JKCI: Kigamboni njooni kupima moyo

Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Samwel George na mwenzake wa Hospitali ya wilaya Kigamboni Ally Kumbuka wakimsikiliza mwananchi aliyefika katika hospitali ya Kigamboni kwaajili ya kupata huduma za upimaji na matibabu ya moyo. Wataalamu wa JKCI na wenzao wa Kigamboni wanafanya kambi maalumu ya matibabu ya moyo ya siku tano kwa wananchi wa wilaya hiyo.

Mtafiti wa Taasisi ya Moyo jakaya Kikwete (JKCI) Saad Kamtoi akichukuwa taarifa za mwananchi aliyefika katika Hospitali ya wilaya Kigamboni kwaajili ya kupata huduma za upimaji na matibabu ya moyo.Wataalamu wa JKCI na wenzao wa Kigamboni wanafanya kambi maalumu ya matibabu ya moyo ya siku tano kwa wananchi wa wilaya hiyo.

  

Mwakilishi wa kampuni ya uingizaji na usambazaji wa dawa za binadamu ya Micro Labs Ltd Festus Asenga akimpatia dawa za kupunguza mafuta mwilini mwananchi aliyefika katika Hospitali ya wilaya Kigamboni kwaajili ya kupata huduma za upimaji na matibabu ya moyo. Kampuni ya uingizaji na usambazaji wa dawa za binadamu ya Micro Labs Ltd inatoa dawa bila malipo kwa wananchi wanaokutwa na matatizo ya moyo katika kambi hiyo inayofanywa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Kigamboni.


Afisa Uuguzi wa Hospitali ya Wilaya Kigamboni Evodia Mduda akimpima kiwango cha sukari kwenye damu mtoto  aliyefika katika Hospitali hiyo  kwaajili ya kupata huduma za upimaji na matibabu ya moyo wakati wa kambi maalumu ya matibabu inayofanywa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Kigamboni.

**********************************************************************************************************************************************************************************************************

Wakazi wa wilaya ya Kigamboni na maeneo ya jirani wametakiwa kujitokeza kwa wingi katika Hospitali ya Wilaya hiyo iliyopo Gezaulole kwaajili ya kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo.

Matibabu hayo yanatolewa katika kambi maalumu ya matibabu ya moyo ya siku tano inayofanywa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya wilaya Kigamboni.

Rai hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na  Mawasiliano wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Anna Nkinda wakati akizungumza na waandishi wa habari walioshiriki zoezi hilo la upimaji.

Anna alisema katika kambi hiyo wananchi wanapimwa vipimo mbalimbali vya moyo vikiwemo vya kuangalia uwiano baina ya urefu na uzito, uwingi wa sukari kwenye damu, shinikizo la damu, kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography - ECHO) na mfumo wa umeme wa moyo (Electrocardiography - ECG).

“Ninawaomba wananchi mje kupima afya zenu katika Hospitali hii ya Kigamboni tutakuwepo hapa hadi siku ya Ijumaa. Wataalamu wetu wanafanya upimaji wa magonjwa ya moyo, wanatoa huduma ya matibabu pamoja na ushauri wa matumizi sahihi ya dawa za moyo na jinsi ya kuepukana na magonjwa hayo”,.

 “Watu ambao tunawakuta na matatizo ya moyo yanayohitaji uchunguzi wa kitaalamu na matibabu zaidi tunawapa rufaa ya kuja JKCI kwaajili ya kufanyiwa uchunguzi  pamoja na kuwapa matibabu ya kibingwa”, alisema Anna.

Anna alisema huduma hiyo ya tiba mkoba ya kuwafuata wananchi mahali walipo inajulikana kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services ambapo wananchi wanapata huduma za kibingwa za uchunguzi, ushauri na matibabu ya moyo.

Kwa upande wake Mratibu wa Huduma za Kitabibu Manispaa ya Kigamboni Dkt. Chemere Sirira aliishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kuwatuma wataalamu wake katika hospitali hiyo ambao wanashirikiana kwa pamoja kutoa huduma kwa wananchi.

“Huduma za kumuona daktarin na vipimo vya moyo vikiwemo za ECHO na ECG zinatolewa bila malipo yoyote yale, wananchi wanalipia huduma ya vipimo vya maabara pia kuna dawa ambazo zinatolewa bila malipo na kuna dawa ambazo wananchi wanazilipia  kwa gharama naafuu”,.

“Pamoja na wananchi kupata huduma ya matibabu ya kibingwa ya moyo  wataalamu wetu wa afya wa Hospitali hii wanajengewa uwezo wa kufanya vipimo na kutibu wagonjwa wa moyo hii itatusaidia baada ya kambi hii nasi tutaweza kutoa huduma hii kwa wagonjwa wetu”, alisema Dkt. Sirira.

Nao wananchi waliopata matibabu katika kambi hiyo ya matibabu ya moyo waliishukuru Serikali kwa huduma waliyoipata na kusema kuwa imewasaidia kupata matibabu kwa haraka na kirahisi zaidi.

“Wananchi wengi wa vijijini tunachangamoto ya kupata huduma za matibabu za kibingwa, tunashukuru huduma hii imetufuata hapa Kigamboni, nimetibiwa, nimepata dawa pamoja na ushauri. Ninawaomba wananchi wenzangu mje kupima moyo kwani wataamu wapo hapa na wanatoa huduma za matibabu”, alisema Rajabu Salumu mkazi wa Tungi Kigamboni.

“Nilisikia taarifa ya kuwepo kwa  kambi hii ya upimaji wa moyo kwenye vyombo vya habari nami nikaamua kuja na mwanangu kupima, nimepata huduma nzuri na kwa haraka ninaiomba Serikali ituletee huduma nyingine za kibingwa zikiwemo za macho pia wananchi wenzangu mtumie nafasi hii mje kupima moyo”, alisema Mwajuma Ponza mkazi wa Chanika wilayani Ilala.


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari