Naibu Katibu Mkuu Ntonda avutiwa na utoaji wa huduma za matibabu ya moyo mkoani Mbeya


Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Methusela Ntonda akizungumza na  Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Anna Nkinda kuhusu kambi maalumu ya upimaji na matibabu ya moyo inafanywa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya (MZRH) na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) katika mkutano wa 109 wa Wadau wa Elimu kwa Umma. Kushoto ni Meneja Uhusiano na Mawasiliano wa Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) Patrick Mvungi.

Afisa  Lishe wa  Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Maria Samlongo akitoa elimu ya lishe bora kwa wananchi waliofika katika viwanja vya City Park Garden vilivyopo jijini Mbeya kwaajili ya kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo zijulikanazo kwa jina la Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services. Huduma hizo zinazotolewa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya (MZRH) na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC).

***************************************************************************************************************************************************************************************************************************

  Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Methusela Ntonda ameipongeza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Hospitali ya Rufaa ya Kanda Mbeya (MZRH) kwa kutoa huduma za kibingwa za upimaji na matibabu ya moyo kwa wananchi.

Pongezi hizo amezitoa leo jijini Mbeya wakati akipewa taarifa ya kambi maalumu ya upimaji na matibabu ya moyo, huduma inayotolewa kwa washitiri wa mkutano wa 109 wa wadau wa Elimu kwa Umma ulioandaliwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) na wananchi wa mkoa wa Mbeya.

Ntonda alisema kutolewa kwa huduma za kipingwa za  uchunguzi na matibabu ya moyo kwa wananchi kutawasaidia kufahamu hali za mioyo yao na  kuchukuwa hatua mapema ya kujilinda kwa watakaokutwa wazima na wale wagonjwa kuanza matibabu mapema.

Akitoa taarifa ya upimaji huo Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Anna Nkinda alisema kwa siku moja ya jana (17/2/2025) waliona watu 139 kati ya hao watu wazima walikuwa 133 na watoto sita, waliohitaji kufanyiwa uchunguzi zaidi na kupewa rufaa ya kwenda kutibiwa JKCI walikuwa 12 kati ya hao watu wazima tisa na watoto watatu.  

Anna alisema ili kusogeza karibu huduma za kibingwa za matibabu ya moyo kwa wananchi taasisi hiyo ilianzisha huduma ya uchunguzi na matibabu kwa kuwafuata wananchi mahali walipo ijulikana kwa jina la tiba mkoba ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Outreach Services.

“Huduma tunazozitoa ni za vipimo vya awali vya magonjwa ya moyo vikiwemo vya kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi pamoja na mfumo wa umeme wa moyo , tunatoa elimu ya lishe, matumizi sahihi ya dawa za moyo pia tunawapatia wananchi vipeperushi vya lishe na kuufahamu ugonjwa wa shinikizo la juu la damu”, alisema Anna.

Kambi hiyo ya siku tano ya uchunguzi na matibabu ya moyo inayofanywa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, MZRH na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) inafanyika katika viwanja vya City Park Garden vilivyopo mkabala na uwanja wa mpira wa Sokoine jijini Mbeya.


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Wafanyakazi waliohama JKCI waagwa