Wakuu wa Vitengo wa JKCI wapewa mafunzo ya kufanya kazi kimkakati na kufikia malengo waliyojiwekea

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na wakuu wa vitengo kutoka JKCI wakati wa kufunga mafunzo ya siku mbili yaliyotolewa kwa viongozi hao na Taasisi ya Uongozi katika ukumbi wa Hoteli ya Giraffe iliyopo jijini Dar es Salaam


Mwezeshaji kutoka Taasisi ya Uongozi Paul Bilabaye akiwafundisha wakuu wa vitengo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) namna ya kutambua viashiria vya hatari eneo la kazi wakati wa mafunzo ya siku mbili kwa viongozi hao yaliyotolewa na Taasisi ya Uongozi na kumalizika jana katika Hoteli ya Giraffe iliyopo jijini Dar es Salaam


Mkuu wa kitengo cha Rasilimali watu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Abdulrahman Muya akitoa neno la shukrani wakati wa kuhitimisha mafunzo ya siku mbili kwa viongozi wa Taasisi hiyo yaliyotolewa na Taasisi ya Uongozi na kumalizika jana katika Hoteli ya Giraffe iliyopo jijini Dar es Salaam



Baadhi ya wakuu wa vitengo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakifanya mafunzo kwa vitengo ya kuonyesha ushirikiano wakati wa mafunzo kwa viongozi hao yaliyotolewa na Taasisi ya Uongozi katika Hoteli ya Giraffe iliyopo jijini Dar es Salaam.

Na: JKCI

*******************************************************************************************************

Wakuu wa Vitengo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kutumia ujuzi walioupata kupitia mafunzo ya uongozi kufikia dira na malengo ya Taasisi hiyo kuiwezesha Taasisi kuwa kituo cha umahiri cha utalii tiba katika kutoa matibabu ya moyo Barani Afrika.

Rai hiyo imetolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati akifunga mafunzo ya siku mbili kwa viongozi hao yaliyotolewa na Taasisi ya Uongozi na kufanyika katika Hoteli ya Giraffe iliyopo jijini Dar es Salaam.

Dkt. Kisenge alisema mafunzo hayo yaendelee kuandaliwa mara kwa mara lengo likiwa kuwakumbusha viongozi kuchukua majukumu yao, kuwa na mahusiano mazuri na wafanyakazi wanaowaongoza ili kwapamoja waweze kufikia malengo ya Taasisi.

“Ninaimani kubwa mkitoka hapa mtaenda kuyafanyia kazi yale yote mliyofundishwa kwa siku mbili ambayo yakifuatwa kama mlivyojifunza mabadiliko makubwa yataenda kutokea katika vitengo vyenu”, alisema Dkt. Kisenge

Dkt. Kisenge alisema mafunzo hayo yametoa fursa kwa wakuu wa  vitengo wa JKCI kujifunza namna bora ya kuongoza, umuhimu wa mawasiliano pamoja na usimamizi wa rasilimali za umma.

“Kama viongozi mnatakiwa kuwa na ujuzi ambazo utasaidia kuwaongoza watu walio chini yanu ili kwa pamoja muweze kufikia malengo ambayo yatawasadia wakati wa kuandaa mpango mkakati katika vitengo vyenu.

Aidha Dkt. Kisenge aliwashukuru wawezeshaji kutoka Taasisi ya Uongozi kwakuwa karibu na JKCI kwani wanapowahitaji kwaajili ya kutoa mafunzo kwa wafanyakazi wa JKCI wamekuwa mstari wa mbele kutoa huduma na kuleta mabadiliko katika utendaji wa kazi.

Kwa upande wake mwezeshaji kutoka Taasisi ya Uongozi Fortune Ekklesiah alisema mafunzo kwa viongozi husaidia kuwaonyesha umuhimu wa kufanya kazi kwa pamoja na watu wanaowaongoza ili kuleta tija katika utendaji wa kazi.

Fortune alisema viongozi wanatakiwa kuwa na uwezo wa kutambua, kutafuta ufumbuzi, kushirikisha na kufanyia kazi yale yote yanayohusiana na idara/vitengo vyao bila ya kuingilia idara/vitengo vingine.

“Katika mafunzo haya tumefanya baadhi ya mafunzo kwa vitendo lengo likiwa kuona ushirikiano unavyojengwa katika kutafuta ushindi lakini pia kuangalia kiongozi anachukua majukumu gani kuhakikisha kundi lake linafikia malengo yaliyokusudiwa”, alisema Fortune

Akielezea mafunzo hayo Mkuu wa kitengo cha Rasilimali watu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Abdulrahman Muya alisema mafunzo hayo kwa viongozi yamefanyika kutekeleza mpango mkakati wa utekelezaji wa majukumu kwa mwaka wa fedha 2023/2024.

Muya alisema mada zilizotolewa katika mafunzo hayo ni pamoja na Uongozi, kujitambua, akili hisia, mawasiliano ya kimkakati, kutunza mali za umma katika sehemu za kazi, namna ya kutambua viashiria vya hatari eneo la kazi, na namna ya kutengeneza mikakati ya kukabiliana na viashiria vya hatari endapo vitatokea.

“Tunaamini viongozi hawa wanaenda kuwa mabalozi wa kufanya mabadiliko katika maeneo yao ya kazi na kuwa timilifu katika uongozi ili waweze kusaidia katika utekelezaji wa majukumu ya Taasisi”, alisema Muya

Naye mshiriki wa mafunzo hayo ambaye ni Mkuu wa wauguzi Hospitali ya JKCI Dar Group Magreth Mbaruku aliushukuru uongozi wa Taasisi hiyo kwakutoa nafasi kwa wakuu wa vitengo kupata mafunzo hayo yaliyoweza kuwakumbusha wajibu wao kama viongozi.

“kupitia mafunzo haya nimejua mimi kama kiongozi natakiwa kujitambua na baadaye kuwatambua watu ninaowaongoza kwasababu kila mtu ametoka katika mazingira tofauti hivyo kama hatutatambuana vizuri tunaweza kukwamisha kazi kutokufanyika kutokana na matendo ya mtu au watu tunaowaongoza”, alisema Magreth

Magreth alisema mafunzo hayo yataenda kumsaidia katika majukumu yake ya kila siku kufikia malengo ya kitengo anachokiongoza kwa kushirikiana na wenzake na kujenga mahusinao mazuri.




Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari