Waingizaji na wasambazaji wa vifaa tiba wakutana mkutano wa kimataifa wa magonjwa ya moyo

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na wataalamu kutoka kampuni ya uingizaji na usambazaji wa vifaa tiba Kas Medics Limited alipotembelea banda la maonesho la kampuni hiyo wakati wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo unaofanyika Zanzibar.

Washiriki wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo wakipata elimu kuhusu matumizi ya vifaa tiba katika banda la maonesho la Bohari Kuu ya Dawa wakati wa mkutano huo unaondelea Zanzibar. 

Mwakilishi kutoka Kampuni ya Snibe Diagnostic Flora M. Kawa akiwaelezea wataalamu wa famasia kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) huduma zinazotolewa na kampuni hiyo wakati wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo unaofanyika Zanzibar.

Washiriki wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo wakipata elimu katika banda la maonesho la kampuni ya Bariki Pharmacy wakati wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo unaofanyika Zanzibar.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiwa katika picha ya pamoja na maafisa kutoka Benki ya CRDB baada ya kutembelea banda la Benki hiyo wakati wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo unaofanyika Zanzibar.

Picha na: JKCI

*******************************************************************************************************

Waingizaji na Wasambazaji wa vifaa tiba na dawa za binadamu kutoka kampuni mbalimbali duniani wameishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kuwakutanisha pamoja kuonesha bidhaa zao wakati wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo.

Mkutano huo unaofanyika kwa siku tatu katika hoteli ya Sea Clif & Spa iliyopo Zanzibar umewakutanisha wataalamu wa magonjwa ya moyo na wasambazaji wa vifaa tiba na dawa kutoka nchi 25 duniani.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hii kwa nyakati tofauti wataalamu hao wa vifaa tiba walisema maonesho hayo yamewakutanisha na watumiaji wa vifaa wanavyozalisha jambo ambalo limewasaidia kuzifahamu zaidi vifaa hivyo.

Meneja mauzo kutoka kampuni ya Novomed inayosambaza vifaa tiba nchini Michael Mchagi alisema kampuni hiyo imeshiriki katika mkutano huo kama mdau wa afya upande wa vifaa tiba na kuunga mkono jitihada za Serikali katika kutoa huduma bora za matibabu ya moyo kupitia Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Michael alisema kampuni hiyo imefaidika kupitia mkutano huo kwani imepata fursa ya kuonesha vifaa tiba kwa watoa huduma za afya pamoja na kukutana na wataalamu mbalimbali katika kada ya afya ambao kwapamoja wameweza kubadilishana ujuzi.

“Tumepata mapokeo mazuri kwa wataalamu waliotembelea banda letu, tumepata ahadi za kushirikiana kwa pamoja lengo likiwa kurahisisha upatikanaji wa vifaa tiba na kuboresha huduma za matibabu ya moyo nchini”, alisema Michael

Kwa upande wake Meneja mauzo kutoka kampuni ya Neusoft Medical System iliyopo nchini China Dkt. Kev Sheng alisema Kampuni hiyo imeshiriki katika mkutano huo upande wa maonesho ya bidhaa kama sehemu ya kuionesha dunia mashine za kisasa za Cathlab inazosambaza.

Dkt. Kev alisema ushiriki wao katika mkutano huo utawasaidia kutengeneza mtandao mkubwa na wataalamu wa afya kutoka sehemu mbalimbali duniani na kujenga mahusiano mazuri katika kuwasaidia wagonjwa wa moyo.

“Vifaa tunavyosambaza ni vya kisasa na kama vitawekezwa katika hospitali zetu vitasaidia kuboresha huduma na kuokoa maisha ya wagonjwa wa moyo”, alisema   Dkt. Kev

Naye Meneja kutoka Hospitali ya Andalusia Health Group iliyopo nchini Misri Dkt. Islam Samir alisema Hospitali hiyo imekuwa na ushirikiano na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) katika masuala mbalimbali ikiwemo kubadilishana ujuzi na kutoa huduma kwa wagonjwa wa moyo.

Dkt. Islam alisema Hospitali ya Andalusia ipo tayari kuwasaidia wagonjwa wa moyo waliopo Tanzania kupitia kambi mbalimbali za matibabu ya moyo pamoja na kubadilishana ujuzi na wataalamu wa afya.

“Kupitia mkutano huu wa magonjwa ya moyo tumeweza kujifunza kutoka kwa wenzetu wa mataifa mbalimbali lakini pia nao wameweza kuona ujuzi tulionao Afrika”, alisema Dkt. Islam

 

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)