Watu milioni 4.9 nchini husumbuliwa na magonjwa ya moyo

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimuelezea Makamu wa pili wa Rais Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla namna wanavyofanya upasuaji wa kubadilisha valvu ya moyo bila kufungua kifua wakati wa ufunguzi wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo uliofanyika jana mjini Zanzibar.

Afisa masoko kutoka kampuni ya Snibe Diagnostic Vonnie Feng akimuelezea Makamu wa pili wa Rais Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla huduma zinazotolewa na kampuni hiyo wakati wa ufunguzi wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo uliofanyika jana mjini Zanzibar.


 Kaimu Mtendaji Mkuu wa shirika lisilo la kiserikali Heart Team Africa Foundation (HTAF) Linda Gideon akimuonesha mmoja wa washiriki wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo bidhaa zinazouzwa na shirika hilo kwaajili ya kukusanya fedha za matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Makamu wa pili wa Rais Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akizungumza na wataalamu wa magonjwa ya moyo kutoka nchi mbalimbali walioudhuria mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika jana mjini Zanzibar.


Naibu Waziri wa Afya Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhe. Hassan Khamis Hafidh 
akielezea namna huduma za afya zilivyoboreshwa nchini wakati wa ufunguzi wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo uliofanyika jana katika Hoteli ya Sea Clif iliyopo mjini Zanzibar


Naibu Waziri wa Afya Mhe. Godwin Mollel akizungumza na wataalamu wa magonjwa ya moyo kutoka nchi mbalimbali walioudhuria mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika katika hoteli ya Sea Clif jana mjini Zanzibar.



Baadhi ya washiriki wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo wakisikiliza wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika jana katika hoteli ya Sea Clif iliyopo mjini Zanzibar

Makamu wa pili wa Rais Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla akiwa katika picha ya pamoja na kamati ya maandalizi ya mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo wakati wa ufunguzi wa mkutano huo uliofanyika jana mjini Zanzibar.

Na: JKCI

*******************************************************************************************

Imebainishwa kuwa magonjwa ya moyo na shinikizo la damu huchangia vifo takribani milioni 20 kwa mwaka duniani, idadi ambayo ni sawa na kupoteza wastani wa watu 50 kila siku.

Kwa takwimu za hapa nchini watu milioni 4.9 husumbuliwa na magonjwa ya moyo ambapo asilimia 13 ya vifo vyote nchini hutokana na magonjwa hayo.

Hayo yamesemwa jana na Makamu wa pili wa Rais Serikali ya Mapinduzi Zanzibara Mhe. Hemed Suleiman Abdull akimuwakilisha Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan katika ufunguzi wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo uliofanyika katika Hoteli ya Sea Clif iliyopo mjini Zanzibar

Mhe. Hemed aliwataka washiriki wa mkutano huo kushiriki na kutumia fursa waliyoipata kujumuika pamoja kutafuta mbinu za kuzuia na kudhibiti magonjwa ya moyo.

“Mkutano huu uwasaidie kujengeana uwezo na kuboresha nyenzo za utendaji kazi wenu ili muweze kukabiliana na ongezeko la magonjwa yasioyoambukiza ususani magonjwa ya moyo na mishipa ya damu”, alisema Mhe. Hemed

Mhe. Hemed aliwataka washiriki kupitia mkutano huo kuweza kuwa na majibu sahihi katika maeneo muhimu yenye changamoto upande wa udhibiti wa magonjwa, ujuzi katika uchunguzi, matibabu na uendelevu wa huduma mpya zinazopatikana nchini.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alimshukuru Rais Dkt. Samia  Suluhu Hassan kwa uwekezaji mkubwa alioufanya katika Taasisi hiyo pamoja na Rais Hussein Mwinyi kwa kuimarisha sekta ya afya Zanzibar.

Dkt. Kisenge alisema JKCI ilivyo sasa ni matokeo ya safari ya ubunifu iliyofanywa tangu mwaka 2015 safari ambayo sasa taasisi hiyo inafanya upasuaji wa tundu dogo kwa wagonjwa 3000 na upasuaji wa kufungua kifua kwa wagonjwa 800 kwa mwaka.

“JKCI ni miongoni mwa Taasisi bora barani Afrika kwa kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo, sasa tunaweza kufanya upasuaji wa kubadilisha valvu za moyo bila kufungua kifua “Tavi Procedure”, alisema Dkt. Kisenge

Dkt. Kisenge alisema kikao hicho cha magonjwa ya moyo kitawasaidia kushirikiana na wadau kwa pamoja kupata suluhisho la kuwasaidia wagonjwa wa moyo wanaowahitaji kutoka nchi mbalimbali duniani.

“Kupitia mkutano huu JKCI inaenda kuokoa Afrika katika masuala ya magonjwa ya moyo kwani sasa nchi za Afrika zinatutumia katika kutoa huduma za matibabu ya moyo kama vile Malawi, Zambia, Comora na hivi karibuni Burkina Faso itatutumia”, alisema Dkt. Kisenge 


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)