Bulembo aipongeza JKCI kupeleka vipimo waliko wananchi



 Mkuu wa Wilaya ya  Kigamboni Mhe. Halima Bulembo akimsalimia mwananchi aliyefika katika Hospitali ya Wilaya hiyo kwaajili ya kupata huduma ya uchunguzi na matibabu ya moyo zinazotolewa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Kigamboni. Kulia ni Mkurugenzi wa Hospitali ya JKCI Dar Group Dkt. Tulizo Shemu.

Mkuu wa Wilaya ya  Kigamboni Mhe. Halima Bulembo akiwasili katika viwanja vya Hospitali ya wilaya hiyo kwaajili ya kuangalia huduma za upimaji na matibabu ya moyo zinatolewa na wataalamu ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali hiyo. Kulia kwa Mkuu wa Wilaya ni Mkurugenzi wa Hospitali ya JKCI Dar Group Dkt. Tulizo Shemu.

Mkuu wa Wilaya ya  Kigamboni Mhe. Halima Bulembo akipata maelezo kutoka kwa Mkurugenzi wa Hospitali ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dar Group Dkt. Tulizo Shemu kuhusu kambi maalumu ya upimaji na matiababu ya moyo inayofanywa na wataamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Wilaya Kigamboni.

Mtafiti wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Maclina Komba akimpima uwiano baina ya urefu na uzito Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni Halima Bulembo aliyefika katika Hospitali ya wilaya hiyo kwaajili ya kuangalia huduma za upimaji na matibabu ya moyo zinatolewa katika Hospitali hiyo. Wataalamu wa JKCI na wenzao wa Kigamboni wanafanya kambi maalumu ya siku tano ya upimaji na matibabu ya moyo kwa wananchi wa wilaya hiyo.
************************************************************************************************************************************************************************************************************

 Mkuu wa Wilaya ya Kigamboni Mhe. Halima Bulembo ameipongeza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kuwafuata wananchi wa Wilaya hiyo na kuwapatia huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo.

Pongezi hizo amezitoa jana alipotembelea kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya moyo inayofanyika katika Hospitali ya Wilaya ya Kigamboni.

Kambi hiyo ya siku tano inafanywa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya wilaya Kigamboni.

Mhe. Halima alisema wataalamu wa JKCI wamekuwa wakijitoa kuhakikisha huduma za matibabu ya moyo zinawafikia wananchi mahali walipo kama ambavyo wamefanya kuwafikia wananchi wa Kigamboni.

“Tunawapongeza sana kwa kujitoa kwenu, tunaamini huduma mnazozitoa sio kazi rahisi lakini mmendelea kuhakikisha wananchi wanafikiwa na huduma za kibingwa”, alisema Mhe. Halima.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Hospitali ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Dkt. Tulizo Shemu alisema JKCI imekuwa ikizunguka maeneo mbalimbali nchini kuangalia ukubwa wa matatizo ya magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo yanayogharimu maisha ya watu wengi na kupunguza nguvu kazi ya watanzania.

Dkt. Shemu alisema kupitia huduma ya tiba mkoba ijulikanayo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services JKCI inazingatia utoaji wa huduma za upimaji wa magonjwa ya moyo kwa kuwafuata wananchi mahali walipo kutoa huduma za kibobezi za uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo pamoja na elimu ya namna ya kujikinga na magonjwa hayo.

“Tumekuwa tukishirikiana na makampuni mbalimbali yanayosambaza dawa za binadamu katika kambi tunazofanya ili tunapopata wagonjwa katika maeneo tunayotembelea tuweze kuwapatia dawa bila gharama”, alisema Dkt. Shemu.

Dkt. Shemu alisema hadi sasa katika kambi hiyo wameshatoa huduma kwa wananchi zaidi ya 150 ambapo baadhi yao wamekutwa na magonjwa yasiyoambukiza na wengine wameshapewa rufaa kufika JKCI kwaajili ya uchunguzi zaidi na matibabu ya magonjwa ya moyo.

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari