Bodi mpya ya ALMC–JKCI kuchochea maboresho ya huduma za Moyo Kaskazini


Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini Kati (DKAK) Dkt. Godson Abel Mollel,  Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge, Katibu Mkuu wa KKKT Dayosisi ya Kaskazini Kati (DKAK) Mwl. Solomon Loshilu Sambweti na wajumbe wa Bodi ya Wakurugenzi wakiwa katika  picha ya pamoja baada ya kikao cha kwanza cha bodi ya wakurugenzi wa Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) ambayo inasimamiwa JKCI kilichofanyika  katika ukumbi wa mikutano wa ALMC.

Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini (DKAK) Dkt. Godson Abel Mollel akizungumza wakati wa ufunguzi wa kikao cha kwanza cha Bodi ya Wakurugenzi wa Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) ambayo inasimamiwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kilichofanyika hivi karibuni jijini Arusha.

Katibu Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini Kati (DKAK) Mwl. Solomon Loshilu Sambweti akizungumza wakati wa kikao cha kwanza cha Bodi ya Wakurugenzi wa Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) ambayo inasimamiwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa ALMC.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza wakati wa kikao cha kwanza cha Bodi ya Wakurugenzi wa Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) ambayo inasimamiwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa ALMC.

Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini Kati (DKAK) Dkt. Godson Abel Mollel akisaini kitabu cha wageni alipotembelea hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) kwaajili ya kufungua kikao cha kwanza cha  Bodi ya Wakurugenzi  wa ALMC  ambayo inasimamiwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

******************************************************************************************************************************************************************************************************************

 Kikao cha kwanza cha Bodi ya Wakurugenzi wa Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) inayosimamiwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), kimefungua ukurasa mpya wa ushirikiano katika kuboresha huduma za moyo Kanda ya Kaskazini.

Kikao hicho kililenga kuweka mkakati wa kuhakikisha huduma za tiba zinakuwa bora zaidi na kuimarisha imani ya wananchi katika sekta ya afya.

Akizungumza wakati akifungua  kikao hicho jijini Arusha, Askofu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya Kaskazini Kati (DKAK) Dkt. Godson Abel Mollel alisema hatua hiyo ni ishara ya mwanzo mpya wa kuimarisha huduma za moyo kupitia ushirikiano kati ya taasisi hizo mbili.

Askofu Dkt. Mollel alisema bodi hiyo mpya yenye wajumbe sita imeundwa kwa uwiano wa pande zote mbili, ambapo wajumbe watatu wanatoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na watatu kutoka Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) ikiwa na jukumu la kusimamia menejimenti na mwelekeo wa kimkakati wa ushirikiano huo.

“Ushirikiano kati ya JKCI na ALMC ni baraka kubwa kwa wananchi wa Kanda ya Kaskazini. Kupitia bodi hii mpya tunaweka msingi imara wa kuboresha huduma za moyo, kuongeza uwajibikaji na kuhakikisha kila mwananchi anapata huduma za afya zenye ubora na utu. Tunaiomba jamii iendelee kuunga mkono jitihada hizi kwa manufaa ya taifa letu.”

“Tunaishukuru sana Serikali ya awamu ya sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kukubali kuwepo kwa ushirikiano huu kati ya JKCI na ALMC, tunamatumaini makubwa kuwa huduma zitakuwa bora zaidi kwa manufaa ya wananchi,”alisema Askofu Dkt. Mollel.

Askofu Dkt. Mollel alisema kupitia bodi hiyo, JKCI na ALMC wanatarajia kuimarisha zaidi huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali yakiwemo ya moyo, kuongeza matumizi ya teknolojia za kisasa pamoja na kuboresha mifumo ya utoaji wa huduma ili wananchi wapate tiba bora kwa wakati.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Dkt. Peter Kisenge alisema bodi hiyo itakuwa chombo muhimu cha usimamizi kitakachohakikisha huduma za afya zinazotolewa na hospitali hiyo zinakuwa bora zaidi kwa manufaa ya wananchi.

“Ushirikiano kati ya JKCI na ALMC ni hatua muhimu katika kuhakikisha tunatoa huduma bora za afya. Bodi hii itasimamia menejimenti ya hospitali hii ili iweze kutoa huduma za kiwango cha juu cha kimataifa na za kipekee kwa wananchi,” alisema Dkt. Kisenge.

Dkt. Kisenge ambaye pia ni daktari bingwa wa moyo na mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba aliongeza kuwa lengo la ushirikiano huo ni kuifanya ALMC  kuwa kituo cha  mfano katika utoaji wa huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa  mbalimbali  yakiwemo ya moyo Afrika Mashariki.

“Tunaamini kupitia ushirikiano huu tutapata ithibati ya kimataifa, jambo litakaloongeza imani ya wananchi katika kupata huduma za afya zenye ubora wa hali ya juu,” alisisitiza.

Mjumbe wa bodi hiyo Tosky Hans alisema kikao cha kwanza cha bodi hiyo kimeweka mikakati mahsusi ya kuboresha huduma za matibabu katika hospitali hiyo na kuhakikisha wagonjwa wanapata huduma bora zaidi.

“Tumeazimia kuifanya hospitali hii kuwa kituo cha mfano hususan katika huduma za matibabu ya magonjwa ya moyo ambazo hapo awali zilikuwa na changamoto katika mkoa wetu wa Arusha, tutahakikisha huduma hizi zinawafikia wananchi wengi zaidi karibu na walipo, bila kulazimika kusafiri umbali mrefu kutafuta huduma hizo”, alisema Hans.

Naye mjumbe mwingine wa bodi hiyo, Prof. Rogate Mshana  alisisitiza umuhimu wa kuimarisha elimu na huduma za moyo kwa manufaa ya wananchi wa Kanda ya Kaskazini na taifa kwa ujumla.

“Tumepewa dhamana ya kusimamia menejimenti mpya ili kuinua elimu na huduma za moyo. Huduma hizi zitakuwa na mchango mkubwa hata katika matukio makubwa ya kitaifa kama mashindano ya AFCON,” alisema Dkt. Mshana.

Bodi hiyo mpya inaundwa na wajumbe watatu kutoka upande wa Serikali kupitia JKCI na watatu kutoka Kanisa la KKKT. Itakuwa na jukumu la kusimamia na kuratibu shughuli za pamoja za hospitali hizo kwa lengo la kuhakikisha huduma bora za afya zinatolewa kwa Watanzania na wananchi kutoka mataifa jirani.

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na Burkina Faso zasaini makubaliano ya ushirikiano katika kutoa tiba ya magonjwa ya moyo

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi

Msumbiji kushirikiana na JKCI katika tiba ya moyo