Dkt. Peter Kisenge aongoza wataalamu wa JKCI kutibu magonjwa ya moyo Kisiwani Anjouan
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimpima mapigo ya moyo mkazi wa kisiwa cha Anjouan aliyefika katika hospitali ya Hombo kwaajili ya kupata huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa kwa wananchi. Serikali ya Tanzania imetuma timu ya madaktari bingwa wa magonjwa mbalimbali kwaajili ya kutoa huduma za matibabu kwa wananchi wa kisiwa hicho.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimpima kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi mkazi wa kisiwa cha Anjouan aliyefika katika hospitali ya Hombo kwaajili ya kupata huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa kwa wananchi. Serikali ya Tanzania imetuma timu ya madaktari bingwa wa magonjwa mbalimbali kwaajili ya kutoa huduma za matibabu kwa wananchi wa kisiwa hicho.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimsikiliza mkazi wa kisiwa cha Anjouan aliyefika katika hospitali ya Hombo kwaajili ya kupata huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa kwa wananchi wa kisiwa hicho. Kulia ni Daktari wa taasisi hiyo Janeth Mmari.
Wakazi wa kisiwa cha Anjouan wakisubiri kupata huduma za matibabu ya moyo zinazotolewa na wataalamu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) katika katika kambi maalumu ya matibabu ya madaktari bingwa wa magonjwa mbalimbali kutoka Tanzania ambapo JKCI inatoa huduma katika hospitali ya Hombo.
***************************************************************************************************************************************************************************************************************
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge anaongoza jopo la wataalamu wa moyo kutoka Tanzania kwaajili ya kutoa huduma za kibingwa za matibabu ya moyo katika Hospitali ya Hombo iliyopo kisiwa cha Anjouan nchini Comoro.
Akizungumza kuhusu kambi hiyo leo kisiwani Anjouan Dkt. Kisenge alisema
dhamira ya JKCI ni kuhakikisha wananchi wa Anjouan wanapata huduma bora za moyo
kwa gharama nafuu na kwa wakati bila kulazimika kusafiri umbali mrefu kufuata
matibabu hayo.
Dkt. Kisenge ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Utalii Tiba
Taifa na daktari bingwa wa moyo alisema kwa siku ya kwanza ambayo ni leo wameanza
kambi hiyo huku mwitikio wa wananchi ukiwa ni mkubwa.
“Siku ya kwanza ya leo tumeona wagonjwa 99 watoto wakiwa 39 na
watu wazima 60 wagonjwa waliopewa rufaa ya kuja kutibiwa JKCI ni 20. Asilimia
80 ya wagonjwa tuliowaona wanamatatizo ya misuli ya moyo kutanuka”.
“Tumekuja na timu kamili ya
madaktari bingwa na wataalamu wa vipimo vya moyo. Tutaendelea kushirikiana na
Serikali ya Comoro kuboresha huduma za moyo kwa wananchi, hasa katika maeneo
yenye uhitaji mkubwa”, alisema Dkt. Kisenge.
Aliongeza kuwa kambi hiyo ya madaktari bingwa kutoka Tanzania itafanyika
kwa muda wa siku nane, huku
ikihusisha uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali yakiwamo ya moyo pamoja
na utoaji wa elimu ya kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza.
Dkt. Kisenge alisema
taasisi hiyo inawapokea wagonjwa wengi kutoka Visiwa vya Comoro ambapo kwa
mwezi wanawaona wagonjwa zaidi 40. Kuwepo kwa wataalamu hao kisiwani Anjouan kutawasaidia wananchi
wenye uwezo mdogo kiuchumi kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo bila
gharama yoyote ile.
Akizungumza na wagonjwa waliofika katika hospitali hiyo kupata
huduma za matibabu ya moyo Balozi wa Tanzania nchini Comoro Saidi Yakubu aliwapongeza kwa hatua
waliyoichukuwa ya kufika katika hospitali hiyo kwaajili ya kupata huduma ya matibabu
ya moyo.
“Wagonjwa ni wengi kuna
madaktari wengine wako njiani wanakuja kutoka Tanzania, nyie nyote mliopo hapa
mtapata huduma na tutahakikisha wagonjwa wote wanapata huduma ya matibabu na
dawa bila malipo yoyote yale”, alisema Mhe. Balozi Yakubi.
Baadhi ya wananchi waliopata
huduma za matibabu ya moyo katika Hospitali ya Hombo walielezea
kufurahia uwepo wa wataalamu wa JKCI, huku wakisema wamepata matibabu na
ushauri wa kitaalamu waliokuwa wakiukosa kwa muda mrefu.
“Huduma zimekuwa bora sana. Tulipokelewa vizuri na madaktari
wametupima kwa umakini. Tunashukuru Serikali ya Tanzania na madaktari wa JKCI
kwa moyo wa huruma waliotuonesha”, alisema Fatima Bounou mkazi wa Domoni.
“Siku zote tulikuwa tukitafuta huduma ya moyo
ya kitaalamu karibu nasi, lakini ilikuwa ngumu kupata, kutokana na ushirikiano
uliopo baina ya Comoro na Tanzania tumepata matibabu bora bila gharama yoyote.
Tunashukuru sana madaktari kwa kujitolea kwa moyo wote”, alisema Ahmed Ali mkazi wa Mutsamudu.
“Huduma hizi ni za kipekee. Tulipokelewa kwa
heshima na madaktari walitupa muda wao kuzungumza nasi moja kwa moja kuhusu
afya yetu ya moyo. Ni faraja kubwa kuona Tanzania kupitia JKCI inatufikishia
matibabu haya hapa nyumbani”, alisema Amina Said mkazi wa Ouani.
Kambi hiyo inatarajiwa kuwafikia maelfu ya wananchi wa Anjouan huku
JKCI ikiahidi kuendelea kutoa mafunzo ya pamoja kwa wataalamu wa afya wa Comoro
ili kuimarisha huduma endelevu za moyo.



Comments
Post a Comment