Wagonjwa 9 wenye matatizo ya mishipa mikubwa ya damu kutanuka na kupasuaji wafanyiwa upasuaji JKCI
Mkurugenzi wa Upasuaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya na Afisa Muuguzi wa Taasisi hiyo Mahawa Asenga wakimkabidhi mtaalamu wa kuendesha mashine ya kuusaidia moyo na mapafu kufanya kazi (Heart Lung Machine) kutoka Shirika la Cardio Start Internation la nchini Marekani Kim Bekker zawadi wakati wa hafla fupi ya kuhitimisha kambi maalumu ya upasuji wa moyo iliyokuwa ikifanyika katika Taasisi hiyo na kumalizika mwishoni mwa wiki. Jumla ya wagonjwa 9 wenye matatizo ya mishipa ya damu kutanuka au kuchanika wamefanyiwa upasuaji katika kambi hiyo.
Rais wa Shirika la Cardio Star International la nchini
Marekani Dkt. Miroslav Peev akimkabidhi cheti ya ushiriki wa mafunzo ya
kuhudumia wagonjwa wa dharura na mahututi Daktari kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Mercy Elinisa wakati wa hafla ya fupi ya kuhitimisha kambi
maalumu ya upasuaji wa moyo iliyokuwa ikifanyika katika Taasisi hiyo na
kumalizika mwishoni mwa wiki. Jumla ya wagonjwa 9 wenye matatizo ya mishipa ya
damu kutanuka au kuchanika wamefanyiwa upasuaji katika kambi hiyo.
Rais wa Shirika la Cardio Star International la nchini
Marekani Dkt. Miroslav Peev akimkabidhi cheti ya ushiriki wa mafunzo ya
kuhudumia wagonjwa wa dharura na mahututi Dkt. Elias Genge wakati wa hafla ya
fupi ya kuhitimisha kambi maalumu ya upasuaji wa moyo iliyokuwa ikifanyika
katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na kumalizika mwishoni mwa wiki jijini
Dar es Salaam. Jumla ya wagonjwa 9 wenye matatizo ya mishipa ya damu ya
kutanuka au kuchanika wamefanyiwa upasuaji katika kambi hiyo.
Mkurugenzi wa Upasuaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) Dkt. Angela Muhozya na Rais wa Shirika la Cardio Star International la
nchini Marekani Dkt. Miroslav Peev wakiwa katika picha ya pamoja na wataalamu
wa JKCI na wenzao wa Shirika la Cardio Star International mara baada ya kumalizika
kwa kambi maalumu ya upasuaji wa mishipa ya damu ya moyo iliyokuwa ikifanyika
JKCI na kumalizika mwishoni mwa wiki. Jumla ya wagonjwa 9 wenye matatizo ya
mishipa ya damu kutanuka au kuchanika wamefanyiwa upasuaji katika kambi hiyo.
***************************************************************************************************
Wagonjwa tisa wenye matatizo ya
mishipa mikubwa ya damu kutanuka na kupasuka wamefanyiwa upasuaji mkubwa wa kurekebisha
na kupandikiza mishipa ya damu iliyohitaji kubadilishwa.
Upasuaji huo ulikuwa ukifanywa na
wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao
kutoka Shirika la Cardiostart International la nchini Marekani umefanyika katika
kambi maalumu ya siku tano na kumalizika mwishoni mwa wiki.
Akizungumza wakati wa hafla fupi
ya kuhitimisha kambi hiyo Mkurugenzi wa Upasuaji kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya
kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya alisema mbali na kufanyika kwa upasuaji huo mkubwa, kambi hiyo
pia ililenga kutoa mafunzo ya vitendo kwa wataalamu wa afya ili kuongeza ujuzi
na kubadilishana uzoefu na wenzao kutoka Marekani.
“Huu ni mwaka wa saba mfululizo
wa ushirikiano wetu pamoja na Shirika la Cardiostart International, wataalamu
hawa ni madaktari bingwa wanaotoa huduma katika kliniki maarufu za moyo nchini
Marekani hivyo kwa kufanya kazi nao tunapata ujuzi mkubwa”, alisema Dkt.
Angela.
Dkt. Angela alisema wataalamu hao
pia walileta vifaa tiba vya kisasa vilivyotumika wakati wa upasuaji kuwasaidia
wagonjwa kupata huduma bora na kupunguza gharama za matibabu.
“Kwa sasa JKCI ni kituo pekee kinachotoa
huduma za upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kwa viwango vya juu katika ukanda
wa Afrika Mashariki na Kati ambapo wagonjwa kutoka nchi jirani ikiwemo Zambia,
Zimbabwe, Malawi, Msumbiji, Comoro na zinginezo wamekuwa wakipatiwa huduma
katika Taasisi yetu”, alisema Dkt. Angela
Kwa upande wake Rais wa Shirika la Cardiostart
International la nchini Marekani Dkt. Miroslav Peev alisema mazingira mazuri ya
kutolea huduma yaliyopo JKCI ndio yanayowafanya wataalamu kutoka shirika hilo
kufika JKCI mara kwa mara kubadilisha ujuzi upande wa upasuaji wa moyo na
mishipa ya damu pamoja na mafunzo ya kuhudumia wagonjwa wa dharura na mahututi ili
kwa pamoja waweze kutoa huduma bora duniani kote.
Dkt.
Peev alisema wataalamu wa JKCI na wenzao kutoka hospitali nyingine walioudhuria
mafunzo ya kutoa huduma kwa wagonjwa wa dharura na mahututi wataenda kuimarisha
huduma za afya katika hospitali zao na ndani ya nchi wote wakiwa na lengo la
kusaidia kuokoa maisha.
“Wito wangu kwa watalaamu wa afya ambao wamepata mafunzo wakati wa kambi hii, muende kutumia mafunzo hayo ili kuweza kuwaokoa wagonjwa ambao wanamatatizo mbalimbali ya afya kwani wanapofika katika hospitali zenu wanakuwa na imani nanyi katika kuokoa maisha yao”, alisema Dkt. Peev
Naye daktari aliyepata mafunzo kupitia kambi hiyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Doto Sebastian aliwashukuru wataalamu kutoka Shirika la Cardiostart International kwa kuwapa ujuzi mpya katika kutoa huduma kwa wagonjwa wa dharura na mahututi pamoja na mafunzo kwa wataalamu wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu.
Dkt. Doto alisema mafunzo ya mara kwa mara kwa wataalamu wa afya yanawasaidia kupata utaalamu mpya lakini pia yanawasaidia kuweza kutoa huduma itakayoendana na maendeleo ya sayansi na teknolojia.
“Dunia ya sasa imebadilika kutokana na maendeleo ya
sayansi na teknolojia, kama utasoma tu darasani na kutoa huduma bila ya kupata
mafunzo ya mara kwa mara utaachwa nyuma ni muhimu wataalamu wenzangu wakisikia
kuna mafunzo ya kuongeza ujuzi wajitokeze ili wote tuwe katika mstari mmoja
wakati wa kutoa huduma”, alisema Dkt. Doto





Comments
Post a Comment