RC Makala awaalika wakazi wa Arusha kupima Afya bure ALMC


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimpa zawadi mkuu wa mkoa wa Arusha Mhe. CPA. Amos Makala alipomtembelea ofisini kwake hivi karibuni kwaajili ya kumpa taarifa ya kambi maalumu ya upimaji na matibabu ya magonjwa mbalimbali inayofanywa na wataalamu wa taasisi hiyo Arusha Lutheran Medical Center (ALMC).


Mkurugenzi wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane akimsikiliza mkazi wa Arusha aliyefika Arusha Lutheran Medical Center (ALMC) kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kambi maalumu ya upimaji na matibabu ya magonjwa mbalimbali inayofanyika ALMC.


Afisa Muuguzi wa Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) Zawadi Kivuyo akimpima mkazi wa Arusha shinikizo la damu katika kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali yakiwemo ya moyo zinazotolewa katika kambi ya matibabu inayofanyika jijini Arusha.


 Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Emmanuel Lingindo akitoa elimu ya lishe kwa wakazi wa Arusha waliofika Arusha Lutheran Medical Centre (ALMC) kupata huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa mbalimbali yakiwemo ya moyo zinazotolewa katika kambi ya matibabu inayofanyika jijini Arusha.

********************************************************************************************************************************************************************************************
 Mkuu wa Mkoa wa Arusha Mhe. Amos Makala amewataka wakazi wa mkoa huo kujitokeza kwa wingi kupima afya zao katika kambi ya matibabu ya magonjwa mbalimbali inayofanyika katika Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Center (ALMC), akisema ni fursa muhimu kwa wananchi kupata huduma za matibabu karibu na makazi yao.

Akizungumza leo wakati wa mazungumzo yake na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge, aliyemtembelea ofisini kwake Mhe.Makala alisema kambi hiyo ni hatua chanya kwa wakazi wa Arusha na mikoa ya jirani kwani imepunguza ulazima wa wananchi kufuata huduma za matibabu mbali hususan jijini Dar es Salaam.

Kambi hiyo ya matibabu inatekelezwa na wataalamu wa JKCI kufuatia mkataba wa ushirikiano kati ya JKCI na Hospitali ya ALMC, unaolenga kusogeza huduma za kibingwa za magonjwa ya moyo pamoja na huduma nyingine maalum karibu na wananchi wa Kanda ya Kaskazini.

“Kuwepo kwa kambi hii ni faida kubwa kwa wananchi wetu kwani watapata nafasi ya kupata huduma kwa urahisi bila usumbufu wa kusafiri umbali mrefu,” alisema Mhe. Makala.

Aliongeza kuwa uamuzi wa JKCI kuisimamia Hospitali ya ALMC kwa kipindi cha miaka 20 utaongeza wigo wa upatikanaji wa huduma za afya, ikiwemo kuwahudumia wageni kutoka nje ya nchi wanaohitaji matibabu hatua itakayochangia kukuza utalii tiba katika Mkoa wa Arusha.

Mhe. Makala alisema Serikali ya Mkoa itaendelea kushirikiana na ALMC pamoja na wadau wengine wa sekta ya afya ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora, akisisitiza kuwa ushirikiano kati ya Serikali na mashirika ya dini katika utoaji wa huduma za afya umeanza muda mrefu na umeleta mafanikio makubwa.

Aidha, aliipongeza JKCI kwa kujitoa kwa jamii kwa kutoa huduma kwa wananchi wengi bila malipo, pamoja na kufanya maboresho ya miundombinu na huduma zinazolenga kuongeza ufanisi na ubora wa huduma za afya.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge  alisema tangu kuanza kwa kambi hiyo ya matibabu inayotolewa bila malipo yoyote jumla ya wananchi 500 wakiwemo watu wazima na watoto wamepata huduma za uchunguzi na matibabu.

Alisema kati ya wagonjwa hao 15 wamepata rufaa ya kwenda JKCI jijini Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu zaidi, huku watoto 36 wakifanyiwa uchunguzi wa moyo ambapo watoto watatu kati yao wanatarajiwa kufanyiwa upasuaji mkubwa wa kuziba matundu ya moyo.

Dkt. Kisenge ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo na mtaalamu wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo iliyoziba alisema kambi hiyo inalenga kutoa huduma za uchunguzi  na matibabu ya magonjwa mbalimbali ikiwemo ya moyo, ili kuhakikisha wananchi wanapata huduma za kibingwa karibu na maeneo yao bila kulazimika kusafiri umbali mrefu.

Akizungumza kuhusu kuanza rasmi kwa usimamizi wa JKCI katika Hospitali ya ALMC, Dkt. Kisenge aliwaomba wanahabari na wahariri kujitokeza Januari Mosi, 2026 kupima afya ya moyo bila malipo, akisisitiza kuwa wao ni wadau muhimu katika kutoa elimu ya afya kwa jamii.

“Tunawaalika wanahabari wa Arusha waje kujionea wenyewe kwa vitendo huduma zinazotolewa. Hospitali ya ALMC ni kitovu cha huduma za matibabu ya moyo na ni kivutio kikubwa cha utalii tiba,” alisema.

Alibainisha kuwa kuanzia Januari Mosi, 2026 JKCI itaanza rasmi kuendesha Hospitali ya ALMC kwa kipindi cha miaka 20, ambapo mitambo na mashine za kisasa zitasimikwa sambamba na matumizi ya teknolojia ya akili unde (Artificial Intelligence) katika kuimarisha huduma za afya.

Dkt. Kisenge alisema lengo kuu la ushirikiano huo ni kusogeza huduma za moyo karibu na wananchi wa Kanda ya Kaskazini, ikiwemo matumizi ya kifaa cha Dozee, shuka maalum inayomwezesha mgonjwa kufuatiliwa hali yake ya kiafya akiwa nyumbani ndani ya siku saba baada ya kufanyiwa upasuaji.

“Kwa kuwa JKCI itakuwa inaendesha hospitali hii, tutafungua na kuimarisha huduma za dharura pamoja na kusimika mtambo wa moyo, na matarajio yetu ni kwamba ndani ya miaka miwili ijayo tutaanza kufanya upasuaji wa moyo hapa hapa ALMC,” alisema.

Aliongeza kuwa hospitali hiyo inalenga kuwa hospitali ya kimataifa kwa kutumia teknolojia ya hali ya juu itakayowezesha kufuatilia mwenendo wa afya za wagonjwa hata baada ya kuruhusiwa kutoka hospitalini.

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na Burkina Faso zasaini makubaliano ya ushirikiano katika kutoa tiba ya magonjwa ya moyo

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi

Msumbiji kushirikiana na JKCI katika tiba ya moyo