Taasisi nne za Afya zashirikiana kuboresha huduma kwa wagonjwa
Wakurugenzi Watendaji kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
(JKCI) Dkt. Peter Kisenge, Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) Dkt. Delilah
Kimambo, Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) Balozi Ulisubisya
na Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) Prof.
Appolinary Kamuhabwa wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa
kikao cha ujirani mwema kuimarisha ushirikiano na kuboresha utoaji wa huduma kilichofanyika
leo katika Ukumbi wa MOI iliyopo jijini Dar es Salaam.
Viongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakisikiliza wakati wa kikao cha ujirani mwema kati ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kuimarisha ushirikiano na kuboresha utoaji wa huduma kilichofanyika leo katika Ukumbi wa MOI iliyopo jijini Dar es Salaam.
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Hospitali ya Taifa
Muhimbili (MNH), Taasisi ya Tiba ya Mifupa na Ubongo Muhimbili (MOI) na Chuo
Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) zimefanya kikao cha
ujirani mwema leo Ijumaa, Januari 23, 2026 jijini Dar es Salaam kwa lengo la
kuimarisha ushirikiano na kuboresha utoaji wa huduma kwa wananchi.
Kikao hicho kimewaleta pamoja wakuu wa taasisi hizo na baadhi
ya viongozi wa menejimenti, ambapo waliangalia kwa kina masuala ya uratibu wa
huduma, matumizi ya miundombinu ya pamoja na uimarishaji wa mawasiliano kati ya
taasisi.
Wajumbe wameweka mikakati ya pamoja itakayosaidia kuboresha
huduma kwa wagonjwa, hususan wale wanaohudumiwa katika taasisi jirani.
"Kwa kuwa taasisi zetu zipo eneo moja na wagonjwa wengi
wanahitaji huduma zinazohusiana, ni lazima tushirikiane kwa karibu ili
kuhakikisha wanapata huduma kwa wakati na kwa ufanisi," alisema Mkurugenzi
Mtendaji wa MOI, Balozi Dkt. Mpoki Ulisubisya.
Dkt. Peter Kisenge ambaye ni Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI
alisema kikao hicho kimewapa fursa ya
kujadili changamoto kwa uwazi na kuweka mikakati bora ya kuzitatua.
"Tumekubaliana kuimarisha mawasiliano na uratibu wa
huduma ili kupunguza usumbufu kwa wagonjwa na kuongeza ufanisi katika matumizi
ya rasilimali zilizopo," alisema Dkt. Kisenge.
Naye Mkurugenzi Mtendaji wa MNH, Dkt. Delilah Kimambo alisema
kwa kushirikiana kama taasisi jirani, wataweza kubadilishana uzoefu, kuboresha
mifumo ya rufaa na kuhakikisha mgonjwa anapata huduma sahihi kwa wakati
unaostahili.
Aidha Makamu Mkuu wa MUHAS, Prof. Appolinary Kamuhabwa
alisisitiza kuwa chuo hicho kinaendelea kuthamini ushirikiano na taasisi
jirani, jambo linalowawezesha kutoa mafunzo kwa wataalamu wa afya, kufanya
tafiti kwa pamoja na kuboresha utoaji wa huduma za vitendo.
Vikao hivi vya ujirani mwema hufanyika mara mbili kwa mwaka
ambapo kikao kijacho kitafanyika katika Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi
Shirikishi Muhimbili (MUHAS).



Comments
Post a Comment