JKCI yaandaa mpango mkakati wa kwanza wa Utalii Tiba

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akipokea mpango mkakati wa kwanza wa utalii tiba ulioandaliwa na kamati ya utalii tiba ya Taasisi hiyo kwaajili ya kuwaongoza kufikia malengo yaliyopangwa na Taasisi hiyo katika kutoa huduma za matibabu ya moyo kimataifa.


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na baadhi ya wanakamati wa utalii tiba wa Taasisi hiyo mara baada ya kupokea mpango mkakati wa kwanza wa utalii tiba unaolenga kufikisha huduma za moyo kimataifa.

Na JKCI

********************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imeandaa mpango mkakati wake wa kwanza wa utalii tiba, hatua inayolenga kuiweka Tanzania kwenye ramani ya utoaji wa huduma za afya bora kimataifa na kuvutia wagonjwa kutoka ndani na nje ya nchi.

Mpango huo uliwasilishwa rasmi na Kamati ya Utalii Tiba ya taasisi hiyo na kukabidhiwa kwa Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Dkt. Peter Kisenge ambaye alisema mpango huo utakuwa dira ya utekelezaji wa malengo ya taasisi katika kukuza huduma za moyo kwa ubora wa juu unaokubalika kimataifa.

“Kupitia mpango huu tunataka kuhakikisha wagonjwa wa ndani na nje ya nchi wanapata huduma za kitaalamu na zenye viwango vya kimataifa. Ni mkakati utakaosaidia sio tu kuimarisha afya ya wananchi bali pia kuchangia pato la taifa kupitia utalii tiba,” alisema Dkt. Kisenge.

Aliongeza kuwa mpango huo umejikita katika maeneo kadhaa ikiwemo kuimarisha miundombinu ya kisasa ya tiba, kuongeza rasilimali watu wenye ujuzi wa kitaalamu, kuimarisha tafiti za kitabibu, kuboresha mazingira rafiki ya hospitali pamoja na kuongeza ushirikiano wa kimataifa na taasisi kubwa za afya.

Kwa mujibu wa Dkt. Kisenge, Tanzania ina nafasi kubwa ya kunufaika na utalii tiba kutokana na ongezeko la mahitaji ya huduma za moyo barani Afrika na gharama nafuu zinazotolewa na JKCI ukilinganisha na nchi nyingine.

“Tunataka mtu anayehitaji matibabu ya moyo Afrika Mashariki na Kati asifikirie kusafiri mbali bali afikirie kuja Tanzania, hususan JKCI, ambako atapata huduma bora na kwa gharama nafuu zaidi,” aliongeza.

Kwa upande wao wajumbe wa Kamati ya Utalii Tiba walisema maandalizi ya mpango huu yametokana na utafiti wa kina na mashauriano na wadau wa sekta ya afya na utalii, ili kuhakikisha Tanzania inanufaika ipasavyo na fursa hii.

Mpango huu unatarajiwa pia kuchochea ajira, kuongeza mapato ya kigeni na kukuza sekta ya utalii kwa ujumla, kwani wagonjwa kutoka nje ya nchi na familia zao watakapofika nchini kupata huduma za tiba, pia watachangia katika sekta nyingine kama hoteli, usafiri na biashara.

JKCI kwa sasa ni kituo kikuu cha rufaa cha kitaifa cha matibabu ya magonjwa ya moyo, chenye uwezo wa kutoa huduma za upasuaji mkubwa wa moyo, upandikizaji vifaa vya moyo na matibabu mengine ya kitaalamu ambayo awali wananchi walilazimika kuyatafuta nje ya nchi.

Kwa kukamilika kwa mpango huu wa kwanza wa utalii tiba, taasisi hiyo inatarajia kuongeza zaidi idadi ya wagonjwa wa kimataifa wanaofika nchini kwa ajili ya huduma, sambamba na kuendelea kutoa huduma bora kwa Watanzania.


Comments

Popular posts from this blog

Wateja wa CRDB kutibiwa JKCI kwa punguzo la asilimia 50%

Wanawake wa JKCI SACCOS wanaongoza kwa kumiliki hisa

JKCI, MOI NA MNH waitwa Comoro kutoa huduma za matibabu ya kibingwa