Dkt. Kisenge: Jazeni PEPMIS kwa wakati
Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete (JKCI) Ghati Chacha akiwasisitiza wafanyakazi wa taasisi hiyo kujaza
taarifa zao za ya kazi za kila wiki katika mfumo wa PEPMIS wakati wa kikao cha
wafanyakazi kilichofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi
hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Kaimu Mkuu wa Hospitali ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
hospitali ya Dar Group Dkt. Tulizo Shemu akichangia mada wakati wa kikao cha
wafanyakazi wa JKCI kilichofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa
Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa Fedha na Mipango wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) CPA Agnes Kuhenga akifafanua jambo wakati wa kikao cha
wafanyakazi wa JKCI kilichofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa
Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
wametakiwa kujaza taarifa zao za kazi wanazozifanya kila siku katika mfumo wa kupima
utendaji kazi wa watumishi wa umma (PEPMIS) ili kuiwezesha Serikali kufuatilia
taarifa za watumishi katika mfumo huo.
Rai hiyo imetolewa hivi karibuni na Mkurugenzi Mtendaji wa
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati wa kikao cha wafanyakazi
kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es
Salaam.
Dkt. Kisenge alisema Serikali imeweka mfumo wa PEPMIS ili kurahisisha
upatikanaji wa taarifa za mtumishi wa umma hivyo kama watautumia vizuri mfumo
huo utawawezesha kupata manufaa mazuri ikiwemo kupanda vyeo.
“Ninawaomba viongozi katika maeneo yenu muwasimamie wafanyakazi wajaze PEPMIS kwa wakati na wale wanaopitia changamoto wafike katika ofisi ya Utawala na Rasilimaliwatu ili waweze kutatua changamoto wanazopitia ili wote kwa pamoja tuwe katika mstari unaotakiwa”, alisema Dkt. Kisenge Aidha Dkt. Kisenge aliwahimiza wafanyakazi hao kufanya kazi kwa pamoja, kwa weledi, kujituma na kutolalamika pia wawahudumie wagonjwa vizuri na kuwa wakarimu kwao kwa kufanya hivyo kila mfanyakazi ataona mafanikio yake kwani idadi ya wagonjwa itaongezeka na hivyo kutimiza malengo ya Taasisi hiyo.
“Kutokana na huduma nzuri inayotolewa kwa wagonjwa wetu idadi ya wagonjwa binafsi wanaotibiwa JKCI
imeongezeka na kufikia asilimia 23 ya wagonjwa wote jambo ambalo linaonyesha
umahiri wa taasisi katika kutoa huduma bora”.
“Idadi ya wagonjwa tunaowahudumia katika kliniki yetu maalumu
ya VIP imeongezeka kutoa wagonjwa 34 na
kufikia 400 hadi 500 kwa mwezi ”, alisema Dkt. Kisenge”.
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali watu
Ghati Chacha aliwasihi wafanyakazi wa
Taasisi hiyo kuwahi kazini na kufuata taratibu na kanuni za utumishi wa Umma.
Ghati aliwakumbusha wafanyakazi hao kuvaa vitambulisho vyao
vya kazi muda wote wanapokuwa eneo la kazi kwa kufanya hivyo kunawasaidia
wagonjwa na wasio wagonjwa kuwatambua watu wanaowahudumia.
Akizungumza kwa niaba ya wafanyakazi wa taasisi hiyo daktari
bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto Godwin Sharau aliushukuru uongozi wa JKCI
kwa kujali maslahi ya wafanyakazi kitu ambacho kimeongeza hamasa ya ufanyaji
kazi.
“Tunajivunia kufanya kazi JKCI na kuwahudumia wagonjwa wa
moyo tutaendelea kufanya kazi kwa weledi mkubwa kwa manufaa ya vizazi vilivyopo
na vijavyo ili huduma hii tunayoitoa ifike katika maeneo mengi nchini”, alisema
Dkt. Godwin.
Comments
Post a Comment