, leo nimefika katika banda la
JKCI nimepimwa shinikizo la damu na kuanzishiwa dawa ili niweze kutoka katika
hatari ya kupata madhara wakati wa kujifungua maana shinikizo langu la damu
lipo juu”, alisema Sada
Sada alisema amefurahia huduma alizopata katika banda la JKCI
kwani hata mtoto wake aliyopo tumboni ameweza kufanyiwa uchunguzi wa moyo wake
na kuonyesha kuwa yupo salama.
“Wanawake wenzangu ambao wana ujauzito wafike katika banda la
JKCI kuchunguza kama afya zao zipo sawa kuondokana na athari zinazoweza
kujitokeza kipindi cha ujauzito na wakati wa kujifungua kama wataalamu wa afya
wanavyoelimisha”, alisema Sada
Akitoa wito kwa Taasisi nyingine zinazotoa huduma za afya
Victor Maduhu ameziomba Taasisi za afya kuwafuata wananchi walipo kama ambavyo
JKCI imefanya ili wananchi wapate huduma za afya kiurahisi kwani watu wengi
wanahitaji huduma za kibingwa lakini kutokana na hali zao kiuchumi wanakosa
fursa ya kupata huduma hizo.
Victor alisema Serikali imewekeza vizuri katika sekta ya afya
ambapo sasa hivi hakuna haja ya mtu kufuata huduma za kibingwa nje ya nchi
kwani huduma zote za kibingwa zinapatikana hapa Tanzania.
“Naipongeza sana Serikali yangu kuwekeza katika huduma za
afya, ila nawaomba wataalamu wa afya kutoka Taasisi za kibingwa kuiga mfano wa
JKCI kutufikia kwani sisi wananchi wenye uchumi wa chini tunawahitaji sana ili tupate
huduma kwa karibu na kirahisi bila ya kuhangaika”, alisema Victor
Comments
Post a Comment